Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika mwelekeo wa mpango huu wa mwaka 2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze na suala hili la mashirika ya umma, Mama Lulida alikuwa kazungumza hapa siku ya jana akieleza kwa masikitiko makubwa sana. Alikuwa amezungumza kwamba baadhi ya mashirika ambayo takribani tuko nayo Tanzania kwa kiasi kikubwa mashirika ya umma yanaendeshwa kihasara. Yapo mashirika mpaka hivi sasa ninavyozungumza, miradi na mali walizokuwa nazo takribani na madeni yote madeni waliyokuwa nayo inazidi mali walizokuwa nazo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa mfano Shirika la Mbolea Tanzania (TFC), wakati tunapitia mpango wao katika Kamati ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma, unaweza ukashangaa sana kwamba deni walilokuwa nalo ni takribani shilingi bilioni 66. Lakini madeni, mali waliyokuwa nayo, mali nzima ukiuza majengo na kila kitu wana mali zenye thamani ya shilingi bilioni 23.8. Kwa hiyo, unaweza ukaona ni jambo la ajabu sana kwamba haya mashirika yamefilisika, Serikali, Waziri wa Fedha na Mipango, sijaona wakati napitia taarifa yake hapa na mwelekeo wa mpango hajaeleza kinaga ubaga kwamba kuna mkakati gani wa kuhakikisha kwamba anafufua mashirika haya ya umma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tumeona hapa na Wabunge wengi wamezungumza kwa kiasi kikubwa sana kwamba Serikali imekuwa ikikopa kwenye mashirika haya, mashirika ya fedha na mashirika ya umma ya ndani ya nchi. Tuhakikishe kwamba tunaweka mikakati kabambe ili haya mashirika yaweze kufufuliwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia uendeshaji wa haya mashirika, yanaendeshwa kinyume na taratibu za kimaadili. Kwa mfano, mwaka jana tuliweza kuzungumza katika mpango hapa kwamba yapo baadhi ya mashirika yanatumia madaraka yao vibaya. Kwa mfano, Shirika la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kiliweza kuingia mkataba na mwekezaji kotoka Botswana, mkataba ambao haunufaishi Serikali. Lakini jabo la ajabu tuliweza kuzungumza katika mpango tukaongea kwenye bajeti hapa, lakini kwenye mpango aliokuja nao Mheshimiwa Mpango hapa hakuna mwelekeo wowote kwamba kuna nini kitafanyika ili kuhakikisha ya kwamba haya mashirika ambayo yanawekeza kinyume na taratibu na sera za uwekezaji Tanzania na kwamba hayaingizi kipato katika Serikali yetu yanachukuliwa hatua stahiki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ukisoma mkataba wa Mlimani City ambao Mbotswana aliingia kwa kiasi kikubwa yule jamaa anakusanya pesa nyingi sana. Lakini jambo la ajabu Serikali inakusanya asilimia 10 tu ya mapato yote na hakuna uhakiki wowote ambao unafanyika wa kuhakikisha kwamba kile anachokusanya kinafanyiwa mahesabu sawasawa ili ile asilimia 10 ama anapata zaidi ya ile asilimia 10 anayotoa Serikali ya Tanzania iweze kunufaika. Ni kwa sababu mipango yetu haioneshi namna gani tunaweza kuweka mazingira ya kiuwekezaji ambayo hawa wawekezaji kutoka nje wanaweza kuliingizia Taifa hili pato.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia suala zima ambalo niliweza kuzungumza katika mpango uliopita, kwamba mashirika haya kwa mfano PSPF, wamekuwa wakiwekeza kwenye viwanja kwa kiasi kikubwa sana na wakati wananunua hivi viwanja wananunua square meter moja kwa pesa nyingi sana kinyume kabisa na bei halisi na halali katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, niliweza kueleza hapa, na leo naomba nilizungumze tena, Shirika la PSPF waliweza kununua kiwanja Mjini Mwanza square meter moja walinunua shilingi 250,000, ndani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lakini ukija kule Mtwara pia, wamenunua square meter moja shilingi155,000, maeneo ambayo bei hiyo haijafika, ni kwa sababu mashirika haya yanawekeza kiufisadi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana katika mpango huu tuhakikishe ya kwamba haya mashirika yanapitiwa upya na waweze kuja na mpango kabambe ambao utaweza kuinua uchumi wa nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze pia suala zima la PPP (sekta binafsi). Tumeweza kuzungumza kwa muda mrefu katika Bunge hili kwamba hawa wawekezaji kutoka nje ya nchi ndio ambao wanategemewa sana na Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi, ambao tunawategemea wajenge viwanda na vile viwanda viweze kutoa ajira. Lakini cha ajabu mazingira mpaka leo tunavyozungumza sio rafiki kwao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza hapa wakati wa mpango uliopita na nikazungumza wakati wa bajeti pia, kwamba tunao wawekezaji wamejenga viwanda, kwa mfano mwekezaji huyu Aliko Dangote kule kiwanda cha saruji Mtwara, lakini mpaka leo huyu mwekezaji ananyimwa kupewa gesi ambayo anaweza kuitumia kama nishati ili sasa bei ya saruji iweze kushuka na saruji iweze kuzalishwa kwa wingi Tanzania na watu wengi waweze kujenga, ni jambo la ajabu sana. Tunaomba sana hawa wawekezaji wapewe gesi, mwekezaji huyu wa saruji apewe gesi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuna mwekezaji wa mbolea ambayo ni kwa muda mrefu hivi sasa, tuliongea wakati wa mpango, wakati wa bajeti pia tulizungumza, ambaye anaomba apewe gesi aweze kujenga kiwanda cha mbolea Msangamkuu pale Mtwara Vijijini. Mpaka leo yule mwekezaji hajapewa hiyo gesi. Tunaomba Waziri Mpango atakapokuja kuhitimisha atupe maelezo kwamba mpango ukoje wa mwakani wa kuhakikisha kwamba hawa watu, hawa wawekezaji wanapewa hii gesi ili iweze kunufaisha katika sekta hii ya viwanda na kweli iweze kuinua uchumi wa Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nizungumze suala zima la miundombinu ambalo tumezungumza kwa kiasi kikubwa sana, lakini sijaona mkazo katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mpango hapa wakati anazungumza. Tulizungumza sana kwamba uchumi wowote hauwezi kuimarika popote duniani kama miundombinu ni hafifu. Tunayo miundombinu ya barabara ambayo imesimama hivi sasa na tuliweza kuzungumza, kwa mfano barabara kadhaa za hapa nchini kama ile barabara ya Ulinzi kule Mtwara ambayo sijaona kwenye mwelekeo wa mpango wapi imewekwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliweza kuzungumza pia reli ya kutoka Mtwara kuelekea Liganga na Mchuchuma ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza. Kwa hiyo, niombe sana kwamba kama kweli tunahitaji kufufua uchumi tuhakikishe kwamba tunajenga miundombinu imara ili kweli Watanzania waweze kuondokana na umaskini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa sababu ya muda.