Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshmiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Napenda kumpongeza sana Dkt. Mpango, Naibu wake na Makatibu Wakuu na timu nzima ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa kazi nzuri ya kuandaa Mpango na kuuwasilisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumefarijika na kama Serikali tumeweka hifadhi ya mazingira kama vipaumbele muhimu katika mipango ya maendeleo ya nchi. Wakati wa bajeti Serikali italeta mipango ya kina ya kueleza tafsiri yake hasa ni nini na nini kitafanyika katika kuhakikisha kwamba hifadhi ya mazingira inazingatiwa katika mipango ya maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba nimefadhaika kidogo kwa michango iliyotoka hapa Bungeni kwa Wabunge walio wengi. Sisi Wabunge bila kujali Majimbo yetu, shida za watu wetu zinafanana bila kujali Jimbo ni la Upinzani au ni la CCM. Unapoikejeli Serikali, unapomkejeli Rais, unapowakejeli Mawaziri, angalau acha fursa ya uwezekano wa kuomba ushirikiano, kufanya kazi na Serikali hiyo hiyo, Rais na Mawaziri hao hao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ndiyo wenye Serikali, ndiyo tunapanga bajeti, ndiyo tunatekeleza maendeleo. Acha fursa ya ubinadamu wa kuweza kufanya kazi kwa pamoja. Mimi naelewa kwamba Upinzani kazi yao kulaumu, lakini ipo fursa ya kutoa Mpango mbadala. Hivi ninyi kwa kazi anayoifanya Mheshimiwa Magufuli leo, kipi mngefanya tofauti? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Bunge lililopita walikuwa wanatulaumu kuna uzembe, kuna ubadhirifu, kuna ufisadi; Mheshimiwa Magufuli anatibu uzembe, ubadhirifu, ufisadi bado mnatulaumu. What would you have done differently, leo kama mngekuwa na Serikali? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na tishio hapa, watu wanazungumza amani itavurugika. Maarifa yaliyounda nchi yetu, maarifa yaliyounda Muungano wetu, maarifa yaliyolinda amani yetu mpaka leo ni makubwa kuliko ukomo wa kufikiri wa baadhi ya watu hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Muungano wetu utadumu, amani yetu itadumu, nchi yetu itakuwa moja, hizi kauli za kutisha kwamba nchi italipuka, kutakuwa na mvurugano, tusiwatishe wananchi dola ipo na busara ya viongozi ambao walishiriki kwenye kuiunda nchi hii ipo. Wapo ndani ya Chama cha Mapinduzi, wapo ndani ya Serikali, nchi yetu itaendelea kuwa ya amani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ufumbuzi wa suala la Zanzibar, naelewa haja ya kuonesha hisia ndani ya Bunge hili, lakini ufumbuzi haupo ndani ya Bunge hili. Ufumbuzi wa suala la Zanzibar haupo kwenye Ofisi za Mabalozi wa kigeni, ufumbuzi wa suala la Zanzibar haupo barabarani na mitaani. Ufumbuzi upo ndani ya Katiba na ndani ya Sheria za Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu kwamba tupo kama Serikali, tupo imara, tutafanya kazi yetu bila uoga, bila wasiwasi na Mheshimiwa Rais anafanya kazi nzuri, anaungwa mkono na Watanzania wote na wenzetu msione aibu kumuunga mkono. Siyo dhambi kama mtu anafanya kazi nzuri, kama Serikali inafanya kazi nzuri, kama Mawaziri wanafanya kazi nzuri, siyo dhambi kuwaunga mkono kwa sababu nchi yetu ni moja, kazi yetu ya kuleta maendeleo ni moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.