Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Na mimi nianze kwa kuunga mkono hoja zote mbili ile ya Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji na ile ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajielekeza kwenye masuala mawili, suala la kwanza ni la korosho. Nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu na Waziri wa Kilimo, Mheshimiwa Dkt. Tizeba na Naibu wake Mheshimiwa Ole-Nasha kwa hatua walizochukua kwa tasnia ya korosho katika msimu huu wa korosho. Kuna mambo matano muhimu wametufanyia sisi wakulima wa korosho. Kwanza, walikuja Mtwara kushughulikia wezi waliohusika na ubadhirifu wa msimu wa mwaka 2014/2015 na walianza na Wilaya ya Masasi kukawa na changamoto kwamba hawakupewa support lakini hawakukata tamaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili baada ya kupata malalamiko yetu, Mheshimiwa Tizeba na timu yake waliamua kumuondoa Mrajisi wa Vyama vya Ushirika. Kiongozi huyu alikuwa ana viongozi wa AMCOS ambao walihusika na wizi na ubadhirifu wa msimu uliopita. Kwa hiyo, kwa ujasiri wake aliweza kumuondoa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Wizara hii katika kipindi kifupi cha msimu baada ya kuonekana kuna dosari ilithubutu kuvunja Bodi ya Korosho na kuisuka upya. Bodi hiyo mpya imeanza kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa na matunda yake tumeona msimu huu kwamba korosho imeuzwa hadi shilingi 4,000 kwa kilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, si hivyo tu baada ya kuona mabilioni mengi ya fedha yanapelekwa kwenye Mfuko wa Kuendeleza Zao la Korosho na hakuna kinachofanyika, Wizara hii chini ya uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Tizeba waliamua kusitisha shughuli zote za mfuko ule na shughuli zake zote kufanywa na Bodi ya Korosho. Hii sasa itasaidia kujipanga upya na kutekeleza majukumu ambayo kimsingi kwa muda wa miaka mingi walikuwa wanapata fedha nyingi lakini hawatekelezi chochote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini si hivyo tu, Wizara sasa imethubutu kuendesha mchakato wa kuhakikisha kiuatilifu muhimu au pembejeo muhimu kwenye zao la korosho sulphur dust kuagizwa moja kwa moja viwandani badala ya kuchukua kwa mawakala. Huu ni ujasiri mkubwa, kuna maneno mengi yamesemwa kwamba Waziri ana-interest na makampuni fulani lakini mti wenye matunda lazima upigwe mawe na kwenye vita ya mawe ya usiku ukiona mtu analalamika basi amegongwa jiwe. Kwa hiyo, hawa wanaolalamika kuna kitu walikuwa wanakipata kwenye mfumo wa ubadhirifu wa ununuzi wa hizo pembejeo, Mheshimiwa Waziri endelea na sisi wana Mtwara tunakuombea usiku na mchana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Wizara ina kazi kubwa tatu sasa hivi. Kazi ya kwanza wasimamie ujenzi wa viwanda vya korosho kwa sababu huu Mfuko wa Kuendeleza Zao la Korosho unapata zaidi ya shilingi bilioni 36 au 37 za export levy kwenye zao la korosho, lakini kwa miaka mingi hakuna kilichofanywa. Kwa hiyo, matarajio yangu sasa baada ya kazi hii kusimamiwa na Bodi ya Korosho tunaona sasa ujenzi wa viwanda vya korosho unaanza mkoani Mtwara na fedha ipo kwenye mfuko huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili kuna kiporo ambacho kimebaki. Tulikuwa tunasubiri taarifa ya ukaguzi ya COASCO. COASCO amekuja na taarifa kwamba msimu wa mwaka 2014/2015 kuna fedha zaidi ya shilingi bilioni sita hazikufika kwa wakulima. Taarifa ya TAKUKURU inaonyesha shilingi bilioni 30, taarifa ya Bodi ilionyesha shilingi bilioni 16; lakini juzi COASCO wamewasilisha taarifa kwamba kuna fedha shilingi bilioni sita zilitakiwa ziende kwa wakulima wa korosho lakini hazikwenda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni matarajio yangu sasa Wizara itaendelea na moto ule ule isimamie haki ya wakulima ili waliohusika na ubadhirifu huu hata kama mkubwa wa ngazi yoyote awajibishwe ili fedha hizi ziende kwa wakulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna AMCOS 34 kwenye taarifa ile ya COASCO inasema hazikukaguliwa, kwamba hakuna kitu kilichoandikwa kwa msimu mzima. Uzembe huu hapa unalindwa na Maafisa Ushirika. Kwa hiyo, ni matarajio yangu kwamba Mheshimiwa Waziri chini ya usimamizi wako na Mrajisi mpya aliyeteuliwa …
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.