Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Sixtus Raphael Mapunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. SIXTUS R. MAPUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa na mimi nafasi ya kuchangia kwenye mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote niwapongeze kwa mpango mzuri waliotengeneza. Ukiusoma mwanzo mpaka mwisho hupati shaka kwa yanayoenda kutekelezwa na hasa walipogundua kuingia na mfumo wa program wa kibajeti ambao mimi naamini wakijielekeza kwenye program itawasaidia huu Mpango ukatekelezeka vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na uzuri wa Mpango huu, nimeusoma kurasa zote lakini huu Mpango una changamoto moja, umekosa kitu kinachoitwa rejea. Tukipata nafasi ya kurejea mafanikio ya Mpango uliopita, unatupa nafasi nzuri ya kushauri Mpango huu tuutekeleze vipi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Walatini wana msemo repetitio est mater studiorum wakimaanisha marejeo ni mama wa mafunzo. Tutakwenda na mpango huu, tusipopata fursa ya kurejea mwaka mmoja uliopita kwamba tulipanga nini, tumefanikiwa nini, tufanyeje ili tusirudi nyuma, hatutafika. Hilo ndilo jambo linalotia shaka mpango huo mzuri. Tusipopata marejeo ya mafanikio ili twende vizuri zaidi; ya upungufu ili turekebishe, hatutakwenda vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango aje angalau na summary ya tulikotoka, tulipo na tunakokwenda ili tuutendee haki huu mpango ili tufanye vizuri ndani ya mwaka ujao na baada ya miaka mitano tuseme Tanzania tuliikuta hapa, tumeitoa mwaka 2015, tunaiacha hapa 2020 kwa mpango unaoeleweka na unatabirika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1981 Chama cha Mapinduzi kilitoa mwongozo. Kwenye ule mwongozo kuna maneno mimi napenda sana kuyatumia na huwa napenda sana yawe sehemu ya maisha ya viongozi wenye utu. Yale maneno yanasema hivi, “kujikosoa, kukosolewa na kujisahihisha siyo dalili ya kushindwa bali ni njia sahihi ya kujipanga na kufanikiwa vizuri zaidi.” Tukiona pale tulipokosea aidha kwa kuambiwa au kwa sisi wenyewe kuona maana yake tumejikosoa, siyo kwamba tumeshindwa, inatupa njia nzuri ya kutoka hapa tulipo, twende mbele zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivi? Nasema hivi kwa sababu huu mpango umekuja na programs ambazo tunaamini tumezipa vipaumbele. Kuna miradi ya vielelezo. Unaposema miradi ya vielelezo tafsiri yake ni kwamba kwenye haya mambo baada ya mwaka mmoja tutasema hiki ndicho kielelezo kinachotuonesha kwamba tumefanya vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mmeelezea vizuri sana kuhusu viwanda, lakini nikiangalia sioni sehemu ambapo kuna mikakati itakayokuja kukabiliana na changamoto za viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifuatilia sana nchi zilizokuwa na viwanda, aidha zile za zamani za Ulaya zilizoanza na coal and steel industries, Wajerumani na Waingereza; au zile za Mashariki ya Mbali zilizoanza na textile industries baadaye zikaendelea, hawa wote walikuwa na misingi minne ambayo namwomba Mheshimiwa Waziri Mpango aiangalie vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa kwanza wa viwanda ni power (energy) na gharama za energy; msingi wa pili wa ni qualified personnel (manpower); watu wenye uwezo wa kuviendesha hivyo viwanda; msingi wa tatu ni malighafi (raw materials). Utavilishaje hivyo viwanda? Msingi wa nne siyo katika maana ya udogo wake, is financing. Una uwezo gani wa kuviendesha, kuvi-finance, kuvigharamia hivyo viwanda aidha kwa mapato yako ya ndani au kwa kushirikiana na watu wengine wenye mitaji kuja kwenye mifumo ya kuwekeza kwa kushirikiana? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiyaangalia haya yote, yananipa sababu za kutosha kumwomba Mheshimiwa Waziri ayaangalie maeneo mawili kwenye mkakati wake. Eneo la kwanza kubwa ni mradi wa makaa ya mawe wa Mchuchuma na mradi wa chuma wa Liganga. Kwa nini nilianza na kusema repetition est mater studiorum? Huu Mpango ulikuwa mwaka 2007, ndiyo kwa mara ya kwanza tunataka sasa Mchuchuma na Liganga ije iwekeze kutuletea chuma, ije ituwekee umeme wa kutosha na iongeze umeme mwingine kwenye gridi ya Taifa, it was 2007. Leo tunapoongea, we are approaching ten years.