Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba nichukue nafasi hii kwanza niwapongeze sana Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia hoja hizi, lakini kwa namna ya pekee niwapongeze Wajumbe wa Kamati zote mbili kwa ushauri wao kwa Serikali. Niendelee tu kusema kwamba Serikali hii sikivu itaendelea kusikia na hakuna shaka lolote na wale wenye wasiwasi naomba waondoe tu wasiwasi wao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze tu kwanza na la Mheshimiwa Paresso kuhusu kuunganisha Mifuko. Ningependa tu kusema suala hili Mheshimiwa Paresso wala asifikiri kwamba yeye ndio analianzisha leo hapa Bungeni. Kama alikuwa anasikia vizuri Mheshimiwa Paresso tukubaliane kwamba Mheshimiwa Rais alishatuagiza siku ya Mei Mosi akatuambia ni lazima tufikirie sasa kuunganisha hii Mifuko, kwa hiyo ushauri wake ni mzuri sana unaendana pia na agizo la Mheshimiwa Rais.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Paresso tuko pamoja na Mheshimiwa Rais alishaagiza suala hili, kwa hiyo, tutalitekeleza tu na tunaendelea na mchakato huo wa kutekeleza agizo hili la Rais pia la kuunganisha Mifuko. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, limezungumzwa hapa suala la Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kukopesha Vyama vya Ushirika vya Akiba na Mikopo. Waheshimiwa Wabunge, naomba niseme hivi, Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii inaongozwa na sheria. Kwanza Mifuko yenyewe ina sheria zake, lakini pia inasimamiwa na Mdhibiti wa Sekta hii ya Hifadhi ya Jamii, na mdhibiti anaongozwa na sheria ambayo tuliitunga mwaka 2008, tukaifanyia marekebisho mwaka 2012 na tukaifanyia marekebisho mwaka 2013. Kifungu cha 9 cha miongozo ya uwekezaji kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kinaruhusu Mifuko hii kukopesha Vyama vya Akiba na Mikopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama miongozo inaruhusu, kwa hiyo, Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii inapokopesha SACCOS haifanyi makosa, labda makosa yawe mengine, lakini haifanyi makosa. Naomba Waheshimiwa Wabunge muelewe kwamba mahali pekee ambapo wanachama wanaweza kufaidika na Mifuko hii kupata mikopo yenye riba nafuu ni kupitia kwenye vyama vyao vya akiba na mikopo na watakapokopa fedha kwenye vyama hivi vya akiba na mikopo ndipo wanachama wanaweza kwenda kufanya shughuli nyingine za uzalishaji na uchumi na kuwafanya waendelee kuwa wanachama sustainable kwenye Mifuko hiyo ya Hifadhi ya Jamii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba suala la Mifuko kukopesha Vyama vya Akiba na Mikopo tusilipotoshe. Tuzungumze sekta nyingine kama walivyozungumza kwenye Kamati, lakini Mifuko hii inaruhusiwa kufanya hivyo. Tumeona kwamba sasa hivi tunataka kupanua wigo wa wanachama, hivi tunapopanua wigo wa wanachama kwenda kwenye sekta binafsi, vijana wetu waliopo katika sekta isiyo rasmi watafaidikaje na hifadhi ya jamii kama hawatapatiwa dirisha la kukopa kwenye Mifuko hii? Kwa hiyo, naomba tuunge mkono juhudi za mifuko kukopesha wanachama wake wakajenge nyumba, wakafanye nini na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niseme, kama kuna tatizo katika utekelezaji wa jambo hili, hilo ndilo suala ambalo sasa Serikali ni lazima ikasimamie kuhakikisha kwamba vigezo vinafuatwa, lakini kuikataza Mifuko hapana, mwongozo uko hapa…
TAARIFA...
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, namheshimu sana mdogo wangu Mheshimiwa Ester, lakini angefuatilia ninachotaka kusema ni kitu gani na naomba ulinde muda wangu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kumwambia Mheshimiwa Esther, akifuatilia Hansard leo wapo baadhi ya Wabunge wachangiaji wamesema Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii isikopeshe fedha kwa wanachama kupitia mfumo wa akiba na mikopo. Sasa nataka kuwaeleza Waheshimiwa Wabunge kwamba Mifuko ile haifanyi nje ya utaratibu na mwongozo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimeendelea kusema hapa na naomba Mheshimiwa Esther anisikilize vizuri; kinachotakiwa kufanyika ni kuhakikisha kwamba mikopo hiyo sasa itolewe kwa kufuata taratibu na sheria zilizowekwa na zisigeuze utaratibu wowote. Kwa hiyo, naomba nimwambie Mheshimiwa Esther, asichukulie udhaifu wa mtu mmoja kuwakosesha haki wanachama wengine wa mifuko, haitakubalika, sisi tutasimamia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Manji liko mahakamani, Serikali kupitia mfumo tumeshaanza kuchukua hatua na ni lazima tutaendelea kuchukua hatua hata kwa wakopaji wengine. Ninyi Waheshimiwa Wabunge mnajua, hata Mheshimiwa Ester anajua, mimi nina taarifa za NSSF hapa, kuna viongozi, hata kiongozi mmoja mkubwa wa chama fulani hapa ndani na yeye amekopa mkopo chechefu, hajarudisha! Kwa hiyo, tunapozungumza haya tuyaweke yote wazi, bayana, tusifichefiche vitu vingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme hivi, kifungu cha tisa (9) kama nilivyosema, kinaweka mfumo wa kukopesha Vyama vya Akiba na Ushirika lakini tunasema hivi, asilimia 10 ya rasilimali za uwekezaji kwenye Mifuko ndicho kigezo kinachowapa ruhusa ya kukopesha Vyama vya Akiba na Mikopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa vyama hivyo vimeshakopesha kwenye vyama hivyo vya akiba na mikopo, mikopo isiyozidi hiyo asilimia 10 ya assets zilizopo. Sisi kama Serikali tutaendelea kusimamia na nina kuhakikishia watu wote waliokopa ni lazima warudishe hela kwenye Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii. Hilo la kwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, menejimenti zote ambazo zinafanya kazi kwenye Mifuko hii bila kufuata utaratibu Waheshimiwa Wabunge nawahakikishia Serikali tutaendelea kuchukua hatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kwa kusema kwamba, Waheshimiwa Wabunge sisi kama Serikali tunawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa ushauri mliotupa, tutafanya kazi na Bunge, lakini tutahakikisha kwamba sekta ya hifadhi ya jamii haitaweza kuhujumiwa na mtu yoyote na tutakuwa makini katika jambo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.