Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. AMINA S. MOLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uzima na kuweza kusimama mbele ya Bunge hili Tukufu ili nami niweze kuchangia mawili matatu katika kuishauri Serikali yangu. Vilevile nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza zaidi katika kutoa ushauri na ushauri wangu utakwenda hasa kwa kuzingatia Wizara mbili ili kuweza kuishauri Serikali yangu katika mpango huu kwamba tunapoandaa mpango huu wa bajeti ya Serikali kwa mwaka 2017/2018 ni mambo gani ya msingi ambayo yanahitaji kuzingatiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukurasa wa 45 naomba kunukuu kwamba, hapa Waziri anasisitiza Maafisa Masuuli wanapaswa kujumuisha masuala mtambuka katika mipango na bajeti ya mwaka 2017/2018 na kwamba, ili kufanikisha lengo hili kila Wizara, Idara Zinazojitegemea na Wakala, Sekretariati za Mikoa, Mamlaka za Serikali za Mitaa na Taasisi za Umma zinasisitizwa kutenga fedha za kutekeleza vipaumbele kwenye masuala mtambuka. Vipaumbele hivyo ni pamoja na masuala ya kijinsia, vilevile masuala ya watu wenye ulemavu katika kuangalia hasa suala zima la ajira, afya, elimu na ujenzi wa miundombinu rafiki kwa watu wenye ulemavu. Naomba nijikite katika haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango huu au mwongozo huu wa bajeti umeeleza tu in general kwa sababu haujaweza kufafanua na kusisitiza masuala hayo kwamba yatatekelezwa vipi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, tunapozungumzia huduma muhimu za kijamii na hivi sasa katika Serikali yetu tunatoa elimu bure, lakini suala la kijinsia hasa kwa watoto wa kike na katika bajeti iliyopita, halikupewa kipaumbele kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kwamba mahitaji muhimu kwa watoto wa shule hasa wasichana yamezingatiwa kwa kiasi gani. Mfano, tunafahamu kabisa watoto wa kike na hasa watoto wa kike wa vijijini na hata wale wa mijini tunafahamu kwamba, kwa mwezi wanakosa kuhudhuria masomo kwa siku nne, tano mpaka saba na hii ni kutokana na siku zao zile ambazo ni muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali na najua Mheshimiwa Waziri ni baba na baba ana watoto na watoto hao wapo watoto wa kike wa kwake, lakini pia jamii yote kwa ujumla hao watoto wa kike tunawaangalia vipi! Mfano, katika vyoo, vyoo hivi vya shule na hasa maeneo mengi unakuta kwamba shule nyingi zina matundu matano mpaka saba na katika Sera ya Elimu inasema kwamba, matundu ya vyoo vya shule kila choo idadi ni 20 kwa 25, ishirini kwa watoto wa kike na ishirini kwa wavulana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watoto wa kike wana mahitaji muhimu mfano, tunazungumzia huduma za maji, mtoto huyu wa kike akiwa katika siku zake anahitaji pia maji, je, tumejipanga vipi katika bajeti zetu kuhakikisha kwamba maji yanakuwepo ili watoto hawa wa kike waweze kujisitiri vizuri!
Mheshimiwa Mwenyekiti, je, katika bajeti yetu pia tumejipanga vipi na je, Serikali haioni kuna umuhimu wa kupunguza kodi au kuondoa kodi kabisa katika suala zima la pedi ili hawa watoto wa kike waweze kupata pedi na hata ikibidi Serikali ilibebe hili kuhakikisha kwamba, wanagawa pedi kwa watoto wa kike. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika huduma za afya tunajua kabisa na tumesikia mengi tu na tumeona maeneo mengi hata ya Vijijini vituo vingine vya afya akinamama wanajifungulia kwenye nyumba za nyasi (full suit). Je, bajeti hii imeangalia vipi mchanganuo wake kuweka vipaumbele katika kujenga vituo vya afya na zahanati ambazo wanawake wamaeneo yote ya vijijini watajifungua salama na kuondoa tatizo la vifo kwa mama na mtoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti hii tunasema kwamba, kama wanawake haya ndiyo masuala muhimu ya kuzingatiwa na tunafahamu kabisa katika Wizara hii tunaye mwanamke na huyu mwanamke tunatarajia kabisa kwamba yeye ndiye atakuwa jicho la wanawake wote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabila la Warangi wana msemo unasema kwamba, mwana wa mukiva amanyire michungiro, kwa maana kwamba mtoto wa maskini hata awe na shida vipi anajua jinsi gani ya kuhimili ile shida. Kwa maana kwamba kama ni khanga imechanika huku nyuma ataishona mbele ataiunga atajifunga na maisha yatakwenda mbele. Kwa maana hiyo, natumia msemo huu kwa kusema kwamba, Naibu Waziri katika Wizara hii yeye ndiyo jicho la kuangalia Wanawake wa Tanzania kwa sababu amebeba dhamana yao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekitiki, katika suala la watu wenye ulemavu. Tumetaja tu ujumla ajira, elimu, afya lakini, je, tumejiandaa vipi kuhakikisha kwamba bajeti kadhaa itakwenda katika kununua vifaa saidizi kwa watu wenye ulemavu? Bajeti kadhaa itakwenda katika kuhakikisha kwamba miundombinu inakuwa rafiki ili watoto wote waweze kupata elimu na hasa watoto wa vijijini ambao miundombinu siyo rafiki. Je, Bajeti hii tumejipanga vipi kuhakikisha kwamba tunaorodhesha idadi kamili ambayo itatimiza mahitaji ya watoto wenye ulemavu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika suala la ajira. Sheria na Wizara pia na yenyewe kama Wizara ya Fedha bado ina jukumu hilo. Je, tunawekaje mipango yetu katika kuhakikisha kwamba watu wenye ulemavu na wenye sifa wanapata ajira, vilevile mitaji kwa ajili ya kuwawezesha ili waweze kujiajiri. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, kama baba, lakini kama Waziri mwenye dhamana katika Wizara hii kuhakikisha kwamba haya mambo katika hii bajeti ijayo ili kusiwepo na maswali haya tuone kwamba tumejipanga vipi ili katika kila kipengele kimoja kijitosheleze katika kusaidia mahitaji hayo ya makundi haya niliyoyataja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kusema; siku zote katika maisha unapokuwa mwongo basi ni vema pia ukawa na kumbukumbu. Tumesikia michango mingi sana ya Waheshimiwa Wabunge, lakini naomba nikumbushe tu mambo yaliyojiri kwa kasi sana mwaka jana, tuliambiwa kwamba: “Nawashangaa sana wanaochoma moto vibaka kwa kumuacha Lowassa akitanua mitaani.”
Mwingine akasema kwamba; “CCM wamempatia Fisadi fomu ya kugombea Urais ni hatari sana.” Swali langu, je, kati ya CCM na wao ni nani hatari katika hili? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine wanasema kwamba “nina ushahidi wa kutosha kuhusiana na wizi na ufisadi wa Lowassa na Rostam Aziz.” Leo hii ni nani ambao walimbeba na kumtangaza nchi nzima kumsafisha na wakati huo huko nyuma walisema kwamba ni fisadi? Ndiyo maana nikasema kwamba ukiwa mwongo uwe pia na kumbukumbu ya yale maneno unayosema. Ahsante.