Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuongea na .kutoa mapendekezo kuhusu mpango huu ambao ameuleta Mheshimiwa Dkt. Mpango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kwenda hapo, naomba niwakumbushe Wabunge kwamba jukumu letu humu ndani kama wengi wanavyosema ni kuishauri na kuisimamia Serikali. Siyo jukumu letu kuonyesha Serikali haifai na kupinga pale ambapo hata haistahili kupingwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namna ya kushauri na kusimamia Serikali kati ya vyama vya upinzani na chama tawala lazima ni tofauti. Nasema hivyo kwa nini?
Nimewasikiliza hamkusikia mama Nagu akisema naomba na wengine wanapoongea msikilize. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mama ukiwa na watoto nyumbani wengine wa kwako na mwingine wa kambo, yule wa kwako anapoangusha glass unasema bahati mbaya, wa kambo anapoangusha glass unasema makusudi, huo ndiyo ukweli wenyewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utamaduni wa vyama vingi unless mnakataa jukumu la vyama vyenu, utamaduni wa vyama vingi ni upinzani kuonyesha Serikali…
MWENYEKITI: Mheshimiwa Nagu hebu kaa kwanza...
MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mama yao hata wakinitukana nitaosha mkono sitaukata. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema kwamba jukumu la wapinzani ni kupinga Serikali iliyo madarakani hilo linajulikana, lakini basi pingeni kwa lugha ya staha. Sisi ambao ni chama wa tawala kazi yetu ni kuisimamia, kuishauri kwa lugha ya staha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naenda kwenye Mpango wa Maendeleo, huu ni mpango wa miaka mitano wa pili ili kufikia dira ya Taifa letu. Dira ya Taifa letu inatutaka mwaka 2025 tuwe ni Taifa ambalo lina uchumi wa kati na tunatumia mipango hii na utekelezaji wake kutusogeza pale. Kwa hivyo, tulifanya tathmini ya miaka mitano ya kwanza tuliyoitekeleza na tukaona kwamba tumepiga hatua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii ilikaa bila mipango kwa miaka mingi. Mimi nakumbuka kabla ya mipango hii uchumi wa nchi hii ulikuwa ni hasi mbili leo tuko asilimia sita na zaidi maana yake uchumi umepanda kwa asilimia nane. Kwa hiyo, miaka mitano ya mpango huu, mwaka wa kwanza ulitufanya tukapiga hatua na huu ninaamini utatufanya tupige hatua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie kwamba hakuna kazi nzuri ambayo haifanywi kwa bidii. Sisi akina mama na nitatumia mfano ambao unanihusu mimi, tunabeba mimba miezi tisa tunatapika tunaenda labor ward tukitegemea kufa na kupona. Katika mpango huu vilevile tufikirie hivyo kwamba baada ya kutekeleza tutapiga hatua. (Makofi)
Sasa nataka niseme tulivyotathmini mpango wa kwanza wa miaka hii mitano ya mpango tumepiga hatua uchumi unapanda. Hata hivyo, tunajua maeneo yanayopandisha uchumi siyo yale ambayo yanahusika na watu directly. Kwa hivyo, sasa tuangalie yale ambayo yanahusika na watu directly. Tunakubaliana kwamba azma yetu ya miaka hii mitano ni kujenga uchumi wa viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimkumbushe Mheshimiwa Dkt. Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango kwamba hatutakuwa na viwanda bila kuwa na kilimo kinachotegemewa. Huo ndiyo ukweli wenyewe kwenye maelezo yake ya hakuongea hata kidogo juu ya kilimo. Kwanza kuongea juu ya kilimo ni kuwapa moyo Watanzania asilimia 80 wanaotegemea kilimo. Kilimo ndiyo kitatoa chakula kwa wale watakaofanya kazi viwandani, kilimo ndiyo kitakachotoa malighafi ya viwanda, tija ya kilimo ndiyo itafanya watu waondoke kwenye kilimo waende kwenye viwanda. Kwa hiyo, naomba katika mpango huu na tunapotekeleza mpango huu kupitia bajeti tuone kwamba kilimo kinapewa kipaumbele ili tufikie viwanda tunavyovitaka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tumeamua uchumi wa viwanda lazima tuangalie ni viwanda gani ambavyo vitatusaidia. Kiwanda cha kwanza narudia tena kama walivyosema Wabunge kiwanda cha chuma ni kiwanda mama, kiwanda cha kemia ni kiwanda mama. Viwanda vile mama lazima tuvipe kipaumbele ili vituwezeshe twende kwenye viwanda vingine na tuwe na sustainable industrial development. