Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili nichangie hoja iliyoko mbele yetu.
Kwanza nianze kwa kusema kwamba, naunga mkono hoja hii na nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa mapendekezo mazuri katika sekta ya elimu. Vilevile nipende kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wameleta michango mizuri kwenye elimu na kwa sababu ya muda sitaweza kugusia maeneo yote mliyoyazungumzia, lakini niseme tu kwamba michango yenu ni mizuri, tunashukuru sana na tutaizingatia tunapokuwa tunafanya mapitio na kutengeneza ule Mpango wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa tu kuzungumzia masuala machache na ningependa nianze na suala la elimu bila malipo kwa sababu limezungumziwa kwa nyanja tofauti, katika sura ya pongezi na katika sura ya kutoa changamoto na yote tumeyapokea.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa tu kuweka wazi jambo moja kwamba, suala la elimu bila malipo linaongozwa na Waraka wa Elimu Na. 6 wa mwaka 2015. Waraka huu umebainisha wazi majukumu ya Serikali, majukumu ya wazazi na wadau wengine wote. Kwa hiyo, kuna wengine wanakuja na dhana kuwa Serikali inafanya utapeli, kwamba imewaahidi wananchi kwamba itakuwa ni elimu bure lakini inachangisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni dhana potofu ambayo ningependa Watanzania waifahamu kwamba waraka umebainisha wazi kabisa, kuna majukumu ya mzazi ambayo bado mzazi atawajibika kumnunulia mtoto wake uniform, mzazi atawajibika kugharamia matibabu ya mtoto wake na kumnunulia vifaa vinavyotakiwa kwenda navyo shuleni. Serikali inatoa capitation grant kwa ajili ya wanafunzi, Serikali imeondoa ile ada ambayo mwanafunzi alikuwa analipa ambayo ni shilingi 20,000/= kwa mwanafunzi wa kutwa na shilingi 70,000/= kwa mwanafunzi wa bweni. Vilevile Serikali imeondoa gharama za mitihani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashindwa kuelewa kwa nini baadhi ya watu wanabeza, wakati nikiwa Baraza la Mitihani tulivyokuwa tunatangaza matokeo, wanafunzi wa Tanzania wengi kwa maelfu walikuwa wanazuiliwa matokeo yao ya mitihani kwa sababu ya kushindwa kulipa ada, leo hii Serikali imewaondolea, badala ya kushukuru, tunaibeza. Kwa hiyo, naomba tu niseme kwamba majukumu yameaninishwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa kuliweka wazi, Serikali haijakataza wananchi kuchangia katika maendeleo ya elimu. Imeweka wazi kabisa kwamba bado jamiii ina wajibu wa kutoa ushirikiano katika shughuli za kuleta maendeleo katika maeneo yao. Bado imeeleza wazi kwamba jamii ina wajibu wa kuendelea kujitolea nguvu kazi na mali ili kuleta maendeleo katika shule.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na Mbunge ambaye amechangia asubuhi, akasema kwamba kuna matatizo katika Jimbo lake na kwamba anatoa mifuko 1,500, Waheshimiwa Wabunge wengine wote ruksa fedha zenu za Mifuko ya Majimbo msije mkaacha kuchangia katika sekta ya elimu eti kwamba Serikali imekataza, hakuna hicho kitu. Nimeona nitoe huo ufafanuzi kwa sababu naona labda hii dhana inaweza ikapotoshwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuzungumzia kwa kifupi pia suala la ubora wa elimu ambalo limezungumziwa. Naomba niwahakikishie Watanzania kwamba Wizara yangu imejipanga na tuna nia thabiti kabisa ya kuhakikisha ubora wa elimu katika nyanja zote, kuanzia elimu ya awali mpaka elimu ya juu. Tutafanya hivyo kwa kuhakikisha kwanza kwenye elimu ya msingi mpaka sekondari tunafanya ufuatiliaji wa karibu, Wakaguzi wetu tayari wameshaelekezwa kufanya ufuatiliaji kwa kuangalia kile kinachofundishwa darasani, kwa sababu maarifa na stadi zinapatikana ndani ya darasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile mamlaka zetu ambazo zina wajibu wa kudhibiti elimu ya kati na elimu ya juu, tutahakikisha kwamba zinafanya kazi zao kwa weledi na vigezo vyao wanavyovitumia katika kuangalia kwamba chuo kinafaa, chuo kina sifa, ni lazima viwe ni vigezo ambavyo kweli vitatutolea wahitimu ambao wana ubora ambao tunauhitaji katika kuipeleka nchi yetu katika uchumi wa kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuzungumzia pia kidogo kuhusu elimu kwa watu wenye ulemavu. Nashukuru sana kwa michango iliyotolewa na niseme tu kwamba ni suala ambalo mimi kama mama, kama Waziri mwenye dhamana ya elimu linanigusa sana. Niseme kwamba Watanzania wenye ulemavu ni asilimia ndogo ukilinganisha na Watanzania ambao hawana mahitaji maalum. Hivyo basi Wizara yangu itahakikisha kwamba wana…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI, TEKNOLOJIA NA UFUNDI: Nashukuru sana Mwenyekiti naunga mkono hoja.