Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba kuchangia hoja hii ya Taarifa ya Shughuli ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa mwaka huu wa fedha. Kwanza kabisa, niseme naunga mkono hoja hii ya Kamati na niipongeze sana Kamati chini ya Uenyekiti wa Mheshimiwa Rweikiza na Makamu Mwenyekiti pamoja na Waheshimiwa Wajumbe wote kwa namna ambavyo wamekuwa wakitushauri na kutusimamia kama Serikali katika majukumu mbalimbali tunayoyatekeleza. Kipekee zaidi niwashukuru kwa ziara mbalimbali walizozifanya katika maeneo yetu tunayoyasimamia na zaidi katika kutembelea miradi ya maendeleo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende tu kusema kwamba, yote yaliyowasilishwa na Kamati tutayafanyia kazi na tutaleta utekelezaji katika Kamati kuona ni kwa namna gani tumeweza kuyatekeleza. Vilevile nipende kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia taarifa hii kwa ushauri wao na kwa changamoto ambazo wamezibainisha na niwahakikishie kwamba tutazifanyia kazi na kuzitekeleza na naamini wataweza kuona mrejesho wake namna ambavyo tutazitekeleza vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa kuna hoja kubwa katika suala zima la utaratibu wa hatua za kinidhamu katika utumishi wa umma. Ni jambo ambalo nimeliona limesemewa sana na Kamati lakini Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa kiasi kikubwa wamelisema suala hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, usimamizi wa nidhamu na ajira katika utumishi wa umma unatekelezwa kwa kuzingatia sheria, kanuni, taratibu lakini zaidi ya yote sheria yetu mama ambayo ni Katiba ya nchi yetu. Vilevile kama Wizara ya Utumishi wa Umma tumekuwa tukitoa miongozo mbalimbali ambayo inasimamia utumishi wa umma na kuongoza viongozi wote ambao wanatekeleza masuala ya nidhamu pamoja na ajira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo mamlaka mbalimbali za ajira na nidhamu. Ukiangalia katika kifungu cha 6(1) cha Sheria ya Utumishi wa Umma pamoja na Kanuni ya 35 ya Kanuni za Utumishi wa Umma zimeeleza bayana ni namna gani mamlaka za nidhamu zitaweza kutekeleza majukumu yake katika kuchukua hatua za kinidhamu. Hata itakapotokea Wakuu wa Mikoa au Wakuu wa Wilaya au kiongozi mwingine yeyote wa Serikali anapochukua hatua stahiki za kinidhamu ni lazima mamlaka ile ya ajira na nidhamu ndiyo itekeleze jukumu hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba ieleweke bayana na napenda kuwatangazia wote tuzingatie misingi ya kifungu cha 6(1) cha Sheria ya Umma pamoja na Kanuni ya 35 ya Kanuni zetu za Utumishi wa Umma. Hata katika makundi mengine ya utumishi, tunao watumishi wa Bunge, tunao watumishi wa Mahakama, tunao wanataaluma wengine, tunao watumishi wengine katika vyombo vya ulinzi na usalama, nao pia ni makundi ya utumishi wa umma lakini ipo miongozo ya mamlaka zao pia za ajira na kinidhamu. Kwa hiyo, niombe sana viongozi wetu wengine wa kisiasa pamoja na viongozi mbalimbali na mamlaka za ajira na nidhamu waweze kuhakikisha kwamba wanatekeleza misingi hii kama ilivyoanishwa katika sheria. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi nisisitize mahusiano. Jambo kubwa ukiangalia sehemu zingine unakuta mahusiano ni tatizo. Kila mmoja aone ana wajibu wa kuhakikisha kwamba kunakuwa na mahusiano mazuri na viongozi wa Serikali vilevile pamoja na viongozi wa kisiasa. Naamini tukiwa na mahusiano na mawasiliano mazuri kwa kiasi kikubwa migongano ambayo ipo itaweza kuondoka kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, imetolewa pia hoja kuhusiana na semina elekezi. Nipende tu kusema kama Serikali na asubuhi nilikuwa na swali nimejibu, tumekuwa tukitoa mafunzo ya aina hii na hatutasita kuendelea kutoa mafunzo kama haya