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo ndugu yangu Mheshimiwa Mpango hakikisha utekelezaji wa kiwanda cha chuma cha Liganga na mkaa wa Mchuchuma umepewa kipaumbele. Vilevile katika kuchochea kilimo hakikisha viwanda vya mbolea vinapewa kipaumbele. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tujue kwamba siyo bajeti ya Serikali tu ndiyo itakayotekeleza mpango wetu. Kwanza naomba katika kukusanya kodi huwezi ukamkamua ng‟ombe bila ya kumlisha, lazima tutambue sekta binafsi inataka kulishwa, muone ni namna gani tutaipa nguvu na iweze kutoa kodi ya kuaminika. Kuna wale wanaokimbia kodi wale ni wachache lakini kwa ujumla sekta binafsi lazima tuiimarishe. Sekta binafsi itatusaidia kutekeleza mpango huu kupitia kilimo, kupitia viwanda na vingine vyote tulivyovipanga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namna rahisi ni utekelezaji wa sera na Sheria ya PPP, ubia kati ya sekta ya umma na sekta binafsi. Naomba sana tusipuuze hili kwa sababu huu ni uchumi wa soko tumeshakubali na uchumi wa soko unategemea sekta binafsi. Nasema kwamba pengine kuna mahali ambapo tumeenda kando, naomba tuache kule tulikoenda kando mimi napendekeza kwamba tukae na sekta binafsi ijue kwamba kodi yao ndiyo itawatengenezea mazingira mazuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu sekta binafsi naomba tuwe na One Stop Center effective ile ambayo ipo ni ya maneno tu. Naomba mfanyabiashara anapotaka kuandikisha biashara yake aweze kutoka na leseni na ajue aende kukopa au equity itatoka wapi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka kulisema ndugu zangu mliongea juu ya Logistic Center ya Kurasini. Logistic Center ya Kurasini tulikuwa tumepanga kwa ajili ya ku-feed Kariakoo siyo kuua Kariakoo. Bidhaa zinazouzwa Kariakoo zinatoka China, Thailand na Indonesia, Kurasini ndiyo italeta bidhaa hizo in bulk na wale wa Kariakoo watachukulia pale, hiyo ni namba moja. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ya pili Logistic Center itaonyesha viwanda gani ambavyo vitakuwa na faida Tanzania kwa sababu pale ndipo demand itajulikana kama ni nguo watu wanataka tukijenga kiwanda cha nguo tutapata faida, kama ni viatu tukijenga kiwanda cha viatu tutapata faida. Kwa hiyo, Logistic Center hiyo tumeshaanza kuitekeleza naomba iharakishwe kusudi tunapojenga viwanda vyetu tujue ni viwanda vipi ambavyo vinatakiwa na tusikisie viwanda vinavyotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ambalo nataka kulisema ndugu zangu ni kwamba hii ni Serikali ya Chama cha Mapinduzi lakini uongozi mpya. Uongozi mpya unapokuja kwa vyovyote watu hawatakuwa na uhakika; na mfanyabiashara anataka awe na uhakika; kabla hajawa na uhakika yanayotokea ndiyo yanatokea. Pale ambapo tutawahakikishia uchumi wao wafanyabiashara watarudi na mimi nina hakika nchi hii baada ya hapo itakuwa steady hatuna sababu ya kuogopa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninarudia tena uchumi huu ambao tunaujenga lazima uwe na uhusiano wa watu na ndiyo maana kama Mheshimiwa Mpango atakumbuka nilimwambia tuandike maendeleo ya watu ili isiwe maendeleo ya vitu tu. Tunavyopiga hatua tunataka maisha ya watu yawe bora zaidi, tunataka uchumi wa nchi uwe bora lakini ubora wake utokane na watu kusema kwamba tuna nyumba bora, tuna dawa za kutosha, tuna nguo za kutosha hii ndiyo itakayofanya mpango huu uwe mpango wa maendeleo ya watu na si maendeleo ya vitu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo ili wengi wapate nafasi na ninaombeni pingeni, tusimamie na tushauri lakini wote wawili tutumie lugha iliyo na staha na tutajenga heshima ya Bunge hili kwa upande wa upinzani na upande wa chama tawala mimi sina wasiwasi, ahsante sana.