Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. Martin Alexander Mtonda Msuha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia taarifa zilizoko mezani kwako. Mimi nitachangia upande wa taarifa ya Hesabu za Serikali za Mitaa.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bunge la Bajeti la 2016/2017 asilimia 40 zinapelekwa kwenye kutekekeleza miradi ya maendeleo, lakini miradi hiyo mingi inatekelezwa katika ngazi za Halmashauri. Pia katika mabadiliko ya sheria za fedha yaliyofanyika mwaka huu yamepandisha kiwango cha kuiwezesha Halmashauri kusaini mikataba kutoka kwenye shilingi milioni 50 mpaka shilingi bilioni moja. Hii ina maana kwamba Halmashauri hizi zinapewa uhuru zaidi wa kufanya maamuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa upande mwingine tunazo oversight committees, tunayo Ofisi ya CAG na tunazo hizi Kamati. Kwa bahati mbaya sana tunakwenda contrary kwa maana kwamba hizo oversight committees zimenyimwa uwezo wa kifedha kwenda kufanya ukaguzi wa miradi. Kwa hiyo, tunachotegemea kuona baada ya mwaka huu wa fedha ni kwamba pengine miradi hii haijatekelezeka kwa kiasi ambacho kinaridhisha kwa sababu ya hizo oversight committees kunyimwa uwezo wa kifedha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya maeneo ambayo Halmashauri zote zilionekana kuwa na matatizo makubwa ni kwenye usimamizi wa mikataba na miradi ya maendeleo. Kati ya Halmashauri zote 66 ambazo tulizihoji mbele ya Kamati, zaidi ya asilimia 75 zilionekana kuwa na upungufu katika usimamizi wa mikataba. Mikataba mingi haikuweza kufikia mwisho kwa maana kwamba mingi ilivunjwa njiani na hivyo kuzisababishia Halmashauri kuingia gharama zaidi.
Kutokana na kuvunjika kwa mikataba hiyo ilisababisha pia miradi mingi kutokamilika kwa wakati na chini ya kiwango ambacho kilikusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, bahati mbaya sana miradi ambayo iliathirika zaidi ni ya maji. Maeneo mengi miradi mingi ya maji ambayo ilikamilika pia haikuweza kutoa maji, lakini mingine pia imekwama kwa kipindi cha muda mrefu. Kwa mfano, mradi wa maji Wilayani Tunduru wa Nalasi na Nandembo ilionekana kuwa imekamilika lakini haitoi maji na mkandarasi ameshasaini. Huu ni udhaifu katika usimamizi wa miradi ya maendeleo lakini pia mikataba husika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ipo miradi mingine kama mradi wa ujenzi wa madarasa katika Kata ya Namswea Ndongosi. Shule ya sekondari ilishakamilika siku nyingi, lakini haikuweza kutumika kwa sababu fedha hazijatolewa na Serikali Kuu kwa ajili ya kukamilisha hii shule ili iweze kutoa huduma ambayo imekusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo liliathirika sana kwenye hizi Halmashauri zetu ni matumizi nje ya bajeti. Halmashauri nyingi zimeonekana zimetumia fedha nyingi sana nje ya bajeti ambayo imepitishwa lakini Halmashauri hizi zilikuwa zinatumia kivuli cha maagizo kutoka kwa viongozi wa juu. Tulipowahoji kwamba hao viongozi waliwaambia wavunje Sheria za Matumizi ya Fedha za Umma wakasema hapana. Hiyo nayo ilipelekea kuathiri miradi mingi sana ya maendeleo kwa sababu fedha zote ambazo zilionekana kama ziko idle zilichukuliwa na kupelekwa kwa mfano kwenye ujenzi wa maabara kwenye shule zetu za sekondari. Bahati mbaya zaidi hizi maabara nyingi pia hazijakamilika japokuwa fedha nyingi sana zilichukuliwa kutoka maeneo mengine kwenda kutekeleza mradi huu wa ujenzi wa maabara.
