Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa dakika tano na mimi nichangie hoja iliyopo mbele yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze moja kwa moja kwenye ukurasa wa 24 wa kitabu cha Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji hasa kwenye miradi mikubwa ya mabwawa nchini ambayo haijatekelezwa kwa muda mrefu. Kama kuna mradi ambao haujatekelezwa muda mrefu kuliko yote hapa nchini basi ni mradi wa Bwawa la Kidunda. Huu mradi wa Bwawa la Kidunda kabla ya uhuru mwaka 1955 ndiyo wazo hili lilianza na andiko lake la kwanza usanifu ulifanyika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya uhuru chini ya Serikali ya Awamu ya Kwanza ya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere mwaka 1962 akaubeba mradi huu akasema huu ndio ukombozi wa uchumi imara kwa sababu nchi yetu inategemea uchumi wake kwa kiasi kikubwa kwenye kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondokana na kilimo cha kutegemea mvua Bwawa hili la Kidunda lilikuwa ndio liwe mkombozi kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji lakini kwa ajili ya maji ya uhakika kwa Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani na Morogoro, ujazo wa wakati ule ulikuwa ukubwa wake zaidi ya cubic meter milioni 450, Serikali zote zilizokuja ziliendelea kuubeba mradi huu lakini haukuweza kutekelezwa kwa sababu ya ukosefu wa pesa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha ajabu kuanzia mwaka 1994 pamoja na mahitaji ya maji kuendelea kuongezeka mradi huu ulibadilishwa matumizi kutoka katika multiple use maana ya kwamba mahitaji ya binadamu, mifugo pamoja na umwagiliaji yakawekwa tu kwa ajili ya single use yaani matumizi ya binadamu na kupunguza ukubwa wa bwawa kutoka cubic meter milioni 450 mpaka 190, kwa kusikiliza tu wadau wa maendeleo wasiotutakia mema kwa ajili ya maendeleo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua wakati mwingine wadau wa maendeleo wakitaka kukuzuia wanaweza kukusingizia tu wakakwambia bwana hapo Selous hapo kuna nyoka hayupo ulimwengu mzima yupo hapo tu, mkilijenga hilo bwawa huyo nyoka atakuwa amepotea, na sisi tumekubali hiyo akili tukapunguza bwawa kutoka cubic meter milioni 450 mpaka 190. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kila nchi ulimwenguni sasa hivi inatanguliza maslahi ya wananchi wake zaidi kuliko ya mtu yeyote. Wamarekani wanasema Marekani kwanza, Waingereza wanasema Uingereza kwanza na Wachina wanasema China kwanza ni lazima tufanye maamuzi magumu katika hili ili tukubaliane na changamoto zinazotukabili nchini kwetu hasa ya ukame. Lazima turudi kwenye usanifu wa awali wa ule ujazo wa 450 milioni badala ya huu wa 190 tu kwa ajili ya matumizi ya binadamu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali tuende na andiko lile la asili ambalo liliandikwa tangu mwaka 1955 wakati ule hata mahitaji ya maji yalikuwa machache sana kuliko sasa hivi mahitaji ya maji ni makubwa zaidi, hata Mto Ruvu unaanza kupungua maji hususan wakati wa kiangazi. Kwa hiyo, hili Bwawa la Kidunda utekelezaji wake ndiyo utakuwa ni uokozi kwa ajili ya uchumi wetu kama tunavyojua Dar es Salaam tunaitegemea zaidi ya asilimia 75 kwa uchumi wa nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa pili kwa Serikali ni kwa sababu miaka yote 62 mradi huu haujatekelezwa shida kubwa ni fedha. Leo hii kule Mkulazi ndiyo kinajengwa kiwanda kikubwa kuliko chote cha sukari kupitia kampuni ya Mkulazi Holding, lakini kwa tatizo la maji huu mradi hautatekelezeka. Bwawa hili ni lazima lijengwe ndiyo huu mradi wa Mkulazi nao u-take-off.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.