tena. Hata Utumishi mwezi huu tumepanga tena mafunzo ya siku saba kwa viongozi hawa kuhusiana na masuala mbalimbali ya kiutumishi, masuala ya maadili ya utumishi wa umma nao kama viongozi vilevile masuala mengine ya rushwa, nidhamu pamoja na masuala ya fedha. Niwaombe sana viongozi hawa wote wanaohusika waweze kuhakikisha kwamba wanazingatia sheria, kanuni na utaratibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru pia kwa Waheshimiwa Wajumbe wote waliochangia kuhusiana na hoja za TASAF na nashukuru kwamba mmeweza kuona ina manufaa. Niwahakikishie kwamba tutaendelea kufuatilia ili kuhakikisha kwamba changamoto zote zinazojitokeza na upungufu wote uliopo basi unaweza kuchukuliwa hatua. Tumeanza kuchukua hatua ya kuboresha usimamizi zaidi pia tunaangalia suala zima la mfumo wa utambuzi, ni namna gani kaya hizi maskini zinazostahili kuingizwa kwenye mfumo zinaweza kutambuliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wote wameeleza hapa, wapo ambao walikuwa hawahudhurii katika mikutano ya hadhara ya wananchi ya kuibua kaya hizo, wako ambao wengine walikuwa wanasema hela hizi ni za freemason matokeo yake zimekuja kuingizwa zingine ambazo hazistahili na zile zinazostahili zimekuwa zikiachwa nyuma. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge tutayafanyia kazi, tumeanza kuondoa kaya 55,692 lakini zaidi tutaangalia control mechanisms. Pia nilimsikia Mheshimiwa Bashe tutaenda kuangalia kwa kina ili kuona tuje na mfumo gani mzuri zaidi ambao utaweza kutusaidia katika kutekeleza mfumo huu wa maendeleo ya jamii bila kuleta matatizo yoyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisikia kuna mtu anasema kuna kaya zimechukua hizi fedha ambazo hazistahili kwamba iweje leo hii waambiwe warudishe. Nipende tu kusisitiza kwamba kila fedha iliyochukuliwa kwa kaya ambayo haistahili ni lazima itarudi whether ni kaya maskini au ni tajiri lazima itarudi kwa sababu kama angekuwa ni maskini angekuwa kwenye mpango kihalali. Yule ambaye ameondolewa hastahili kwa mujibu wa vigezo vilivyowekwa na ofisi yetu ya Takwimu ya Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya suala zima la ajira, niendelee kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge tayari tumeshaanza kufungulia ajira. Tulishaajiri nafasi 5,074 na tayari wamesharipoti na kwa sasa tuko katika hatua ya kuajiri watumishi wengine wa sekta ya elimu pamoja na maabara watumishi 4,348. Baada ya hapo tutaingia katika sekta ya afya pamoja na sekta zingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewasikia Waheshimiwa Wabunge walioeleza upungufu katika sekta ya afya, ni kweli tuna upungufu wa takribani asilimia 51.3 ambao ni sawa na watumishi 54,459. Tunachokifanya sasa tunaangalia pia uwezo wetu wa kibajeti, tungependa kuajiri watumishi wengi sana. Kwa ujumla kwenye Serikali tuna upungufu wa watumishi 160,172,000 lakini kwa sasa tunajitahidi kwenye maeneo yenye vipaumbele na kwenye Halmashauri zenye upungufu mkubwa kuona ni kwa namna gani tunawapatia watumishi hao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja pia kuhusiana na uhakiki wa matamko ya fomu za maadili. Niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wameshawasilisha matamko yao. Kweli kwa kipindi hiki tumeweza kuvuka lengo ukiangalia waliowasilisha tarehe 31 walikuwa ni zaidi ya asilimia 87, ni namba ambayo kwa kweli ilikuwa haijawahi kufikiwa huko nyuma. Kwa hiyo, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge. Zaidi niwahakikishie pia tutaendelea na uhakiki, tumeshafanya uhakiki kwa viongozi wa umma 116 na lengo letu kabla ya kufika mwezi Juni tutakuwa tumefanya uhakiki wa viongozi 500. Kwa hiyo, tunaomba tu Waheshimiwa viongozi wa umma waweze kutoa ushirikiano