Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuishukuru sana Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa inayoongozwa chini ya Uenyekiti wa Mheshimiwa Jasson Samson Rweikiza na Makamu Mwenyekiti wake Dkt. Pudenciana Kikwembe pamoja na wajumbe wote kwa ujumla akiwepo Mzee wangu Lubeleje, Mbunge wa Mpwapwa na Mheshimiwa Mwanne Mchemba. Tunawashukuru sana kwa namna mnavyotupa ushirikiano na mara zote mmekuwa ni walezi wetu na kusema kweli Kamati hii tunafanya nayo kazi vizuri sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote kwa ujumla kwa michango mizuri kupitia kazi hii ya Kamati iliyofanyika kwa muda wa miezi 12. Kazi hii ni kubwa na mambo mengi wameyasema. Nitangulize tu kusema kwamba yote tumeyapokea na tumeyachukua na tutayafanyia kazi yote kwa ufanisi na kwa ufasaha mkubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yaliyosemwa ni mengi lakini siyo rahisi kwa muda niliopewa kuweza kuyajibu yote na kwa kuwa wajibu wangu na mimi ni kuchangia, basi nitumie nafasi hiyo kusema baadhi ya yale tu ambayo naona yamesemwa sana na watu wengi na mengine haya tutaendelea na mfumo ule wa Kanuni za Kudumu za Bunge kuendelea kufanya kazi kwa pamoja ili tuweze kuyamaliza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo kubwa na la kwanza ambalo limesemwa sana na wote ni namna ambavyo Wakuu wetu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wanavyohusiana katika kufanya kazi ya umma na kuleta maslahi tunayoyatarajia wote. Imesemwa hapa kunakuwa na misuguano katika baadhi ya maeneo ya Wilaya na Mikoa kati ya viongozi hawa wa kiserikali na viongozi wawakilishi wa wananchi kwa maana ya viongozi wa kisiasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa tofauti zao ukiondoa udhaifu wa baadhi ya wengine ambao ni hulka zao na hapa ndiyo maana inasemwa hata habari ya semina elekezi. Siku za nyuma mambo ya semina hizi yalilaumiwa sana na kupingwa kweli kweli kwamba semina elekezi, semina elekezi. Tukasema tutoke kwenye semina elekezi as long as mtu ana CV nzuri amesoma, akipewa vitabu vya kufanyia kazi lakini wakati anapoteuliwa akaelekezwa naamini atafanya kazi vizuri kama ana hekima na busara kwa sababu naamini suala la uongozi siyo tu kuwa na PhD, Masters au First Degree pia hekima ni kitu cha msingi sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu hizi zinatusaidia tu kujua vitu lakini hekima inatusaidia kujua useme na ufanye nini kwa wakati gani. Kwa hiyo, nitoe rai na niwasihi sana baadhi ya wenzetu hawa Wakuu wa Mikoa na Wilaya wajitahidi pamoja na kuzingatia sheria, kanuni na taratibu lakini pia wawe na hekima na busara kwa sababu sasa wao ni viongozi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili katika hili wakati mwingine na wao kama binadamu wanakuwa tempted, anatokea kiongozi anasema mimi ni mwakilishi wa wananchi bwana, huwezi kuniambia kitu na unamwambia kiongozi mwenzio vile na yeye atakwambia anavyoweza kusema. Ndiyo maana yanatoka majibu kama yale na mimi ni mteule wa Rais, ni kwa sababu kulikuwa kuna reaction fulani iliyopelekea na yeye akawa excited akafikia hatua hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nitoe rai kwa sote, sisi kama viongozi wa kisiasa na viongozi wengine wote, tunapokwenda mbele ya jamii basi tusichukue nafasi hiyo ya kutambiana kwamba mimi ni nani, mimi ni nani, bali wote tujitahidi kuwa waadilifu na kujua kwamba nafasi zetu ni kubwa kwa jamii. Wakati mwingine ni mambo ya mahusiano tu, unamkuta Mbunge au Diwani, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya iko pale au ya Mkuu wa Mkoa iko pale hajawahi kwenda hata siku moja ku-pay courtesy call, wanakutana kwenye matukio. Hili si jambo jema kwa sababu pia viongozi hawa sheria imewapa madaraka na mamlaka makubwa tu na kwa sababu ya muda sina haja ya kuisema. Niwasihi na niwaombe viongozi wenzangu kwamba wale ni viongozi wenzetu tushirikiane nao, tufanye kazi nao pamoja kwa faida yetu sote lakini kwa maslahi mapana ya wananchi wetu na kwa nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine la pili lililoguswa sana ni kwamba flow ya fedha kwenda kwenye shughuli za Mamlaka ya Serikali za Mitaa si nzuri sana. Takwimu za Kamati zinaonesha kwa utafiti walioufanya na ambao na sisi tunao ni kwamba 85% zimekwenda kwa ajili ya maendeleo, kwa hiyo utaona ni 15% ndiyo haijaenda na bado tuna miezi kadhaa hapa, nadhani tunaweza tukafikia hatua nzuri ya 100% kwenye fedha za maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye OC zimekwenda 46% kwa fedha iliyotoka Serikali Kuu lakini sehemu ya OC pia ni pamoja na own source. Makusanyo ya ndani ya Halmashauri na yenyewe ni sehemu ya OC. Kwa hiyo, niwasihi sana Waheshimiwa Wabunge tuyasimamie sana makusanyo ya ndani ili yaweze kutusaidia kutekeleza majukumu mengine ambayo yangeweza kutekelezwa na OC ile ambayo imepungua iliyotakiwa