Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Saed Ahmed Kubenea

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Ubungo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. SAED A. KUBENEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja hii.
Kwa ufupi sana, kwanza naunga mkono hoja ya Kamati iliyopo mbele ya Bunge lako Tukufu na pili, naunga mkono pia hoja iliyoletwa kwenye Bunge hili ya kuvunja RUBADA na kuleta shughuli zote za RUBADA katika Halmashauri ya Wilaya ya Rufiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, katika ripoti imeelezwa kwamba Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limekuwa linajenga nyumba na kuweka miundombinu ya umeme, maji na barabara na matokeo yake nyumba hizo zinazojengwa zimekuwa za gharama kubwa. Pamoja na wito wa Kamati wa kutaka Serikali na wadau wengine wachukue hatua za kuweka miundombinu ya maji na barabara katika maeneo ambayo miradi ya National Housing inapelekwa, lakini kuna jambo moja muhimu sana ni muhimu Bunge lako Tukufu hili likaazimia kwamba Shirika la Nyumba la Taifa linajenga nyumba mpya za kisasa ambazo zinauzwa kwa watu binafsi, lakini zipo nyumba katika nchi hii ambazo zimejengwa tokea wakati wa ukoloni na nyingine zimejengwa mwanzoni mwa uhuru zipo katika maeneo ambayo siyo ya biashara, lakini Shirikala Nyumba la Taifa halitaki kuuza kwa wapangaji walioishi katika nyumba zile kwa zaidi ya miaka 30.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nyumba hizo nyingine ziko Ilala Sharrif Shamba kwenye Jimbo lako la uchaguzi, nyingine ziko Temeke, nyingine ziko Ubungo na maeneo mengine mengi katika nchi hii. Kama Serikali inauza nyumba kwa wananchi wa kawaida, kwa wafanyabiashara wakubwa, kama shirika linaingia mikataba ni muhimu shirika hili likauza hizi nyumba kwa wakazi ambao wameishi katika hizo nyumba kwa zaidi ya miaka 20 au 30. Hili ni jambo muhimu sana kwa sababu litawasaidia wananchi wetu kupata nyumba za makazi. Tayari Serikali ilishakiri Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete akifungua nyumba mpya Iringa mwaka 2008 alikubali kwamba Serikali yake itauza nyumba zote hizo ambazo zinakaliwa na wananchi wa kawaida.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ripoti hii kuna suala zima la utalii, lakini Bodi ya Utalii haikutengewa fedha katika bajeti, Bodi ya Utalii haina fedha, Serikali imefunga kituo cha biashara, kituo cha utalii cha uwekezaji kilichopo London na imefunga kituo cha biashara kilichopo Dubai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo hivi vilikuwa vinafanya kazi ya kuutangaza utalii wa Tanzania nje ya nchi, lakini sasa vituo vimefungwa na utalii hauwezi kutangazwa tena. Vituo hivi vilikuwa vinatangaza mambo ya TANAPA, mambo ya Ngorongoro, Zanzibar Island, Mafia na maeneo mengine ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Leo Bodi ya Utalii haina fedha, utalii hautangazwi matokeo yake Mlima Kilimanjaro unaambiwa uko Kenya wakati uko Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bila uwekezaji, bila Serikali kuwekeza katika maeneo haya haiwezi ikapata faida, utalii unazalisha asilimia 17.5 ya bajeti ya Taifa, lakini Serikali imetupa utalii inasubiri Mwenyezi Mungu awaletee neema wakati neema haiwezi kuja bila kuwekeza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sana kwamba Bodi ya Utalii lazima ipewe fedha, ni lazima utalii utangazwe ili Taifa hili liweze kupata mapato mazuri kwenye utalii wetu. Bila kuweka fedha kwenye utalii wakati Serikali inafunga taasisi za utalii nje ya nchi hatuwezi kufika mbele, ni muhimu sana kwamba Bodi ya Utalii, Shirika la Utalii, Ngorongoro na kodi ya VAT kwa watalii iondolewe ili kuweza kuvutia watalii nchini, watalii waweze kuja wengi nchini na utalii uweze kutoa ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wetu wengi kabisa wametumbukia katika utalii lakini utalii katika…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)