watakapofuatwa kwa ajili ya kufanyiwa uhakiki wa mali zao na madeni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja pia ya maabara ya uchunguzi au forensic laboratory, tunazo maabara za aina mbili. Kuna moja yenye uwezo wa kufanya uchunguzi wa kieletroniki na nyingine ina uwezo wa kufanya uchunguzi wa kimaandishi. Ile ya uchunguzi wa kieletroniki imeshaanza kazi. Tunawashukuru Kamati kwa kuifuatilia na tayari wameshachunguza majalada takribani 109. Kwa upande wa document forensic au uchunguzi wa maandishi, kwa sasa kwa mujibu wa kifungu cha 59 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ni Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ndiyo ambaye anaruhusiwa kuwaruhusu TAKUKURU kuweza kuwa na maabara hii ya kuweza kufanya uchunguzi wa kimaandishi. Tayari tumeshawasilisha na tunaendelea vizuri na tunaamini ataweza kukubali maombi haya ili TAKUKURU maabara yake iweze kufanya kazi kwa ajili ya kuharakisha uchunguzi na kuongeza ufanisi wa uendeshaji wa kesi zetu mahakamani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa tukisikia watu wanasema uhakiki hauishi. Tumekuwa tukifanya uhakiki kwa umakini mkubwa sana na niseme uhakiki kwa watumishi hewa tumeshamaliza, lakini mwisho wa siku bado utakuwa endelevu pindi tutakapokuwa tunaona kuna watu ambao wameingia hawastahili watakuwa wakihakikiwa na watakuwa wakiendelea kuondolewa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa tunachokifanya ni uhakiki wa vyeti vya kitaaluma na nipende kusema kupitia Bunge hili tumeshatangaza kwa mtumishi wa umma ambaye aliombwa awasilishe cheti chake cha taaluma cha form four, six na cheti cha ualimu au taaluma nyingine akashindwa kuwasilisha lakini bado tukatoa fursa aweze kuwasilisha index namba na bado akashindwa, basi itakapofika tarehe 1 Machi tunaanza mchakato wa kuanza kufukuza kazi mtumishi wa aina hiyo. Kwa hiyo, niombe kupitia Bunge hili iweze kusikika vizuri kabisa na waweze kuzingatia suala hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema uhakiki hauishi hapana, huu ni uhakiki mwingine kabisa. Ni lazima tuwe na watumishi wa umma ambao kweli wamebobea na kweli wameenda shule. Wako watu wengine wana vyeti vya ualimu hata kwenye chuo cha ualimu chenyewe hakuwahi kufika kabisa, unategemea nini? Tunalaumu hapa kwamba ni masuala ya elimu bure fedha inaenda kidogo, kuna mambo mengine ni kama haya ndiyo ambayo yanachangia. Kwa hiyo, tunaomba mtupe fursa tujitahidi kuweka mambo sawa kuhakikisha kwamba tuna watumishi wa umma wale tu ambao kweli walisomea, kweli vyeti vyao ni vya halali na hawajaingia katika ajira kwa sifa ambazo hawastahiki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa pia kuna hoja nyingine kuhusiana na hatua za kinidhamu ambazo zimechukuliwa dhidi ya watumishi wa umma au viongozi waliobainika kusababisha watumishi hewa. Nipende tu kusema kwamba hadi sasa Serikali imeshawachukulia hatua watumishi wa umma 1,595 kwa mujibu wa Sheria zetu za Utumishi wa Umma na taratibu zao za nidhamu ziko katika hatua mbalimbali. Kati ya watumishi hao 1,595 watumishi 16 wanatoka katika Wizara sita, watumishi tisa wanatoka katika Sekretarieti za Mikoa na 1,564 wanatoka katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Tutaendelea kusimamia na kuhimiza utekelezaji wa sheria, kanuni na miongozo mbalimbali iliyopo katika utumishi wa umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa pia kuna hoja kuhusiana na Wakala wa Serikali Mtandao kwamba inawezekanaje mpaka sasa bado wana ukosefu wa sheria inayoanzisha Wakala huu. Nipende tu kusema kwamba tunashukuru na tunapokea ushauri wa Kamati na tayari tumeanza kuufanyia kazi, tuko katika hatua nzuri ya kuandaa Waraka kwa ajili ya kuanzisha Wakala huu.