Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia
nafasi hii adhimu ili nami niweze kutoa mchango wangu katika hotuba za Kamati zetu mbili za
kudumu za Bunge; Kamati ya Nishati na Madini na Kamati ya Bunge ya Miundombinu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi hii ili kwa namna moja au nyingine,
niweze kwanza kuipongeza Serikali yetu kupitia Wizara hizi mbili pia. Wizara ya Nishati na Madini
imefanya kazi kubwa, nzuri na ya kutukuka kwa Taifa letu hili la Tanzania; tumeona juhudi zilivyo
nzuri katika kuhakikisha kwamba umeme unapatikana katika Taifa letu na umeme wa uhakika.
Kwa hiyo, naomba tu kwa kweli Serikali kupitia Hazina, itoe pesa kwa wakati katika miradi
mbalimbali ambayo imeletwa na Wizara hii ndani ya Bunge lako na kuidhinishwa ili ikapate
kutekelezwa katika mwaka unaohusika.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni Wizara hii pia ambayo imeonesha kwa mfano kabisa,
kuwachukua Watanzania wenzetu na kuwapa full scholarship katika Mataifa mbalimbali
kuweza kujielimisha na kupata taaluma muhimu katika Sekta mbalimbali za Nishati na Madini
katika Taifa letu. Nina imani baada ya muda siyo mrefu, Tanzania itakuwa na wataalam
waliobobea wa hali ya juu na Taifa letu litapata manufaa makubwa katika sekta hizi zote mbili.
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Wizara ya Nishati na Madini ijitahidi sana kuisimamia
Sekta ya Umeme nchini, maana hii ndiyo injini ya mapinduzi ya viwanda kule ambako
tunatarajia kwenda. Kwa sababu umeme unapokuwa unapatikana katika bei ambayo ni
ndogo, tunaamini kwamba tunaweza tukavutia wawekezaji wa ndani na nje kwa urahisi zaidi.
Hata katika Wakala wa Umeme Vijijini, napendekeza Serikali iendelee kutoa pesa kwa wakati ili
hata hii REA Phase III iweze kutekelezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona kwa macho yetu wote kwamba Tanzania imepiga
hatua katika usambazaji wa umeme katika maeneo mbalimbali vijijini na naomba tu kwamba
ule mtandao wa umeme vijijini uendelezwe zaidi. Pale ambapo tumefika, kasi iongezwe zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa miundombinu, napo tuongeze jitihada katika
kuhakikisha kwamba Reli ya Kati inaendelezwa. Naipongeza kwanza Serikali kwa kuingia
mkataba na Waturuki kutaka kujenga hii Reli ya Kati kwa kiwango cha standard gauge.
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini Serikali yetu kwa dhamira ya dhati ya Rais wetu,
Mheshimiwa Dkt. Joseph Pombe Magufuli tutafika kule ambako tunatarajia ili tuweze kuwa na
treni ambazo zinaweza kwenda mwendo kasi; bullet train, tuweze kuzipata katika Tanzania hii,
watu na vitu viweze kufika mahali panapostahili kwa wakati.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua kabisa kwamba Taifa la Tanzania tumejaliwa kuwa
katika eneo ambalo kijiografia linatupa nafasi nzuri ya kuweza kuwa tegemeo katika ukanda
wetu wa Afrika Mashariki na Afrika ya Kati. Kwa maana hiyo, upanuzi wa bandari zote; ya
Tanga, Dar es Salaam, Bagamoyo pamoja na kule Mtwara ni bandari ambazo ni za muhimu
sana. Ni muhimu kabisa Tanzania ikawa na kipaumbele cha peke yake katika hizi bandari, kwa
sababu zote zinategemewa. Bandari ya Mtwara, Mataifa ya Msumbiji, Malawi hata Zimbabwe
wanaweza wakaitumia bandari hii. Kwa maana hiyo, ile reli ya kutoka Mtwara mpaka
Mbambabay ni ya muhimu sana kwa sababu itakuwa na matokeo mazuri sana katika ukuzaji
wa uchumi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Reli ya Kati inaunganisha Bandari ya Dar es Salaam na nchi hizi
za Zaire kwa maana ya DRC, Rwanda na Burundi pamoja na Nchi ya Uganda. Bandari ya
Tanga imeteuliwa kabisa na nchi ya Uganda na kwa maana hiyo, ujenzi wa reli ya kutoka
Tanga - Arusha mpaka Musoma na yenyewe ni muhimu ikapewa kiaumbele.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, niseme kabisa kwamba Taifa letu la Tanzania
katika mchango wake wa kuleta uhuru katika Mataifa mbalimbali ya Afrika, bado inayo nafasi
nzuri tena katika kuchangia ukuzaji wa uchumi katika Mataifa yote haya ya Afrika ambayo
Tanzania yenyewe ilishiriki katika kuyaletea uhuru.
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme dhahiri tu kwamba kwetu huko Geita ni sehemu
ambayo tunayo madini ya dhahabu. Naishauri Serikali ifanye kila linalowezekana kuharakisha
kuhakikisha kwamba wachimbaji wadogo wadogo katika maeneo ya Wilaya yetu ya Mbogwe
na wachimbaji waliotapakaa katika Mkoa wa Geita, wapate kutengewa maeneo ya kufanya
shughuli zao za uchimbaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema maneno haya, nakushukuru kwa mara
nyingine kwa kunipatia nafasi hii. Ahsante sana.