Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Amina Nassoro Makilagi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. AMINA N. MAKILAGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.
Lakini vilevile nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kusimama na kuweza kuchangia
katika hoja hii muhimu iliyo mbele yetu katika sekta hizi muhimu za miundombinu na nishati.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nianze kwa kukipongeza Chama cha
Mapinduzi kwa kutimiza miaka 40 kwa kuzaliwa kwake kwa mafanikio makubwa sana katika
kuwaletea wananchi maendeleo, ikiwemo miundombinu ya barabara, reli, mawasiliano ya simu
na bandari na kadhalika. Maana ni ukweli usiopingika kwamba kabla ya miaka 40 ya Chama
cha Mapinduzi, hali yetu haikuwa namna hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kukishukuru Chama cha
Mapinduzi na ninaomba kukitakia kila la heri katika miaka mingine 40, kiendelee kutekeleza Ilani
yake na miaka mingine 40 tuwe tumefika mbele zaidi kuliko ilivyo sasa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nichukue nafasi hii kuwashukuru wananchi wote wa
Tanzania walioshiriki katika uchaguzi wa kata 19 katika chaguzi ndogo za Madiwani na uchaguzi
mdogo wa Jimbo la Dimani ambako Chama cha Mapinduzi kiliibuka mshindi wa kishindo kwa
kupata kata 18 na Jimbo la Dimani Chama cha Mapinduzi kilipata 75%. Kipekee nichukue nafasi
hii kuwashukuru wananchi wa Tanzania na ninaomba niwaambie kwamba imani huzaa imani
na leo tunazungumzia suala la miundombinu ya barabara, tunazungumzia mawasiliano ya simu,
tunazungumzia suala la nishati vijijini, waendelee kuwa na imani na CCM, yote tuliyowaahidi
kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi tutayatekeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya utangulizi huo naomba sasa nijielekeze
kwenye mambo machache niliyoyachagua kuyatilia mkazo. Jambo la kwanza naomba
niwakumbushe Wabunge kwamba katika bajeti ya mwaka huu wa fedha 2016/2017 Bunge la
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha fedha nyingi sana kwa ajili ya maendeleo ya
miradi ya barabara, reli, nishati na kadhalika. Lakini kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa hali
inaonekana kwamba fedha hazipelekwi kwenye miradi kama ilivyokusudiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua nafasi hii kuishauri Serikali, kwa sababu
inabana matumizi katika kuendesha shughuli zake, inakusanya mapato, imebuni vyanzo vipya.
Ninachoiomba Serikali fedha hizo zilizotengwa na Bunge kwa ajili ya miradi ya maendeleo
ninaomba ipelekwe ili miradi iweze kutekelezwa kama ilivyokusudiwa kwa sababu, nimepitia
ripoti za Kamati mbalimbali zilizowasilishwa, Kamati ya Miundombinu kabisa inaonekana hata
30% bado hawajafikia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimejaribu kutazama Kamati ya Nishati na Madini kiwango
kilichopelekwa ni zaidi ya 25% tu. Ninaiomba Serikali na kwa kweli na Waziri wa Fedha yuko
hapa, hebu tujipange vizuri kupeleka fedha za maendeleo katika miradi iliyokusudiwa kwa
sababu kama haikupelekwa fedha hata kama Mawaziri ni hodari namna gani, hata kama
watendaji ni hodari namna gani hatutafikia lengo lililokusudiwa.
Naomba Serikali ibuni mipango mipya ya kuhakikisha fedha za miradi ya maendeleo
zinapelekwa ili miradi yote iliyokusudiwa iweze kutekelezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Serikali kuna miradi mingi ya maendeleo ya
miundombinu ya barabara, miundombinu ya reli na miundombinu mingine, na hasa hapa
nizungumzie ya barabara. Kuna miradi mingi iliyoanzishwa mwaka 2010 haikukamilika, 2011
haikukamilika na sasa hivi tuko mwaka 2017 miradi ya baadhi ya barabara haijakamilika na
alipomalizia Mheshimiwa Mipata na hapa nitoe mifano ya barabara za Mkoa wa Mara.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninafurahi sana Waziri wa Miundombinu juzi amekwenda na
amejionea mwenyewe zile barabara hali yake ilivyo, inasikitisha. Barabara ya kutoka Makutano,
Butiama kwa Baba wa Taifa, barabara ya kutoka Butiama kuelekea Mugumu mpaka Loliondo,
mpaka Mto wa Mbu, kwa kweli ni hatari. Ile barabara tangu imeanza kujengwa hakuna
kinachoendelea, Mheshimiwa Waziri amekwenda amejionea kuna wakandarasi wazalendo
zaidi ya 10 wanajenga ile barabara, mimi nimekata tamaa kwa sababu ninachokiona sasa hivi
ni kuchimba tu udongo wanaleta barabarani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ile ni barabara ya kihistoria, ni barabara aliyopita
Baba wa Taifa kudai uhuru wa nchi hii, ni barabara ambayo hatupaswi kupiga kelele namna
hiyo, Mwalimu Nyerere aliangalia Watanzania wote bila kujijali yeye mwenyewe, leo barabara
ya kutoka Butiama kuelekea nyumbani kwake, kwenda Mugumu, kwenda mpaka Loliondo,
kwenda mpaka Arusha ili kufungua barabara wananchi wa Mkoa wa Mara na hasa ukizingatia
kuna mbuga ya wanyama ya Serengeti, kuna ziwa, kuna uchumi uliotukuka, lakini barabara hii
kwa kweli sasa inatuchonganisha kwa wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumejaribu kuzungumza, wananchi wa Mkoa wa Mara wana
imani na CCM, wamechagua CCM, lakini barabara hii sasa inawafanya wanaanza kujenga
wasiwasi.
