Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa fursa hii ya kuweza kuchangia taarifa hizi za Kamati mbili kutokana na ukaguzi wa CAG.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niiambie Serikali kwamba eneo hili ni muhimu kuliangalia na kusikiliza kwa makini lakini tupate matokeo mazuri. Kwenye ripoti hizi hakuna siasa, hili ni jicho la tatu la kuona utendaji wa Serikali yetu kupitia Halmashauri na Serikali kwa ujumla na kwa sababu nia yetu ni kutengeneza na siyo kuharibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na suala la uteuzi wa Wakurugenzi. Kwa upande wangu sina tatizo na mamlaka ya uteuzi kwani inafanya kazi yake vizuri, lakini sisi kama Kamati ya LAAC tumeona upungufu mwingi siyo kidogo ya utendaji ya Wakurugenzi wetu. Wapo Wakurugenzi ambao hawajawahi kufanya kazi kabisa kwenye mfumo wa Serikali hata kwenye mashirika ya Serikali kiasi kwamba hata hawajui uendeshaji wa Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali kwa nia njema tu, tusibane sana matumizi, tuwafanyie mafunzo kidogo. Kuna Wakurugenzi walikuja mbele ya Kamati hawajui hata itifaki ya vikao. Sasa ukiwa na Mkurugenzi wa aina hiyo, unajua maneno wanayotumia wengi wanasema mimi nimeteuliwa na Rais, wanadhani uteuzi wa Rais unaweza kumfanya akaendelea kudumu pale, mimi sikubaliani nao. Bahati nzuri mimi nimetokea kwenye Halmashauri, kwa hiyo najua vizuri mno shughuli za Halmashauri, lakini kwa uelewa wangu mdogo wa hesabu Wakurugenzi wengi kwa kweli hawana uwezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hilo tu, wapo ma-DT kwa maana ya Watunza Hazina wetu pamoja na kuwa na vyeti hawana uwezo wa kazi. Wapo ma-DT ambao wana CPA, lakini uwezo wao wa kufanya kazi ni mdogo sana. Kwa hiyo, niiombe Serikali tutupie macho utendaji wa watu hawa hasa Wakurugenzi na Watunza Hazina. Kule kwenye uteuzi kama nilivyosema hatuna mamlaka nako, lakini basi wapewe mafunzo kuwapa uwezo wa kufanya kazi na kuzielewa kazi. Wenzangu wamesema kuna watu wametoka kwenye NGOs, mashirika, VETA na sehemu mbalimbali, kwa idadi kubwa wachache sana waliotoka kwenye Local Government. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nigusie kidogo suala hili la UDA. Tumepata taarifa Kamati mbalimbali zimekuwa zinashughulika na jambo hili la UDA. Niiombe Serikali ifike mahali tumalizane na UDA. UDA kila siku inatajwa Bungeni, kila siku haina mwenyewe, tumehoji nani mmiliki wa UDA mpaka tunamaliza vikao hatujapata majibu nani wamiliki wa UDA. Ifike mahali sasa tupate majibu nani wanamiliki na ilikuwaje alipatikana Simon Group.
Mheshimiwa Naibu Spika, Simon Group kwenye ripoti mbalimbali ameibuka tu kwamba huyu kapatikana anauziwa hisa, sasa amepatikana vipi hapaonyeshi mchakato ulioendeshwa kumpata Simon Group. Hili ni jambo la hatari kama kampuni inakuja tu ghafla, Serikali inakubali inaipa kazi. Tumempa umiliki mtu ambaye hajashindanishwa, hili ni jambo la hatari sana. Sasa tunataka tumjue mmiliki kwa sababu kumekuwa na shida ya kujua nani na nani anamiliki UDA. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema mwenzangu pale Mheshimiwa Msuha zipo hisa zilipouzwa ilikubalika ziende kwenye shughuli za maendeleo, kwa muda wote hizi pesa zimetunzwa pale BOT. Kwa nini sasa muda usifike uamuzi upite zile fedha ziende kwenye shughuli za maendeleo. Ni fedha ndefu hizi, barabara, huduma za hospitali na shughuli mbalimbali za maendeleo zinahitajika kwa nini pesa ikae tu BOT ambapo yenyewe inatunza pesa tu ambazo kumbe zingekwenda kwenye shughuli za maendeleo. Zile hisa nyingine zilizobaki zigawanywe kwenye Manispaa nyingine ili Manispaa zote ziweze kumiliki UDA kwa pamoja. Hata hivyo, kama Serikali inaamua iachane nayo basi tujue imefika mwisho. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nipendekeze sasa labda Kamati ya PAC, LAAC zikutane kwa pamoja kulimaliza jambo hili. Kwa sababu kila Kamati ina uamuzi wake, ina uchunguzi wake, ina mapendekezo yake ambayo hayaishi. Kwa nini sasa sisi kama Bunge tusiungane pamoja tukamaliza jambo hili. Sasa UDA tunaona imeingia kwenye kazi nyingine mradi unazidi kuwa mkubwa halafu tunamuacha mwekezaji huyu ambaye hatujui wenzake ni akina nani na kazi gani anafanya, lakini baadaye hata huu mradi wa DART utatuingiza kwenye shida. Nina imani Serikali ni sikivu na Mawaziri wapo wanasikia.