kuletwa na Serikali Kuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tufahamu kwamba mahusiano ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa na Serikali Kuu huwezi kuyaachanisha kwa sababu kwa nature yake Serikali Kuu ndiyo imezaa Serikali za Mitaa na Serikali Kuu kazi yake ni kuzilea Mamlaka za Serikali Mitaa. Tunahitaji mishahara, tunahitaji fedha za maendeleo ambazo Serikali Kuu inatafuta na Mamlaka za Serikali za Mitaa ni lazima zitimize wajibu wake kuhakikisha kwamba zinatunza fedha za makusanyo na kuhakikisha kwamba zinaenda kwenye maendeleo pia kwa maana ya sehemu ile ya usimamizi wa miradi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko Mamlaka za Serikali za Mitaa nyingine ambazo hata pamoja na kukusanya own source kubwa tu inayofikia kwa mwezi hata zaidi ya milioni 100 ambayo ni kiwango kidogo, ziko zinazokusanya mpaka bilioni moja kwa mwezi, zinashindwa kuwalipa hata posho za vikao halali Madiwani. Huku ni kugombanisha Serikali Kuu na Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa maana ya Madiwani. Kwa sababu haiwezekani wewe umekusanya fedha, kikao kile kwa mwezi kinatakiwa kifanyike kwa chini ya shilingi milioni 20, wewe unazipeleka kwenye matumizi mengine mnapeana likizo, mnapeana safari watumishi, Wakuu wa Idara wanapeana safari zinatumika zinakwisha halafu wanasema Serikali haileti OC ndiyo maana hatuwalipi posho za vikao. Kuanzia sasa Halmashauri ambayo itawakopa Madiwani huyo Mkurugenzi hana sifa ya kuendelea kuwa Mkurugenzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine lililosemwa sana ni suala la mihuri ya Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji. Nilikwishalisema, Wenyeviti hawa wa Mitaa na Vijiji mbali ya masuala ya ulinzi na usalama lakini mihuri yao ile ndiyo inayowatambulisha kwa wananchi wao wanaowaongoza. Mihuri yao ile ndiyo inayowafanya watu wamalizane katika mahusiano ya mikataba midogo midogo katika maeneo yao. Ni lazima mamlaka za juu ziheshimu madaraka na majukumu waliyopewa hawa viongozi wa chini, Wenyeviti wa Mitaa na Wenyeviti wa Vijiji na hata Wenyeviti wa Mashina. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kitendea kazi hicho ni muhimu kwao na vizuri wakaachiwa na ndiyo maana nilisema warejeshewe na hii niliisema siyo kwa Dar-es-Salaam ni kwa nchi nzima. Viongozi hawa nchi nzima warejeshewe kitendea kazi hiki ili wafanye kazi yao vizuri. Ndiyo wanaotambulisha mgeni anapoingia au kutoka kwenda sehemu nyingine lakini ndiyo wanaoandika vibali hata vya mifugo, mfugo ukauzwe hapa na ndiyo wanaosababisha kule chini kunakuwa na amani na utulivu, lazima tuwape nafasi yao hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ma-WEO na ma-VEO ambao hawajaajiriwa na Serikali Kuu haitatokea hata siku moja kwa idadi ya vijiji tulivyonavyo tukatimiza idadi yao kutokana na watumishi wa umma tulionao na changamoto tulizonazo za upungufu katika idara mbalimbali. Niendelee kusisitiza kwamba Mamlaka ya Serikali za Mitaa ni mamlaka kamili zinazoweza kuamua kutafuta watu wa kuwaajiri hata kwa mikataba na wakawalipa fedha hiyo kutoka kwenye own source. Hawa ndiyo watakaosababisha ufanisi na makusanyo hata kwenye Halmashauri zenyewe. Kwa hiyo, hili halijazuiwa lakini kadiri tutakapopata vibali vya ajira tutaendelea kuwaajiri kupitia Serikali Kuu. Mheshimiwa Kairuki akitoa vibali sisi tutaendelea kuajiri lakini kwa upungufu tulionao Halmashauri ziendelee kuwaajiri hawa watendaji watakaotusaidia wenye sifa zinazostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni miradi ya Halmashauri ambayo haijakamilika. Iko miradi ambayo haikuwa ya Serikali Kuu lakini ilipangwa na Halmashauri zenyewe na ikawa vipaumbele vyao na wakasema wataitekeleza miradi hiyo kwa kutumia own source zao. Nitoe rai na niagize Mamlaka ya Serikali za Mitaa pale ambapo wana mikataba na wakandarasi au na suppliers, wanawatesa wenzao wanahangaika, wao walishaanza kutekeleza upande wao wa mikataba, wametekeleza miradi hiyo, lakini hawawalipi kwa kisingizio cha kwamba Serikali Kuu haijatoa fedha. Mlikubaliana kwamba mtawalipa kutoka kwenye own source, muwalipe suppliers and contractors kwa sababu ni kuwaonea na wengi wamefilisika na wengi hata wamekufa kwa sababu ya madeni hayo, hii haikubaliki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, nichukue nafasi hii kuzungumzia juu ya property rates…
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeshamaliza maandalizi yote ya kukusanya kodi ya majengo katika Halmashauri 30 ambazo tulikubaliana hapa na tukapitisha sheria na kwa sasa wako tayari kuanzia mwisho wa mwezi huu kukusanya fedha hizo. Hata zikikusanywa na Waziri wa Fedha kwa sababu ndiye anayeshika Sera na Sheria ya Fedha, mwisho wa siku zitarudi huku kuja kutusaidia katika miradi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naomba kuunga mkono hoja.