Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mkataba wa Ubia wa Uchumi baina ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Umoja wa Ulaya.

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Spika, nimesimama mbele yako kwanza, kukushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia na kumshukuru Mwenyezi Mungu pia kwa kunipa afya kuweza kusimama na kuchangia katika mkataba huu.
Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kuanza kwa kumwomba Rais wangu kipenzi, Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, asiusaini mkataba huu kwa manufaa ya Watanzania. Tunamwomba sana kama Wabunge, kwa sababu mkataba huu hauna manufaa hata kidogo kwa Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, sisi kutokusaini huu mkataba hatuwi wa kwanza na wala hatuwi kituko. Kwa upande wa SADC, Angola hawajasaini; kwa upande wa ECOWAS, Nigeria na Gambia hawajausaini mkataba huu. Kwa hiyo, sisi hatuwi wa kwanza kuukataa mkataba huu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mkataba huu hauna manufaa yoyote na Watanzania kwa sasabu zifuatazo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza, kwa mujibu wa takwimu za Benki Kuu, nchi kumi ambazo Tanzania tunafanya nazo biashara, nchi ambazo sisi tunachukua bidhaa, tuna-import kutoka kwao, ya kwanza ni Saudi Arabia; ya pili, ni China; ya tatu, ni India; ya nne, ni Falme za Kiarabu; ya tano, ni Afrika Kusini; ya sita, ni Uswiss; ya saba, ni Japan; ya nane, ni Marekani; ya tisa, ni Kenya; na ya kumi ni Andorra. Katika hizo nchi kumi, nchi za Ulaya ni Uswiss peke yake. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, ukienda kuangalia katika nchi ambazo sisi tunapeleka bidhaa zetu katika zile top five; ya kwanza ni China; ya pili ni India; ya tatu, ni South Africa; ya nne, ni Saudi Arabia; na ya tano, ni Kenya. Hakuna nchi yoyote ya Ulaya hapo.
Mheshimiwa Spika, pia ukiangalia katika FDI; ya kwanza ni Uingereza ambayo na yenyewe ni inajitoa kwenye Jumuiya ya Umoja wa Ulaya; ya pili, ambayo ndiyo itakuwa ya kwanza, kwa sababu Uingereza inatoka katika Jumuiya ya Ulaya, ni India; ya tatu ni Kenya; ya nne, ni Netherland; inafuata China, Marekani, Afrika Kusini, Canada, Ujerumani na Oman. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nchi zenyewe za Ulaya unaziona ni kama mbili tu. Kama tunataka kuua biashara zetu, kama tunataka kuua viwanda vyetu, tuingie katika huu mkataba. Wanachotaka hawa ni kutaka kuchepusha mfumo wetu wa biashara. Wanataka kututoa tusifanye biashara na Saudi Arabia, China na India; na kwa sasa hivi, masuala ya biashara wanaotawala duniani ni China, India na Marekani. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hawa Jumuiya ya Ulaya wanataka kuturudisha tena tulikotoka. Wanataka tena scramble for Africa, hatuko tayari. Pia wanachokifanya Jumuiya ya Ulaya, kwa sababu makubaliano ya EPA ni kusaini Jumuiya ya Afrika kama nchi moja na sio mmoja, mmoja. Kwa hiyo, wanachotaka ni kuvunja Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki. Tuwaambie kabisa, Jumuiya ya Ulaya kwa kuanza kusaini na nchi moja moja badala ya kanda nzima kama Afrika Mashariki, wanataka kubeba dhima ya kuuwa Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, narudia tena, namwomba Mheshimiwa Rais, kwa kweli asisaini mkataba huu. Kuna mtu amesimama hapa akasema tusomewe mazuri yaliyoko katika mkataba. Mkataba tumekabidhiwa, angeusoma huu mkataba akatueleza yeye mazuri. Yeye anasimama, anasema tusaini, lakini hajasema hata moja zuri, anakusudia nini? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, napenda nimuunge mkono Mheshimiwa Bobali aliyesema hivi sisi, tuna kitu gani tunachoweza kwenda kuuza Ulaya? Sana sana sisi tunategemea malighafi; tunategemea kuuza nyama, samaki, lakini je, tuko tayari? Tunao uwezo wa kushindana na bidhaa kutoka Ulaya au sisi tunataka kufanywa soko la kuja kutupa bidhaa zao za kuja hapa? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nchi za Caribbean ambazo zilijiunga, tafiti zinaonesha zimepoteza mapato yao kuanzia mwaka 2009 hadi 2013, wamepoteza zaidi ya Euro milioni 74.
Mheshimiwa Spika, narudia tena, tusisaini mkataba huu, hao wanaoshabikia, ndio wafadhili wao. Sisi hatuko tayari kusaini mkataba ambao pia katika kifungu cha 96 cha Cotonou ambacho kinaoanisha na Ibara ya 136 ya EPA pia haki za binadamu zimo, ambamo ushoga umo. Tuko tayari sisi kuingizwa kwenye ushoga kwa kupitia hii biashara? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, narudia tena kusema siungi mkono hoja. Mkataba huu Mheshimiwa Rais tunakuomba usiusaini.