Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. William Vangimembe Lukuvi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ismani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi ya dakika tano. Kama tulivyokuwa tunajadili hotuba ya Mheshimiwa Rais, Wabunge wengi wamerudia maneno mengi ambayo yalisemwa wakati ule. Nataka kurudia kuwaahidi kwamba katika kutayarisha Mpango huu, sekta ya ardhi ni msingi na muhimu sana katika maandalizi ya kujenga uchumi kama ilivyoandaliwa. Hivyo, nataka kuwaahidi kwamba yale yote waliyozungumza tutashirikiana na Mheshimiwa Waziri wa Fedha kuhakikisha mikakati mbalimbali ya kuboresha ardhi ili iweze kutumika vizuri katika uchumi tutaifanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na michango hii, nataka niseme moja, jana Mheshimiwa Mbunge mmoja Anatropia Theonest, kwanza nataka nimwombe radhi Mheshimiwa uncle wangu Tundu Lissu amejitahidi lakini naona niliseme kwa sababu tunamaliza. Jana alinihusisha kwa jina kwamba mwaka 2011 nilikuwa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, kwa hiyo nilihusika sana katika kupora viwanja vya Mabwepande.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi hata waandishi wa habari wamerekodi kama ilivyo hata kutafakari kidogo, mimi 2011 nilikuwa kwenye kiti hiki hapa, nilikuwa Chief Whip. Sasa mdogo wangu wa Segerea, ungechanganya kidogo tu ungejua kwamba unayoyasema hata kama umeambiwa ungetumia na akili yako, ungejua, lakini sikutaka kuingia kwenye huo mjadala kwa sababu nilimwomba Chief Whip wa Upinzani ashughulikie nafikri imeshindikana, lakini nimekuandikia Mheshimiwa Mwenyekiti barua nafikiri kama ana ushahidi atakuletea ili tuendelee na safari hii kwenye Kamati ya Maadili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nataka kusema, Mpango wa Serikali, mpango unaosimamiwa na Wizara yangu ni kuhakikisha kila kipande cha ardhi kinapimwa ili kila mwananchi aweze kumiliki. Ni kwa kumiliki ardhi kila mtu ndipo tutaongeza na mapato ya Taifa na ndiyo maana speed ya umilikishaji sasa tunaitilia umuhimu na hata sasa nimeagiza, speed ya utoaji hata tittle ambayo ilikuwa ni miezi sita sasa tumeanza kutoa hati kwa mwezi mmoja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili la migogoro, hatuwezi kuujenga uchumi kama hatuna utulivu. Wananchi wanagombana kati ya hifadhi, vijiji na watu binafsi. Kwa hiyo, nataka kuwahakikishieni taarifa zenu tumeshazipata. Hili halihitaji Mpango kuandikwa, sisi tukitoka Bunge hili tunaanza. Taarifa zenu zilizokuja na Mheshimiwa Maghembe na TAMISEMI tutaanza kushughulikia ili kuhakikisha kwamba watu tunawapa raha, waweze kusimamia shughuli zao za maendeleo ya kiuchumi kwa kupunguza migogoro iliyopo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanzia upimaji kama nilivyosema, mwezi huu tutaanza Wilaya ya Kilombero na Ulanga kama Wilaya za mfano za upimaji wa kila eneo. Upimaji huu hautanyang’anya ardhi ya mtu, lakini tutahalalisha ardhi yake na tumpe karatasi zitakazomwezesha kutambulika Kiserikali kwamba ni mmiliki halali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza hizo wilaya, tutaona mfano huo na gharama zake ili twende kufanya nchi nzima. Kwa hiyo, nataka kuwahakikishia tu Waheshimiwa Wabunge, sekta ya ardhi tutasimamia mawazo yenu, haya yaliyopo kwenye mpango na yale ambayo ni ya utekelezaji wa muda mfupi maana yake haya ya mpango yanaweza kuwa yameandikwa machache, lakini tuliyoyasikia ni mengi, tutasimamia ili kuhakikisha kwamba Sekta ya Ardhi inakuwa kwa manufaa Watanzania wenyewe wa nchi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naomba tu kwamba, wakati mwingine kumekuwa na dhoruba za kutupiana maneno, upande wa rafiki zangu hawa, wakati mwingine wanatumia maneno makali sana kwa Mawaziri, wanasahau kwamba Mawaziri hawa ni Wabunge kama ninyi. Hata hivyo, haipiti dakika moja, wana-cross kwa Mawaziri hao hao wanataka kuteta. Sasa mfikirie jamani, binadamu hawa wote tunafanana, haiwezekani huyo Waziri umwite tapeli, mjinga halafu una-cross hapa akusikilize kama vile hukusema kitu. (Makofi)
Ningependa tujenge hoja kama Mbatia, kama Zitto Kabwe, hoja nzito lakini hazina kashfa wala matusi kwa mtu mmoja mmoja, kwa sababu Mawaziri hawa siyo vyuma, ni binadamu. Kwa hiyo, naomba tu, wote hapa ni marafiki na Serikali haitawabagua, itawatumikia wote, lakini tukiwa…
WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.