Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria Pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Mchango wangu nitaanza kujielekeza kwa ndugu zangu wa TAMISEMI. Serikali ya Awamu ya Tano toka iingie madarakani haijaongeza nyongeza ya mishahara, lakini pia watumishi wamepandishwa madaraja lakini hakuna mabadiliko ya mishahara kutokana na madaraja waliyopandishwa. Sasa naomba Serikali iwaangalie watumishi ambao watastaafu katika kipindi hiki, kwamba wao walistahili wapate nyongeza hizo kwa mujibu wa sheria, lakini kwa kuwa sasa Serikali imeamua kutofanya hivyo maana yake kuna uwezekano wa watumishi hawa kukosa haki yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali watumishi wataostaafu katika kipindi hiki basi lazima wazingatie kwamba watastaafu kwa kukokotoa kwa hesabu zipi? Kwamba watakokotolewa kwa hesabu zile ambazo kabla mshahara haujabadilishwa au mpaka hapo sasa ambapo Serikali itaamua kuongeza nyongeza hizo za mishahara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ni suala la waraka uliotolewa na Serikali kuhusiana na vigezo vipya vya namna gani sasa shule zinaweza zikapata usajili. Kuna waraka mpya umetolewa kwamba ili shule iweze kusajiliwa lazima shule hiyo iwe na madarasa 10, nyumba tatu za Walimu, matundu 10 ya vyoo. Suala hili nafikiri Serikali haijafanya utafiti wa kutosha kwa sababu mazingira ya maeneo ya vijijini ni ngumu sana kwa shule kuwa na uwezekano wa kujenga vyumba 10 vya madarasa, nyumba tatu za Walimu ili waweze kufikia vigezo vya kuweza kupata usajili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali lazima ikumbuke pia wana jukumu kubwa la kuhakikisha linafuta ujinga, linaondoa vijana ambao watakuwa na matatizo ya kushindwa kuhesabu, kusoma na kuandika, sasa kama hili halitazingatiwa maana yake upo uwezekano wa Serikali kuzalisha vijana wengi wenye shida ya kupata ujuzi huo.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali bado haijawaangalia Wenyeviti wa vijiji na vitongoji, wanafanya kazi kubwa lakini bado Serikali haijawaona. Naishauri Serikali ione uwezekano wa Wenyeviti wa Vitongoji na Vijiji waweze kupata posho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mahusiano mazuri kati ya watendaji wa Serikali na wawakilishi wa wananchi kwa maana ya Madiwani pamoja na Waheshimiwa Wabunge. Katika Halmashauri Wakurugenzi wengi wapya walioteuliwa hawana mahusiano mazuri na Waheshimiwa Madiwani na hoja kubwa katika utendaji wao wa kazi, wanasema sisi ni wateule wa Rais, kwa hiyo mara zote, hata katika mambo ambayo yanahitaji kutumia hekima na busara msingi mkubwa unakuwa kwamba sisi ni wateule wa Rais kwa hiyo tunafanya vile tunavyoona. Niishauri Serikali itoe semina kwa Wakurugenzi hawa, lakini pia inatakiwa wawashauri watumie hekima na busara ili kuona kwamba haya mambo yanakwenda katika utaratibu unaotakiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la TASAF ambalo limezungumziwa na Waheshimiwa Wabunge wengi, mimi pia kwa msisitizo niseme, Serikali imefanya makosa na lazima ikubali kwamba imefanya makosa. Kwa sababu, wananchi hawa hawakwenda kwa Serikali kuomba msaada kwamba wasaidiwe katika kaya maskini hapana, ilikuwa ni utaratibu wa Serikali. Kama hivyo ndivyo Serikali ilijipanga na ikaweka taratibu zake kwa kutumia Maafisa wake. Kwa hiyo, Maafisa wa TASAF wanapokwenda katika kijiji fulani na kuhitaji kupata vigezo vya nani anastahili apate usaidizi huu, hilo lilikuwa ni jukumu la hao Maafisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kilichotokea sasa hivi wakasema kwamba Serikali imeleta agizo la kwamba vigezo havikufuatwa ili wananchi husika waweze kupata hizo stahili, matokeo yake, kwa mfano katika Jimbo langu la Kilwa Kaskazini katika Kijiji cha Miteja, Mkurugenzi ameagiza kwamba fedha zile ambazo zilipelekwa kwa wananchi ambao hawakustahili zilipwe na Serikali ya Kijiji na Serikali ya Kijiji sasa inatakiwa itoe zaidi ya milioni tano, hii imefanyika katika Kata ya Mandawa na Kata nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niitake Serikali izingatie tena haya maagizo yake, haikuwa ni ombi la wananchi kupata hizo pesa, ulikuwa ni utaratibu wa Serikali, kwa hiyo Serikali lazima hili iliangalie kwa umakini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vitambulisho vya Taifa; hili suala imefikia mahali kwamba wananchi wanashindwa kuelewa, walikuja hawa watu wa NIDA, wamefanya zile process zote za kupata taarifa kutoka kwa wananchi lakini mpaka sasa hivi, kwa mfano kwenye Jimbo langu la Kilwa Kaskazini wananchi hawafahamu vitambulisho hivyo watavipata lini, Serikali nalo hilo iliangalie ili wananchi wapate vitambulisho hivyo vya Taifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa ni suala la Mabaraza ya Ardhi; chombo hiki cha baraza la ardhi ni chombo kizuri sana na kimesaidia wanyonge kupata haki zao. Niishauri Serikali ihakikishe chombo hiki kinakuwepo katika ngazi zote. Kwa sasa, chombo hiki kinapatikana katika ngazi ya kijiji na ngazi ya Kata, baadaye ngazi ya Wilaya huwezi kupata chombo hiki, uende mpaka kwenye ngazi ya Mkoa na kule kwenye ngazi ya Mkoa kuna Mwanasheria mmoja tu. Kwa hiyo, naishauri Serikali ihakikishe panakuwa na Baraza la Ardhi la Wilaya ili basi kupeleka huduma hizi kwa wananchi. Pia sisi watu wa Kusini katika Mahakama Kuu Kanda ya Kusini kuna Jaji mmoja tu, kwa hiyo, utoaji wa haki unacheleweshwa kwa sababu Jaji mmoja hawezi kukidhi haja ya usaidizi wa sheria kwa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.