Kwa hiyo, Kamati ilikuwa inashauri TAMISEMI wafanye juhudi pengine kwenda kutathmini ni kiasi gani fedha zilichukuliwa kutoka maeneo mengine zikatekeleza mradi wa maabara, lakini kuna tija kiasi gani imepatikana upande huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya miradi ambayo tulifanikiwa pia kuipitia ni mradi wa uuzwaji wa Shirika la Usafirishaji Dar es Salaam (UDA). UDA ni shirika la umma ambalo lilikuwa chini ya Hazina. Shirika hili lilikuwa na jumla ya mtaji wa hisa milioni 15 lakini Serikali iliamua ku-issue hisa milioni 7.1 na ikabakiza hisa milioni 7.8 ambazo hazikuwa allotted. Kati ya zile hisa ambazo Serikali ili-issue, zile milioni 7.1 iliamua kutoa hisa zake asilimia 51 kuipa Jiji la Dar es Salaam, lakini baadaye Jiji la Dar es Salaam waliamua kuuza hisa zao zile asilimia 51 kwa Kampuni moja binafsi ambayo inaitwa Simon Group.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baadaye pia Bodi ya UDA iliamua nayo kufanya mchakato wa kuuza zile unissued and unallotted shares za milioni 7.8. Hisa za Jiji zililipwa na Simon Group na fedha hizo zikawekwa kwenye akaunti ya Amana Benki Kuu na fedha hizo bado zipo kwenye Akaunti hiyo, Jiji halijaweza kuzitumia. Fedha ambazo zilipatikana kutokana na uuzaji wa hisa hizo ni kiasi cha shilingi bilioni 5.875. Baadaye Serikali iliona kwamba uuzwaji wa zile hisa ambazo hazikuwa issued na kuwa allotted za milioni 7.8 ilikuwa ni kinyume na sheria na taratibu. Kwa hiyo, Serikali iliamua kuzuia mauzo hayo na Simon Group aliamua ku-surrender hisa hizo kwa hiyo zikabaki chini ya Msajili wa Hazina mpaka hivi tunavyoongea. Pia zile fedha ambazo zilipatikana kutokana na uuzwaji wa zile hisa za Jiji zile bilioni 5.8 hazijaweza kutumika kwa ajili ya miradi ya maendeleo ndani ya Jiji la Dar es Salaam.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kusubiri baadhi ya nyaraka kutoka kwa Msajili wa Hazina ili jambo hili liweze kufika mwisho, Kamati ilikuwa inapendekeza mambo mawili; la kwanza, Halmashauri za Manispaa za Dar es Salaam ziweze kushirikishwa katika umiliki wa UDA ili ziweze kuwa wabia wa uendeshaji wa kampuni hiyo kwani ndiyo kampuni ambayo inategemewa kusafirisha abiria ndani ya Jiji la Dar es Salaam kwa kuwauzia baadhi ya hiza zile ambazo hazikuwa allotted za milioni 7.8.
Lakini pia tulikuwa tunapendekeza kwa vile hizi fedha shilingi bilioni 5.8 ambazo zimebaki BOT bila kutumika, Serikali ingetengeneza utaratibu wa kuangalia ni namna gani fedha hizo zinaweza zikaruhusiwa zitumike kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ndani ya Manispaa zinazounda Jiji la Dar es Salaam badala ya kuzibakiza ziwe idle katika Akaunti ya Amana Benki Kuu.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo liligusa karibu Halmashauri nyingi ni upotevu wa nyaraka za matumizi. Utakuta mkaguzi anakagua unakuta nyaraka za thamani kubwa tu hazionekani lakini baada ya wakaguzi kuwa wamemaliza kazi yao wametoka Afisa Masuuli anakuja na majibu kwamba nyaraka hizo sasa zimeshapatikana na ziko tayari kwa ukaguzi.
Kamati inauliza kama kweli nyaraka hizo zilikuwa ni halisi kwa nini zisipatikane wakati zoezi la ukaguzi linafanyika na siyo baada ya zoezi kumalizika na pengine baada ya miezi mingi sana ndiyo nyaraka hizo ziweze kupatikana? Hilo limeonekana ni eneo ambalo lina udhaifu mkubwa katika utunzaji wa hizi nyaraka kinyume na taratibu na sheria za fedha zinavyohitaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine lililoonekana kuwa na matatizo makubwa hasa kwenye Halmashauri mpya ni ufanyaji kazi wa Mfumo wa Uandaaji wa Taarifa za Fedha unaoutwa EPICOR. Halmashauri nyingi mpya hazijaunganisha kwenye mtandao huu kwa hiyo taarifa zao nyingi aidha wanatengeneza nje ya mfumo au wanasafiri kwenda kutengenezea kwenye Halmashauri ya jirani. Pia ilionekana kwamba taarifa nyingi haziwezi kutolewa na mfumo huu. Kwa hiyo, Serikali iangalie ni namna gani ya kuboresha mfumo huu ili uweze kukidhi mahitaji ya utengenezaji wa taarifa za fedha katika Halmashauri hizi husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ilionekana wahasibu wengi hawaufahamu vizuri mfumo huu. Wahasibu walio wengi hulazimika kutengeneza baadhi ya taarifa kwenye mfumo huu lakini taarifa nyingine kutengeneza nje ya mfumo na hivyo kukosa uwiano wa taarifa zinazotoka katika hiyo mifumo miwili.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuliona maeneo mengi yenye changamoto lakini kwa vile kuna wachangiaji wengi, naomba niunge mkono hoja na niwaachie wenzangu wagusie maeneo mengine. Ahsante.