Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru ningeomba kuchangia kuhusu hoja ya Kamati na kwanza niseme kabisa kwamba Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia sana kuhusiana na masuala ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ambayo ni kielelezo tosha kabisa kuhusu namna suala la Kilimo, Mifugo na Uvuvi lilivyo na kipaumbele kwa Watanzania wengi ndiyo maana Wawakilishi wa wananchi wameweka mkazo katika kulizungumzia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja za Wabunge ziko nyingi kwa vyovyote vile kwa dakika tano sitaweza kuzipitia zote lakini kwa ujumla wake, Waheshimiwa Wabunge wameonesha moja; kwamba kuna haja ya kuongeza bajeti ya kilimo kuliko vile ilivyo sasa ili iweze kuakisi umuhimu wa sekta hii katika jamii. Kimsingi Serikali inakubaliana na hili na nafikiri Waheshimiwa Wabunge tutashirikiana nao tunavyoelekea katika bajeti inayokuja ili kuona kwamba bajeti ya Kilimo inaongezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia sana kuhusu suala la pembejeo katika maana ya ubora, kufika kwa wakati kwa wakulima lakini vilevile kuhusu bei ambayo inaweza ikahimilika kwa wakulima wengi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara imejipanga kukabiliana na changamoto hii ya pembejeo na tunafikiria tuko mbioni kuanzisha utaratibu ambao mbolea inapatikana kwa utaratibu wa bulk procurement kama utaratibu ulivyo wa sasa wa mafuta unaofanywa na EWURA. Kimsingi tunaamini kwamba kama tunaweza kuta-subsidies kutoka kwenye source inakuwa ni rahisi Watanzania wote kupata mbolea kwa bei moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunaamini kwamba, gharama ya sasa ya juu iliyopo katika mbolea na baadhi ya pembejeo ni suala vilevile linalosababishwa na tozo na kodi ambazo zimewekwa katika bidhaa hizi. Kwa hiyo, vilevile tutaomba Bunge lako, tutakuja na mapendekezo ya namna ya kuondoa kodi, tozo na ada mbalimbali ambazo zinaendelea kuchangia pembejeo iwe bei ya juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile Serikali bado ipo kwenye mkakati wa kuhakikisha kwamba mbolea inazalishwa ndani. Tunaamini kwamba bei kubwa iliyopo ya sasa ya mbolea ni suala vilevile la kwamba ni gharama kwa sababu tunaagiza kutoka nje kwa hiyo tukiwa na viwanda vya kuzalisha mbolea ndani tunaamini kwamba itatusaidia kupunguza bei.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imezungumzwa vilevile suala la ukame na uhaba wa chakula. Hili tulishalitolea ufafanuzi katika Bunge hili lakini niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba kutokana na tathmini ya kina ambayo Serikali imefanya, Serikali inaamini kwamba tumejizatiti vya kutosha vya kuhakikisha kwamba hamna Mtanzania atakayekufa na njaa na nimhakikishe tu Mheshimiwa Lwakatare ambaye yeye keshasema watu watakufa njaa mwezi wa tatu, kwamba, Serikali itahakikisha hili halitokei, tumeweka mikakati ya kufuatilia kuhakikisha Watanzania wanakuwa na usalama wa chakula.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la migogoro kati ya wafugaji na wakulima; Hili nalo limevuta hisia ya Waheshimiwa wengi. Kimsingi kama Serikali tunakubali kwamba hili ni eneo ambalo matokeo chanya na ya haraka yanahitajika kutokea kwa sababu migogoro hii imeongezeka. Tunavyozungumza tayari Serikali ina Tume ambayo inazunguka nchi nzima kupitia migogoro yote ili kuweza kutoa mapendekezo ambayo tunaamini kwamba yakifanyiwa kazi kwa kiasi kikubwa tunaweza tukaondoa migogoro hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wamezungumzia vilevile kuhusiana na suala zima la haja ya kuongeza jitihada katika kufanya kilimo cha uwekezaji. Wizara imelipokea hili tunaamini kwamba ni kweli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya machache nashukuru sana na naomba kuunga mkono hoja.