Ninaomba hatua zichukuliwe, kama Serikali imekuwa ikichukua hatua kwa makandarasi
wabovu, makandarasi ambao wako tayari naomba na hatua zinazostahili huyu mkandarasi
anayejenga hii barabara atazamwe upya, je, anao uwezo? Kwa sababu nimefuatilia fedha
ameshalipwa, ni kwa nini hajengi hii barabara? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sio barabara hii peke yake, barabara zote za ule mkoa haziko
sawasawa. Barabara ya Kisorya - Bunda mpaka hapo Mugumu kupita Nyamuswa mpaka
Serengeti haiendelei! Barabara zote ambazo kwa kweli zimetengewa fedha na zilipitishwa
kuanzia mwaka 2010 hakuna kinachoendelea.
Naomba Serikali hebu ichukue hatua za haraka ili Mkoa wa Mara na wenyewe ufunguke
kwa sababu, ni mkoa wa kiuchumi. Na ukifunguka kuanzia kule Ukerewe mpaka Mara uchumi
wa samaki, uchumi wa madini, uchumi wa mbuga za wanyama na kadhalika. Hata Kaburi la
Baba wa Taifa ni uchumi, maana watalii wanakuja kuangalia kaburi, lakini hawana pa kupita
kwa ajili ya uchumi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nizungumzie suala zima la fedha za Mfuko wa
Barabara (Road Fund). Nimefuatilia kitabu hiki kunaelekea kuna tatizo, hizi fedha pia hazitoki.
Sasa ningependa tutakapokuwa tuna wind up, hebu Waziri atuambie tatizo ni nini? Maana hii
fedha iko kwenye ringfence, hazitakiwi zitoke. Kwa nini haiendi kuhudumia Mifuko ya Barabara
Vijijini, kumetokea kitu gani? Barabara hazipelekewi fedha, barabara zimeharibika tena ni za
vumbi zinazounganisha vijiji na vijiji, kata na kata, lakini hazijengwi kwa Mfuko wa Barabara.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nitoe ushauri, kwa sababu zimekuwa zikitengwa fedha
nyingi na Watanzania wanakatwa kodi kwa ajili ya kuimarisha hizi barabara za vijijini, barabara
zinajengwa na baada ya muda mfupi mvua ikinyesha barabara zinabomoka. Ushauri
ninaoutoa hebu tuangalie sasa mbinu mpya, badala ya kuwa tunajenga barabara za vumbi za
changarawe na kila baada ya mwaka barabara inaondoka na fedha inapotea hebu twende
na mpango mpya sasa wa kujenga hata lami kwa kilometa hata tano, tano. Tunajenga kitu
cha kudumu, kuliko mabilioni ya fedha yanateketea na baada ya muda barabara inaondoka,
halafu sasa tunatenga nyingine kila mwaka. Hebu naomba tubadilike tujaribu kutumia
wataalam wetu wa barabara, hebu watushauri at least tujenge kila kata kilometa tano, tano ili
tuweze kupata matokeo ya haraka na ya mapema. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala zima la upanuzi wa Bandari ya Dar
es Salaam. Nimefurahishwa na maoni ya Kamati yaliyo kwenye ukurasa wa 35 mpaka ukurasa
wa 40. Nayaunga mkono kabisa, na hapa naishauri Serikali na Mamlaka inayohusika, hebu
chukueni ushauri walioutoa Kamati ya Miundombinu muufanyie kazi. Ile gati ya kwanza mpaka
ya saba zipanuliwe, lakini na ile gati ya 13 na yenyewe ijengwe ili Dar es Salaam ipanuke na
meli ziweze kuja za mizigo, zinashusha mzigo kwa haraka na uchumi uweze kukua kwa haraka.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na hapa nishauri, hebu tuangalie na Bandari ya Bagamoyo,
ilikuwa kwenye mpango mzuri na maendeleo yalishafikia hatua nzuri, lakini mimi sioni kama
inazungumzwa na sioni kinachoendelea. Bandari ya Bagamoyo ingejengwa kama ambavyo
tulikusudia na kama ambavyo tuliweka kwenye mpango, nina imani uchumi wa haraka katika
nchi yetu ungeweza kupatikana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nishauri tujenge na bandari ya Tanga kwa sababu,
Bandari ya Tanga itatuimarisha zaidi maana itawezesha nchi mbalimbali na ikiwemo na Bandari
ya Musoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.