Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali Pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango kwa kuandaa mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa pamoja na mwongozo wa kutayarisha mpango wa bajeti kwa mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada nzuri zinazochukuliwa na Serikali katika kuongeza pato la Taifa kwa kiasi kikubwa tegemeo kubwa ni mapato ya ndani (tax revenue) kuliko kuangalia vyanzo vingine vya mapato (non tax revenue)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni vema Serikali ikajielekeza katika vyanzo vingine vya mapato (non tax revenue). Serikali ijiimarishe katika usimamizi wa taasisi zake zilizo chini ya Msajili wa Hazina ili zijiendeshe kibiashara na kurudisha mapato Serikalini kupitia gawio (dividend) na hata mapato mengine nje ya gawio. Serikali ichukue hatua za kurekebisha Mashirika yanayolegalega na hata kuyafunga yale ambayo hayana tija. Katika kufufua Mashirika na viwanda ambavyo havifanyi kazi, Serikali ichukue tahadhari kubwa hasa pale inapopelekea ubinafsishaji kwa wageni.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na lengo zuri la kufufua viwanda ambavyo kwa muda mrefu havifanyi kazi, lengo liwe kuanzisha kitu kipya katika mazingira ya sasa. Kwa mfano, Kiwanda cha Tanganyika Packers cha Mbeya, kwa sasa yaliyolengwa kuwa mashamba ya malisho (holding ground) kwa sasa yapo katikati ya mji na sheria za mipango miji zina ukomo wa shughuli za kilimo kwa mijini. Hivyo ni bora kuangalia kupata eneo mbadala jipya nje kidogo ya mji.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuipongeza Serikali kwa kujikita katika kuimarisha uchumi kupitia sekta ya viwanda. Pamoja na mkakati wa kuimarisha uchumi kupitia viwanda, Serikali iweke mkakati wa kuimarisha kilimo cha mazao yote. Nchi yetu kwa asilimia zaidi ya 70 wananchi wake wanategemea kilimo hivyo viwanda vilenge kutumia malighafi inayozalishwa Tanzania ili ukuaji wa uchumi uwaguse Watanzania walio wengi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania imejaaliwa kuwa na ardhi kubwa na nzuri ambayo inaweza kuzalisha mazao mbalimbali yenye soko zuri la ndani na nje. Zao kama pareto limeachwa yatima licha ya mahitaji makubwa katika soko la dunia. Kuna haja ya kuongeza uzalishaji wa pareto na pia kuwepo na viwanda vya pareto maeneo yanayolima pareto. Kwa sasa soko la pareto hapa Tanzania linayumba kutokana na kukosa ushindani katika manunuzi toka kwa mkulima.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie utekelezaji wa miradi iliyomo katika mipango iliyopita. Pamoja na mahitaji ya miradi mipya, mikakati iwepo ya kutekeleza miradi ya nyuma kama vile miradi ya maji, zahanati na vituo vya afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mashirika kama NHIF yajikite katika malengo yake ya msingi na yakisimamiwa vizuri wanaweza kuwekeza katika ujenzi wa zahanati, vituo vya afya na uwekezaji huo una uhakika wa kuilipa NHIF kutokana na mapato ya hizo zahanati na vituo vya afya. Kwa sasa NHIF wamejiingiza katika kuwekeza kwenye real estate badala ya kuboresha afya za Watanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza Serikali kwa kutenga shilingi milioni 50 kwa kila kijiji na mtaa. Ili kutimiza lengo hilo, napendekeza Serikali itenge angalau shilingi bilioni 300 kila mwaka kuanzia 2017/2018 ili kukamilisha upelekaji wa fedha hizo kwenye maeneo yote kabla ya 2020.
Mheshimiwa Naibu Spika, dhamira ya milioni 50 kwa kila kijiji inahitaji kuandaa utaratibu mzuri kushirikisha SACCOSS na pia napendekeza kuitumia Benki ya kilimo TADB. Kwa kuitumia TADB Serikali itatimiza malengo ya kuinua uchumi, wakulima pia kuiwezesha TADB kupata mtaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na ujenzi wa reli ya kati kwa standard gauge, Serikali iweke mkakati wa kuboresha utendaji wa TAZARA ikiwemo kujenga matawi ya reli kuunganisha Liganga na Mchuchuma.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iweke mkakati wa kuboresha miundombinu ya Baraza la vijijini kuwezesha usafirishaji wa mazao na kurahisisha masoko ya mazao.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.