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo nasema marudio ndiyo mama wa mafunzo. Tusiporudia kutaka kujua tulipotoka, tutadhani tunakuja na kitu kipya kumbe kitu kipya kilipata changamoto nyingi sana na hizo changamoto hatukupata fursa ya kuzirekebisha. Kwenye huu mpango, Mchuchuma, mmesema itazalisha Megawatt 600. Kati ya Megawatt 600, Megawatt 250 ndiyo zitazalisha umeme kwa ajili ya chuma kile cha Liganga na 350 ndizo sasa watauziwa TANESCO kuingia kwenye grid ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna taarifa za wazi zinasema haya mambo yote yako sawasawa isipokuwa kuna mvutano mmoja kwenye power purchase agreement ambapo mbia anataka tununue umeme kwa 13% sisi tunataka tununue umeme kwa 7%; lakini tukumbuke agenda ya umeme ni ya mradi mmoja tu na agenda ya chuma ile siyo hoja pale ya sisi kujadiliana tumeuziana umeme kiasi gani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashindwa kuendelea na mradi wa chuma cha Mchuchuma kwa sababu tu ya bei ya umeme. Kwa nini kwenye zile Megawatt 250 ambazo ndiyo za mbia, azalishe 250, atuletee chuma sisi tuzalishe chuma, tuachane na 350 ambao tutaununua kwa sh. 7/= au sh.13/=. It is wastage of time! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri Mpango, kwa dhati ya moyo wangu, hebu a-focus kwenye hili kwa sababu nalo lina maneno ya hujuma; hujuma zina sura mbili. Wanasema, bwana, kusikiliza maneno ya mtaani siyo jambo zuri, lakini yakisemwa kwa muda mrefu yanawafanya watu waamini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasema huu mradi unahujumiwa; kwanza unahujumiwa na mashirika makubwa na makampuni makubwa ya upande mwingine kwa sababu mradi kapewa Mchina, wanataka usuesue usifike kwa wakati, lakini wa pili wanasema, eh, kwa sababu Kusini siku zote ni Kusini, basi Kusini iwe ya mwisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa haya mambo hayatujengi sisi kama Wabunge, haya mambo yanatufarakanisha, yanatufanya sisi watu wa Kusini tuendelee kuwa maskini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikwambie Kusini siyo Kusini kama mnavyofikiri, kama Kusini ingekuwa inamaanisha chini, Mto Nile usingetoka Ziwa Victoria kwenda Kaskazini. Nataka kukwambia Kusini ni juu na Kaskazini ni chini kwa lugha kama hiyo. Niombe kabisa, tusifike sehemu tukawafanya watu wa Kusini ionekane kwamba wanahujumiwa katika hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tujipe muda wa kutosha kwenye hoja nzima ya Mchuchuma na Liganga. Kwa nini nasema hivi? Kanuni ni mbili tu; tukifanikiwa kwenye Mchuchuma katika maana ya kuleta chuma na chuma kile hakitafika peke yake, kitakuwa na madini mawili, tutapata vanadium na titanium. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, huku chuma sasa ndipo tutakapoongelea mataruma yale ya kwenda reli ya kati yapatikane pale; mtakapotaka sasa madaraja yenu, vitu vitoke pale. Ndiyo zile kanuni nne nilizozisema; angalia sehemu zote, angalia eneo la power; power tunayo. Sasa unafanyaje kukifanya kiwanda cha textile industry kiende vizuri? Power yetu ni ghali, tuangalie.
Mheshimiwa Mwenyekiti, utatengeneza kiwanda cha nguo, tuna soko kubwa la nguo, tutashindwa ku-compete kitakufa. Kwa sababu nguo ya Thailand, China na Uturuki itauzwa bei ya chini kwa sababu ya cost of production, haya mambo yote Mheshimiwa Mpango yaweke katika mizani yake, tutatue hili tatizo Watanzania tutoke hapa tulipo twende mbele zaidi. Watanzania wanataka viwanda, nami nataka viwanda, nawe unataka viwanda; lakini viwanda lazima tuvipange vizuri kwa kuangalia kila element, tusiache untouched stone, kila jiwe likanyagwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.