Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo; na Taarifa ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) pamoja na Maoni na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hiyo

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia hizi Kamati mbili. Niwapongeze Wenyeviti wa Kamati na Wajumbe kwa kazi nzuri. Naomba nianze na hili, kwamba Bunge ni mhimili unaojitegemea na sisi Wabunge kazi yetu ni kuisimamia Serikali, lakini hatuwezi kuisimamia Serikali kwa kupata taarifa tu kutoka kwenye taasisi mbalimbali bila kutembelea miradi ya maendeleo, huko sio kuisimamia Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, safari hii tumeshindwa kabisa kwa sababu Bunge halina fedha. Sasa nauliza, tulikuwa na Mfuko wa Bunge, huo Mfuko wa Bunge tulikuwa na fedha, je, Mfuko wa Bunge aliyeuondoa nani? Kwa sababu Mahakama wana Mfuko wao, Serikali na Bunge lilikuwa na Mfuko wake. Kwa hiyo, Bunge lazima liwe na fedha za kutosha kuwawezesha Wabunge, Kamati kutembelea miradi, huku ndiko kuisimamia Serikali. Hatuwezi kuisimamia Serikali kila siku tunakaa Dodoma kwenye Kamati, eti tunasubiri wataalam waje watoe taarifa, hapana, lazima tuisimamie Serikali kwa kutembelea miradi mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, mwezi wa Sita tumepitisha bajeti ya Serikali, lakini cha kushangaza sasa hivi wilayani hakuna fedha ambazo zimepelekwa kule, hakuna kabisa. Hakuna barabara inayotengenezwa, hakuna kisima kinachochimbwa, kwa mfano kwangu pale Wilaya ya Mpwapwa, kuna vituo vya afya viwili, Kituo cha Afya cha Mima pamoja na Kituo cha Afya cha Mbori, ni muda mrefu, miaka 10 havijakamilika vituo vile, ni kwa sababu fedha hazipo. Sasa mwaka huu vile vituo vimetengewa, kwa mfano Mima imetengewa milioni 25, lakini hizo fedha sijui kama zimeshapelekwa au hazijapelekwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Kituo cha Afya Mbori kimetengewa milioni 20, sijui kama pesa zimeshapelekwa au hazijapelekwa, ni miaka 10 havijakamilika. Akinamama wajawazito wanapoteza maisha kwa sababu ya usafiri kutoka Mima kwenda Mpwapwa. Kwa hiyo, naiomba Serikali, pamoja na matatizo, haya mazingira magumu ya ufinyu wa bajeti lakini fedha zipelekwe kwenye halmashauri zetu ili miradi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, kuhusu utendaji wa halmashauri, halmashauri zinafanya kazi katika mazingira magumu. Halmashauri zilikuwa zinapata fedha toka TAMISEMI kwa ajili ya fidia, kwa sababu halmashauri zilikuwa zinakusanya kodi, kwa mfano kodi ya mafuta, kodi ya hoteli, Serikali kuu ilikuwa ndiyo inayokusanya na sasa kodi ya majengo inakusanya TRA. Kwa hiyo, tunaomba kama TRA watakusanya hiyo kodi, basi wapeleke hizi fedha haraka, wasikae nazo mpaka halmashauri tuanze kudai tena, hapana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine asilimia 20; vijiji vina miradi mbalimbali, sasa vijiji vimekwama kutekeleza miradi yao kwa sababu hawana fedha na wanategemea hii asilimia 20, lakini asilimia 20 haiwezi kupelekwa vijijini kwa sababu halmashauri hazina fedha. Halmashauri nyingi hazikusanyi vizuri mapato ya ndani, usipokusanya mapato ya ndani huwezi kupeleka hii asilimia 20 kwenye Serikali za Vijiji. Nataka nijue, kwa sababu Waziri na Naibu Waziri wapo; hivi ni kweli ile fidia waliyokuwa wanapeleka halmashauri ya kufidia hii kodi ya maendeleo ambayo ilifutwa na ushuru mbalimbali wa halmashauri, wamesitisha au bado wanapeleka?
Mheshimiwa Naibu Spika, hii asilimia 10 ya akinamama na vijana, hii ni revolving fund wala siyo zawadi. Nakubaliana na Kamati, kwamba halmashauri zitenge asilimia 10 kwa ajili ya kuwapatia akinamama na vijana, lakini warejeshe hii mikopo, bila kurejesha hii mikopo vikundi vingine haviwezi kupata mikopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu manunuzi, pamoja na kwamba tumerekebisha Sheria ya Manunuzi hapa, lakini halmashauri nyingi bado karibu asilimia 75, fedha zinapotea kwenye manunuzi kwa sababu hawafuati utaratibu. Kwa hiyo, lazima halmashauri zisimamamiwe ili kufuata Sheria hii ya Manunuzi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utengenezaji wa magari, hivi najiuliza, halmashauri za wilaya hazina gereji au kila halmashauri inatengeneza magari inapotaka? Ndiyo maana gharama zinakuwa kubwa na halmashauri zinakosa pesa
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ukaimu, ni halmashauri nyingi. Nimekuwa Mjumbe wa Bodi ya Mikopo ya Serikali za Mitaa, nimetembelea halmashauri nyingi sana, watumishi wengi wanakaimu. Sasa kama anakaimu, Mheshimiwa Waziri, kama mtumishi huyo ana sifa kwa nini asithibitishwe kazini apate kile cheo. Ukaimu una mwisho wake, miezi sita, lakini mtumishi anakaimu zaidi ya miaka miwili, miaka mitatu, huo ni ukaimu wa namna gani, lazima wathibitishwe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ya kwangu yalikuwa hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kwa hiyo, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja za Kamati zote mbili, Kamati ya LAAC pamoja na Kamati ya PAC.