Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa. Nianze nami kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango na Naibu wake kwa kazi nzuri sana. Kwenye hotuba ya Waziri na makabrasha naona hapa, wameongelea kuhusu maboresho yanayofanyika Bandari ya Itungi, lakini kwa kifupi sana, nataka nieleze tu, kuyapanua kwa sababu nilikuwa huko hivi majuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli yanayotokea Bandari ya Itungi, ni mapinduzi makubwa, katika historia ya miundombinu nchini. Kwa sababu kwa mara ya kwanza toka Uhuru, Tanzania inajiondoa kwenye utegemezi kwa nchi ndogo ya Malawi katika kukarabati vyombo vyake vya majini. Sasa hivi kutokana na chelezo ambayo imefungwa pale, Tanzania tunaweza sasa katika Ziwa Nyasa kujenga vyombo vyetu sisi wenyewe, kuviunda vipya na kukarabati vyombo vipya. Sasa hivi zinajengwa bajezi mbili pamoja kuanzia mwezi wa sita tunajenga meli yenye uwezo wa kubeba abiria 200 na tani 200 za mizigo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni initiative ya TPA na baada ya pale wanahamia Lake Tanganyika na Lake Victoria. Kwa hiyo, wananchi wanaona hayo na tuendelee tu na juhudi hizo. Nimefurahi vilevile kusikia, kwenye hotuba ya Waziri kuhusu ujenzi wa hivi vituo, Kituo cha Utoaji Huduma Pamoja, hivi vinavyoitwa One Stop Border Posts, tumejenga nyingi kwa Rwanda, Burundi, tunayo Uganda, kwa mpaka wetu na Kenya tunazo tatu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunajenga Zambia, sasa ipo ya Malawi na Tanzania. Kwa kweli, ni taarifa nzuri sana kwa wafanyabiashara wa Malawi na Tanzania na vile vile fursa ya kufanya biashara kubwa kwa wananchi wa Wilaya Kyela na Kasumulu upande wa Malawi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, dogo tu kuhusu masuala ya Katiba. Wiki hii tumekuwa tukijenga msingi wa kutekeleza masharti ya Ibara ya 63(3)(c) ya Katiba ambayo inasema; “Bunge hili, litajadili na kuidhinisha Mpango wa muda mrefu au muda mfupi wa Taifa.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, wengi walidhani Serikali inakuja na Mpango, ilionekana hapa katika majadiliano ya mwanzo pale. Inakuja na Mpango, hapana hapana, hili ni zoezi shirikishi la Kikatiba, linataka sisi tuchangie. Nataka nisisitize tu hapa kwamba, dhana ya zoezi hili kuwa shirikishi, linatokana na masharti ya Ibara ya 8 ya Katiba hii, inayosema kwamba; “Wananchi wa Tanzania ndiyo msingi wa mamlaka yote. Pili, lengo kuu la Serikali ni ustawi wa wananchi. Tatu, Serikali inawajibika kwa wananchi. Nne, wananchi washirikishwe au watashiriki katika shughuli za Serikali.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, niongeze maneno yangu, kupitia wawakilishi wao ambao ni Wabunge. Sasa Ibara ya 63(3)(c) inatutaka sisi wawakilishi wa wananchi, sasa tuchangie tuweze ku-reflect haya, kwamba Serikali katika mipango yake, inajali ustawi wa wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikimbie tu neno moja dogo la haraka haraka lingine, maana muda wenyewe ndiyo huo. Kumekuwa pia na kejeli katika kuiangalia hii kaulimbiu ya hapa kazi tu, inaonekana kama ni kauli ngeni, kauli ya kipropaganda tu, lakini nataka kusisitiza hapa kwamba hii ni kaulimbiu ya Kikatiba, tena Katiba yenu wenyewe hii hapa, niliyoishika hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 25(1) inasema: “Kazi pekee ndio huzaa utajiri wa mali katika jamii, ndiyo chimbuko la ustawi wa wananchi na kipimo cha utu na kila mtu anao wajibu wa kushiriki kwa kujituma na kwa uaminifu katika kazi halali na ya uzalishaji mali.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Ibara ya 9(e), Katiba inasema; “Serikali itahakikisha kwamba kila mtu mwenye uwezo wa kufanya kazi, anafanya kazi na kazi maana yake ni shughuli yoyote ya halali, inayompatia mtu riziki yake.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiendelea tena ibara ya 22 inatupa confidence, inasema…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.