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni uhai wa Halmashauri. Kwa wale ambao hamfahamu hizi Halmashauri zilikuwepo zikafa kama ushirika lazima tuangalie nini kiliua Halmashauri zetu. Sasa hivi toka tulipokwenda kwenye uchaguzi mwezi Juni, 2015 pesa ya maendeleo haijaenda na hii quarter ndiyo kabisa pesa ya maendeleo haijaenda, kule kwenye Halmashauri zimelala hakuna kazi inayoendelea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwaambie Serikali pamoja na Waheshimiwa Wabunge tutaua hizi Halmashauri kwa mara nyingine tena kama hatukuwa makini. Tuliua Halmashauri hizi zamani, tukaua ushirika baadaye tumevirudisha vyama vya ushirika pamoja na Halmashauri, kutozipelekea pesa kunaua kila kitu. Athari zake ni nini? Toka tumemaliza uchaguzi wananchi wanadhani Serikali ipo likizo kwa sababu hakuna kazi inayoendelea kwenye Halamshauri zetu, Halmashauri zimelala, ofisi za Serikali za Vijiji hazichangamki. Siku zote kukiwa na pesa vijijini wanachangamka na utaratibu wetu ule wa kupeleka watu sita kwenda kusaini hata kama shilingi 200,000 hakuna sasa. Kwa hiyo, lazima tuhakikishe Serikali lazima ipeleke pesa kule. Pesa haziendi, tunasema madawati, tunasema hiki, sasa hivi kuna maboma mengi, litakuja agizo maboma yaishe, wanatoa wapi pesa? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zipo Halmashauri zinaishi kwa ubuyu. Samahani watani zangu Wagogo, zipo Halmashauri zipo hoi bin taabani lazima tuziwezeshe. Zipo Halmashauri mpya ambazo zinahitaji kuongezewa nguvu ili ziweze kusogea. Halmashauri hizi nyingine hazina mapato. Kulishawahi kutoka tishio hapa kwamba Halmashauri kama haikusanyi itajifuta, sasa mbona Serikali yenyewe haipeleki pesa na yenyewe itajifuta? Jambo hili haliwezekani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niwasihi sana Serikali tupeleke pesa za maendeleo ili maendeleo yaonekane. Pia ni namna gani tunatimiza ahadi au Ilani ya Chama cha Mapinduzi ni lazima pesa ziende kama haziendi tutakuwa tunarudi nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lipo suala la madeni. Halmashauri hizi pamoja na mambo mengine kuna Halmashauri zinadaiwa mpaka shilingi bilioni 16 na wadau mbalimbali, watoa huduma, tender, Halmashauri zitalipa lini. Kama Serikali tunalipa madeni ya nje sasa wakati muafaka umefika tulipe madeni ya ndani ili huduma ziendelee. Shule na vyuo wataanza kufunga kwa sababu hakuna mtu ataendelea kutoa huduma wakati halipwi. Kwa hiyo, Serikali tupelekeni pesa tulipe madeni ya ndani ili Halmashauri zetu zifanye kazi vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo mengi sana yametokea huko lakini kikubwa kingine tumeshindwa kuelewa Wakurugenzi wanatoa wapi kiburi cha kutokujibu hoja za CAG. Siyo hoja tu za CAG hata maagizo ya Kamati yaliyopita, Wakurugenzi wanakuwa na kiburi.
Mheshimiwa Naibu Spika, namshauri Mheshimiwa Waziri ajaribu kuliona hili kama CAG anadharauliwa, kama Kamati ya Bunge inatoa maagizo hayajibiwi maana yake ni dharau. Hebu tulirekebishe hili ili Bunge kama Bunge maana yake Kamati ni Bunge lichukue nafasi yake tukiwa tunatoa maelekezo na maagizo yajibiwe. CAG anatoa maelezo yake yajibiwe, kama yanakaliwa kwa kweli tunakuwa hatuitendei haki ripoti ya CAG. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, CAG hapiwi pesa za kutosha na kuna tishio mwaka huu CAG anaweza asikague Halmashauri hata kumi. Kwa hiyo, kama pesa haziendi kwa CAG ambaye ndiyo jicho letu sisi hatuna uwezo wa kwenda kwenye Halmashauri kugundua tunaletewa kitu kilichofanyiwa kazi. Niiombe Serikali pamoja na mwaka huu tulipiga kelele wakati wa bajeti hebu mchakato wa bajeti unaokuja tumuangalie kwa karibu sana CAG ili apewe pesa za kutosha kufanya kazi yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, siyo vizuri kupigiwa kengele la pili na mimi ni Chifu nisingependa kupewa adhabu, nakushukuru.