Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UTUMISHI NA UTAWALA BORA): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia mapendekezo haya. Niupongeze uongozi mzima wa Wizara ya Fedha na Mipango kupitia Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote. Mpango huo au mapendekezo haya yaliyowasilishwa kwetu kwa kweli ni mazuri, kwa vigezo vyote, lakini zaidi, ukiangalia katika masuala matatu.
Mapendekezo haya ya Mpango, yamejengwa katika mafanikio ya Mpango wa Maendeleo wa Kwanza. Pili, mapendekezo haya yamezingatia Ilani ya Uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi, inayotekelezeka, iliyo bora, lakini vilevile ni ilani ambayo inapimika, lakini tatu, ukiangalia umezingatia, mabadiliko yaliyopo katika Serikali ya Awamu ya Tano, katika utendaji wake kazi na kupitia dhana nzima ya hapa kazi tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na masuala ya Utawala Bora, katika Mpango huu, utaona kabisa suala zima la utawala bora limewekwa kama kipaumbele muhimu sana. Ukiangalia ili tuweze kupata mafanikio yoyote, ili tuweze kufanikiwa katika uchumi huu wa viwanda, ni lazima tuweze kuwa na mafanikio makubwa katika utawala bora.
Kwa upande wetu tutahakikisha kwamba, tunaimarisha taasisi zetu mbalimbali zinazotekeleza masuala ya utawala bora ikiwemo TAKUKURU, ikiwemo Sekretarieti ya Maadili, lakini vilevile kwa upande wa Mahakama na taasisi nyingine za utoaji haki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wapo watu ambao walisema hakuna utaratibu wa kuandaa viongozi. Niseme tu kwamba katika Serikali utaratibu huo upo na hivi sasa wameandaliwa viongozi wengi, wamepatiwa mafunzo na wengi wao wapo katika kanzidata ambapo itkapojitokeza tuna mahitaji, basi wanaweza kuchukuliwa na kuweza kupewa nafasi mbalimbali kwa ajili ya kutekeleza. Tunayo assessment center methodology, ambayo kimsingi imeweka watumishi mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee tu kurudia na kusisitiza kwa watumishi wenzangu wa umma. Tuombe sana sana, waweze kuzingatia nidhamu ya hali ya juu. Waweze kuwa wabunifu, waweze kuzingatia maadili, kwa sababu bila ya kuwa na watumishi wa umma wenye sifa na wenye kutekeleza majukumu yao kwa kujituma na kuwa na uwajibikaji, Mpango huu utakuwa ni ndoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali, tutaendelea kufuatilia na kuchukua hatua, dhidi ya mtumishi yoyote wa umma ambaye atakiuka utumishi wake. Vilevile kama mnavyofahamu, kupitia utumishi wa umma, viongozi mbalimbali wamesaini, wamekula kiapo, kupitia ahadi ya uadilifu. Niwaombe tu watumishi hawa wa umma waendelee kuishi, kupitia viapo vile walivyokula.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba tumeyapokea yote mengi mazuri, ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyapendekeza hapa na tutayatekeleza. Pia niseme kwamba, kupitia TAKUKURU tutaendelea kuijengea uwezo. Ukiangalia hivi sasa, wanazo ofisi 52 tu nchi nzima, majengo 52. Ukiangalia katika kila Wilaya mahitaji ni zaidi ya watumishi sita mpaka saba ili uweze kuwa na ufanisi. Hivi sasa wapo watumishi watatu tu na kupitia Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma, tutahakikisha tunawapa idadi kubwa ya watumishi wasiopungua 400 katika mwaka ujao wa fedha, ili basi kila Wilaya iweze kuwa na ufanisi katika suala zima la ufuatiliaji kwa watu wanaokiuka masuala mbalimbali ya uadilifu, lakini vilevile wanaochukua rushwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, rushwa inaathiri masuala ya haki za binadamu, rushwa inaongeza tofauti kubwa iliyopo kati ya walionacho na wasionacho, rushwa kwa kiasi kikubwa, imekuwa ikiathiri sana utoaji wa huduma. Kama ambavyo nilisisitiza wakati ule nikiwa nachangia hotuba ya Mheshimiwa Rais, tutaendelea kufuatilia miradi mbalimbali ya maendeleo na kuhakikisha kwamba fedha zile zinazotengwa, basi zinakuwa na ufanisi na zitatumika kama zilivyokusudiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa uongozi, tutaendelea kutoa programu mbalimbali za mafunzo, lakini vilevile kwa upande wa sekta ya umma tunaamini, ni lazima tuhakikishe tunaboresha huduma tunazozitoa. Kwa hiyo, tutaendelea kuhakikisha kwamba watumishi wa umma wanaendelea kuongezeka, kwa kadri ya mahitaji na kadri uchumi utakavyoruhusu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tunafahamu kwamba watumishi hawa hawawezi kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi, bila ya kuangalia maslahi mbalimbali ya watumishi wa umma. Niwatoe hofu, watumishi wa umma wenzangu, tutayaangalia kwa kina na wataweza kupata maslahi ambayo wanastahili baada ya kuwa tumefanya tathimini ya kazi, itakapokamilika baada ya miezi 15. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi.