Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya na wewe kwa kunipatia nafasi hii ili nami niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naunga mkono hoja. Serikali yetu ya Awamu ya Tano imekuja na mipango kabambe kwa ajili ya kufufua uchumi wa nchi hii na kwa maana hiyo, sisi kama Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao ndiyo tunahusika kwa namna zote kuisimamia Serikali kuhakikisha kwamba inafanikiwa katika mipango yake ya kila siku, basi tuwe mstari wa mbele kuhakikisha kwamba tunaiunga mkono Serikali yetu hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utaanza na suala zima la uhamishaji Makao Makuu kutoka Dar es Salaam kuja hapa Dodoma. Ni wazo zuri na ni la kimaendeleo lakini limechelewa. Pamoja na kuchelewa huko, tunatakiwa tujipange sawasawa kuhakikisha kwamba hatushindwi njiani. Kwa maana hiyo, mipangilio iwe thabiti tusije tukajikuta kwamba sasa tunakwamisha Serikali katika utendaji kazi wake kwa sababu sasa watumishi watakuwa mguu mmoja nje, mguu mmoja ndani. Kwa hiyo, nishauri Serikali kwa kweli ijipange vizuri na Maafisa Masuuli kama Waziri wa Fedha alivyoainisha kwenye mpango wake kwamba jambo hili waliweke katika bajeti ili liweze kutekelezeka kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo pia niishauri Serikali kuhakikisha kwamba inaweka katika mipango yake ya bajeti gharama za ujenzi wa Halmashauri katika Wilaya mpya kama Mbogwe na nyingine. Pia itenge bajeti kwa ajili ya ujenzi wa Makao Makuu ya Mikoa mipya ambayo imeanzishwa kama Mikoa ya Geita, Songwe, Simiyu, Njombe na Katavi ili wananchi wa mikoa hii na wao waweze kupata huduma karibu zaidi kama Serikali ilivyojipanga kwa ajili hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala zima la utaratibu wa Serikali kufuta retention na kuziagiza taasisi mbalimbali kupeleka pesa zao katika akaunti ya Benki Kuu. Jambo hili ni zuri kwa sababu linaongeza udhibiti wa mapato na matumizi ya Serikali ili kuweza kufahamu thamani halisi ya yale mapato ambayo yanapatikana. Hata hivyo, niishauri Serikali iwe makini kuhakikisha kwamba pesa ambazo zimepangwa kwa ajili ya taasisi hizi zinaenda kwa wakati ili miradi ya maendeleo ambayo imepangwa kwenye sekta hizo isikwame. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala zima la miradi ya kielelezo. Miradi hii mingi imeainishwa lakini mradi mkubwa ambao unatakiwa tuufanye haraka ni mradi wa reli ya kati na ujenzi wa Bandari za Tanga, Dar es Salaam, Mtwara na pia bandari zile za maziwa makuu kama Mwanza, Bukoba, Karema, Kigoma na nyingine nyingi. Nasema hivi kwa sababu tumepakana na nchi mbalimbali ambazo nyingi zinategemea sana Bandari ya Dar es Salaam ambayo inaunganishwa na maziwa makuu kwa kupitia njia ya reli. Sasa reli ya kati kutoka Dar es Salaam – Tabora – Kigoma - Mwanza na nyingine ambayo itaanzia Isaka - Kigali, zote hizi zina muunganiko mzuri wa kuweza kutumiwa na nchi jirani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, naiomba Serikali ihakikishe inafanya kila liwezekanalo kuhakikisha kwamba mradi huu kwa kushirikiana na wabia wa maendeleo ambao ni nchi ya China ambayo imekubali kufadhili mradi huu, ufanyike kwa umakini na kwa haraka ili kuweza kuhakikisha kwamba Tanzania ya viwanda inafikiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala zima la shilingi milioni 50 kwa kila kijiji. Nikiwa mwanakamati wa Kamati ya Bajeti, tumeona kwamba ili Serikali iweze kufanikiwa katika lengo hili ni vema basi ikaongeza chagizo lake katika bajeti kutoka shilingi milioni 59 kwa mwaka mpaka kufikia shilingi bilioni 200 ili kwa miaka yake minne iliyosalia lengo la kukipatia kila kijiji shilingi milioni 50 liweze kufikiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala zima la kubadilika kwetu kwa mindset kwa maana ya Watanzania. Imeonekana kwamba wakati mwingine Watanzania tunakuwa na matatizo ya kutengenezwa kwa kuwa na urasimu mkubwa ambapo wawekezaji wanapokuja hapa nchini hucheleweshwa, matokeo yake wanaamua kukimbilia katika nchi nyingine ambazo na zenyewe zina uhitaji wa wawekezaji kama sisi. Kama tusipobadilika tunaweza tukajikuta tunaachwa na wenzetu nchi zenye ushindani na sisi, wakapokea wawekezaji wa kutosha na matokeo yake nchi zao zitaneemeka kiuchumi kuliko sisi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, itoshe tu kusema haya, ahsante kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.