Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Charles John Mwijage

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Muleba Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia fursa ya kuchangia Mapendekezo ya Mpango. Mapendekezo ya Mpango ni mazuri na kama mnavyojua, lugha ya mjini ni kujenga uchumi wa viwanda ili kufanya mageuzi ya uchumi yatakayoleta maendeleo ya watu na hiyo inawezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya upungufu wa muda, ningependa nijibu baadhi ya maswali yaliyojitokeza na nianze na shemeji yangu, kusudi wajomba zangu kule wasijisikie vibaya, baba yao anajua takwimu na mjomba wao anajua takwimu. Kwa nini tunakwenda kwenye viwanda? Tutatengeneza ajira. Ilani ya CCM Ibara ya 32 mpaka 33, inasema asilimia 40 ya nguvu kazi itokane na viwanda, inawezekana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa nini, tunakwenda kwenye viwanda? Tunalenga kwamba asilimia 15 ya GDP basi itokane na viwanda, inawezekana. Kwa nini tunakwenda kwenye viwanda, tunazo rasilimali asilia tulizopewa na Mwenyezi Mungu, sasa ni wakati wa kuzichakata, hizi rasilimali hizo zipitie kwenye viwanda ili pato, tutakalopata liweze kwenda kwenye maendeleo ya watu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tunakwenda kwenye viwanda? Tunakwenda kwenye viwanda kwa sababu kwa kuchakata viwanda vya Mzee Mwigulu tutaweza kuwashirikisha wananchi walio wengi na wananchi walio wengi wakishiriki ule umaskini utaweza kuondoka. Kwa nini tunakwenda kwenye viwanda? Viwanda tulivyonavyo sasa vimeonyesha utendaji mzuri, export ya bidhaa za viwandani zimeongezeka kwa takwimu sahihi. Sasa tunataka kuongeza zaidi, twende kwenye soko la nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza juzi nchi ya India, pamoja na matatizo ya jana, wametufungulia milango kwamba bidhaa itengenezwayo Tanzania na ipelekwe kule. Sasa tunalenga viwanda gani? Tunalenga viwanda vya chuma Mchuchuma na Liganga zichakatwe ziende kule. Engaruka soda ash ichakatwe, mazao ya kilimo na mifugo yachakatwe. Hizo ni shughuli ambazo zitashirikisha watu wengi, lakini edible oil, alizeti, mawese ya Kigoma yachakatwe tuweze kutosheleza soko la ndani. Tanzania tunaagiza tani 350,000 za mafuta ya kula. Napenda mimi nikiwa katika nafasi hii tusiagize mafuta, ila sisi tuuze nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nijibu swali lingine, nani atafanya hivi? Kama alivyosema Profesa Muhongo ni mimi na wewe Mbunge, ni sekta binafsi. Sekta binafsi ndiyo injini, sekta binafsi ndiyo itasukuma hii. Kwa hiyo, sekta binafsi ndiyo ambayo itatuongoza katika kutekeleza suala hili. Sekta binafsi, nini jukumu la Serikali, Serikali itatengeneza mazingira safi, kusudi wawekezaji tuwaondolee vikwazo. Njoo kesho iishe, ardhi inapimwa pale, unakuja una mgogoro, mahakamani, mambo yanawekwa sawa. Unakuja saa tatu unasajili saa saba, hiyo iko chini yangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la kufanya, nini uzoefu wa dunia? Uzoefu wa dunia unaonyesha kwamba asilimia kubwa ya shughuli za ujasiriamali zinamilikiwa na SME, viwanda vidogo na vya kati. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge mjiandae, nilikuwa nagawa nguzo mwaka jana, sasa nitakuwa nagawa viwanda vidogo. Kwa hiyo, tafuteni viwanda vidogo, asilimia 99 ya shughuli za kiuchumi duniani ni viwanda vidogo. Lakini GDP angalia mfano wa Brazil, South Korea, India, coated industry ndiyo inazalisha bidhaa zilizo nyingi. Kwa hiyo, tunakwenda kwenye viwanda vidogo vidogo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie Waheshimiwa Wabunge, angalieni kwenye Manispaa zote na Miji muangalie, guest house yenye vyumba kumi, ni kiwanda kidogo. Mtaji wa milioni 50, milioni 100 unanunua kiwanda kidogo. Juzi, nimenunua Kiwanda Bangkok Thailand, kitazalisha chakula cha samaki, ambacho kwa mwaka kitazalisha samaki wenye thamani ya bilioni 60, juzi wamekizindua Muleba, mimi nakwenda kukihamasisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rweikiza wa Bukoba Vijijini, amenunua mtambo wa kuchakata nyanya, kwa shilingi milioni 140. Ni Mbunge gani anaweza kukosa kwenda benki akaaminiwa, kwa milioni 140, akawahamasisha wananchi, wakazalisha nyanya, akazichakata. Wale wanaochakata wanaweza kuongeza kipato.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache, tutakutana kwenye Mpango na naunga mkono Mpango.