Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.

Hon. Sixtus Raphael Mapunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Mkataba huu wa ubia baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Jumuiya ya Ulaya.
Mheshimiwa Spika, awali ya yote niwapongeze waliotangulia kuupinga huu mkataba kwa nguvu kubwa na maneno mazuri yalio-base kwenye content nikianzia na mchangiaji wa mwisho Cosato Chumi aliyechangia kabla ya mimi, michango ya Mheshimiwa Kabwe Zitto, Mheshimiwa Azzan Zungu, Mheshimiwa Hawa Ghasia, Mheshimiwa Hussein Bashe na wengine wote, wameenda vizuri sana kwenye content, na Mheshimiwa Hamidu Bobali na chama chake na Mheshimiwa Khatib Said Haji.
Mheshimiwa Spika, sitakwenda kwenye content nitagusa mambo ya jumla ambayo ninadhani jumba lako hili Tukufu ni vema likajua ili tuweze kwenda katika mtiririko mzuri. Kuna watu wamesema hapa, nakubaliana Tanzania siyo kisiwa na wengine wamesema tusiikimbie hii ndoa, hii ndoa ni muhimu ni nzuri ina mazuri yake ni vema tukayatafuta mazuri yaliyoko sirini yasiyoonekana ili tuone kuna nia njema ndani ya hili. Naomba niseme machache yafuatayo:-
Mheshimiwa Spika, nchi yoyote inapoamua kufanya urafiki na Taifa lingine lolote, kuna mambo inapoteza kama Taifa na kuna mambo inayapata kama Taifa, kwa maneno mepesi, mahusiano yoyote baina ya mataifa yanaunganishwa na principle ya statism, principle ya self-help na principle ya survival. Katika mazingira yoyote yale unapoingia kwenye makubaliano na Taifa lolote lile, kanuni ya kwanza inayopaswa kuku-guide, una interest gani kama Taifa kwenye ule mkataba.
Mheshimiwa Spika, jambo la pili, unalopaswa kuliangalia, utanufaika kwa kiwango gani katika ule mkataba? Lakini kuna mazingira mengine, unaweza usinufaike, ila ule mkataba ukakusaidia kuishi uione kesho yako, labda kuwakimbia maadui hiyo ndiyo inayoitwa national survival.
Mheshimiwa Spika, yawezekana kuna wengine wanayatafuta mazuri kwenye Mkataba huu kwa sababu tu ya ule woga katika makubaliano kuna mchawi asiyeonekana, yaani wanatafuta ku-survive sehemu ambayo hakuna survival. Niwaombe ndugu zangu Wabunge, historia ya nchi yetu tumeshirikiana na mataifa mengi katika nyakati tofauti. Kuanzia karne ya tano tuliposhirikiana na nchi za Mashariki ya Mbali na nchi za Uarabuni mpaka kipindi nchi za Ulaya zilipoingia, kipindi cha ukoloni na mahusiano baada ya uhuru. Wote mmeona kila Tanzania tulipojikwamua kutoka kwenye makucha ya kutaka kuendelea kumekuwa na uhusiano wa mjomba wa kuturudisha nyuma.
Mheshimiwa Spika, tumetoka kuanzia mwaka 1961 mpaka leo tunaongea mwaka 2016, kuna mikakati mingi sana tumeipanga kama Taifa, kuna mikakati mingi sana tumeipanga kama nchi na majirani zetu, kuna mikakati imefanikiwa na mikakati haikufanikiwa. Ni jukumu letu sasa kujiuliza kama Taifa, haya mahusiano tuliyowahi kuyafanya nyuma yalitusaidia kwa kiasi gani? Na haya mahusiano tunayotaka kuyafanya sasa yana tija kiasi gani?
Mheshimiwa Spika, niwakumbusheni ndugu zangu Wabunge, tulishawahi kugawanywa katika block mbili, block ya East na block la West. Mnakumbuka kipindi cha cold war. Nchi yetu kama Taifa ilisimama ikasema hatutageuka kulia wala kushoto tutakwenda katika mfumo ambao tunaona nchi yetu ina maslahi nayo, hatukugombana na Wamarekani na Waingereza na wala hatukugombana na marafiki zetu wa Urusi.
Mheshimiwa Spika, leo tunavyokwenda kuujadili mkataba huu, ni mkataba wa kwanza ndani ya nchi yetu kuwekwa fungu moja as a bargaining block against European Union. Haikuwa kutokea huko nyuma na wala hatukuwahi na experience ya kundi zima tukawa na interest sawa, tukawa na historical background sawa, tukawa na matamanio sawa, tukawa na ndoto sawa, leo tukae kwenye meza ya majadiliano against a huge block - European Union.
Mheshimiwa Spika, ninaona kuna tatizo, kuna matatizo mawili; tatizo la kwanza si mahusiano yetu na Jumuiya ya Ulaya na wala siyo mahusiano yetu na majirani zetu wanaotuzunguka, tuna tatizo la kwanza la content, mambo yaliyopo ndani ya mkataba ambayo tunayapinga. Kwa bahati mbaya sana kwa hatua tuliyofikia, hatuna fursa ya kuchambua kifungu kimoja baada ya kingine, tuna fursa moja tu sasa hivi ya kuukataa, kwa sababu ya kukubali hatunayo. Baada ya kukataa hayo mazuri msiyoyaona hapa mnayodhani yapo, ndiyo yatakuja.
Mheshimiwa Spika, leo hii hapa tujadili nini, tu-suspend, uende halafu urudi, hapana. Hatuna fursa hiyo, tuna fursa leo ya kusema Serikali isaini mkataba au Serikali isisaini mkataba. Kutokana na hoja zote zilizotolewa ndani humu na Wabunge, nakubaliana na ninaiomba Serikali isisaini mkataba huu. Kwanza, haujatupa room ya kufanya marekebisho, kama kutaonekana huko mbele kuna haja ya kurekebisha vifungu tutakwenda.
Mheshimiwa Spika, tuna marafiki zetu wametangulia, ndugu zetu Walatini wana msemo amicorum omnia communia wakimaanisha between friends all is common au wakimaanisha for friends all things are shared. Sasa kwa style ya wenzetu wanavyokwenda tunaona ile principle ya amicorum omnia communia haipo, hatuoni kitu hapa kinachoenda in common. Walishakaa Wakuu wetu wa nchi wakasema tujipe muda wa miezi mitatu, wenzetu wamekwenda speed.
Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie kwa kusema machache yafuatayo; umefika wakati sasa kwa Watanzania kutoka kwenye giza nene la urafiki wa kinafiki wenye lengo la kudidimiza na kuua ndoto ya Tanzania kuwa na viwanda. Umefika wakati sasa kwa Tanzania kutoridhishwa na aina hii ya urafiki mpaka pale mishipa yetu ya fahamu itakapojiridhisha kwamba urafiki huu haufanani na ule urafiki wa paka na panya kukumbatiana na kubusiana ilhali shimo la panya la kutorokea liko mbali.
Mheshimiwa Spika, wakati sasa umefika kwa Watanzania kutokuwa na kiu ya kutaka kunywa maji ambayo yako kwenye kikombe cha mateso, uchungu na maumivu makubwa.
Mheshimiwa Spika, kwa maneno haya, siungi mkono hoja na ninaiomba Serikali isipitishe na isisaini mkataba huu. Ahsante sana.