Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. Mussa Bakari Mbarouk

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Tanga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. MUSSA B. MBAROUK: Mheshimiwa Naibu Spika, labda kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametujalia kukutana ili tuzungumze masuala ya nchi yetu. Vilevile nichukue fursa hii nikiungana na wenzangu waliotangulia kuchangia Kamati ya LAAC na PAC.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kukumbusha tu kwamba Serikali za Mitaa zipo kwa mujibu wa Katiba, Sheria na Kanuni. Hata hivyo, taarifa ya Kamati pamoja na kuandikwa vizuri kuna baadhi ya maeneo kuna upungufu. Labda nisema katika Halmashauri zetu kumekuwa matatizo ya matumizi mabaya, lakini Kamati imetupa taarifa ya baadhi ya maeneo yaliyochambuliwa kwa mfano katika uchambuzi wa taarifa ya CAG kwa mwaka wa fedha wa 2013/2014 na 2014/2015 na kuonesha hesabu zake zina matatizo katika baadhi ya maeneo. Kwa mfano, katika matumizi yasiyozingatia Sheria za Manunuzi, hapa kuna upungufu mkubwa kwa sababu Sheria za Manunuzi hazifuatwi na matokeo yake baadhi ya bidhaa au huduma zinazotolewa katika Halmashauri zinakuwa chini ya kiwango au nyingine haziridhishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu, mfumo uliopo sasa hivi katika Halmashauri zetu ambapo Madiwani wametolewa katika ile Tender Board na kuachwa watendaji peke yao ndiyo wanaofanya shughuli za manunuzi, naona huu ni upungufu, naishauri Serikali iliangalie upya suala hili kwa sababu watendaji wanapobaki peke yao huku tukiambiwa kwamba Madiwani ndiyo jicho la Serikali katika Halmashauri, wao wanafanya wanavyotaka, wanatoa zabuni kwa watu wanaowataka, matokeo yake sasa ama bidhaa au huduma zinazotolewa zinakuwa chini ya kiwango.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna upungufu katika kutekeleza mapendekezo ya Kamati kwa kipindi kilichopita na pia kutojibu hoja za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Lingine kuna usimamizi mbovu katika kupeleka au kutokukamilika kwa miradi au miradi inakuwa chini ya kiwango. Vilevile katika Halmashauri kuna taratibu zilizofanyika za kuzinyang‟anya Halmashauri makusanyo ya property tax.
Kwa maoni yangu naona hili ni tatizo kubwa sana kwa sababu Halmashauri zilikuwa zikitegemea sana property tax kama chanzo chake kikubwa cha mapato. Leo Halmashauri zimenyang‟anywa kukusanya property tax imepelekwa Mamlaka ya Mapato (TRA). Kwa mfano, hata Halmashauri yetu ya Jiji la Tanga ilikuwa na nyumba za kupangisha (quarters) pia zimeingizwa katika ukusanyaji wa TRA. Mimi naliona hili ni tatizo au Serikali itueleze kama imeamua kuziua Halmashauri kwa kifo cha kimya kimya (silent killing). (Makofi)
Mheshimwa Naibu Spika, kwa nini nasema hivyo? Leo Halmashauri zinahudimia wananchi ikiwa ni moja ya majukumu yake, kuna zahanati, shule, barabara, mifereji na usafi wa miji, unapozinyang‟anya vyanzo vya mapato shughuli hizo zitafanyikaje bila fedha?
Mimi nashauri ikibidi Halmashauri zirudishiwe kufanya mapato au kama Serikali imeona property tax ni chanzo ambacho inastahili kupata Serikali Kuu basi irudishe vyanzo vingine ambavyo ilizinyang‟anya Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine kwenye suala la Serikali za Mitaa, Serikali nayo inahusika moja kwa moja kuziwezesha Halmashauri ili ziweze kutenda shughuli zake vizuri lakini Halmashauri zimenyang‟anywa uwezo wake. Hata katika kitabu chetu hiki kuna miradi ambayo imefanywa chini ya kiwango au haijatekelezwa. Kwa mfano, mradi wa maji katika Kijiji cha Kayanze, Jijini Mwanza wenye thamani ya shilingi 618,704,554 haujatekelezwa. Pia kuna mradi wa maji wenye thamani ya shilingi 5,049,000,000 katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji nao pia haukutekelezwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, namalizia kwa kusema miradi ya maji itekelezwe.