Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Joseph George Kakunda

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Sikonge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nampongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. Mpango kwa uwasilishaji wa Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo. Nampongeza kwa kutuletea vipaumbele vilevile kama vilivyokuwa mwaka 2016/2017 kujenga msingi wa uchumi wa viwanda, kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara na usimamizi wa utekelezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni commitment ya kuendelea kutekeleza Mpango wa Pili wa Maendeleo ya nchi na hii inaonesha kielelezo cha uendelevu wa mIpango yetu, kielelezo cha sera zinazotabirika na kielelezo cha mipango imara. Kwa hiyo, namshukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefurahi alipoonyesha katika kitabu hiki cha mapendekezo mkakati wa ufuatiliaji na tathmini chini ya uratibu wa Tume ya Mipango ambao umewekwa vizuri sana. Napongeza lakini natoa rai kwamba yale mazuri ambayo yalikuwa yanatekelezwa na ule Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa, yaingizwe katika huu Mpango wa Ufuatiliaji na Tathmini ili kuboresha zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti nimeshituka kidogo niliposoma tathmini ndogo iliyoko kwenye kitabu cha mapendekezo hasa kuhusu hali ya viwanda ya sasa (status). Tuna viwanda vikubwa 1,322, tuna viwanda vidogo 47,921, takwimu ni nzuri. Hata hivyo tatizo nimeliona kwenye viwanda vikubwa vya uzalishaji yaani manufacturing industries viko 998; lakini kati ya hivyo 998 asilimia 53 ya viwanda hivyo viko katika mikoa mitatu tu ya Dar es Salaam, Arusha na Kagera. Sasa hii mimi nimeona kwamba kwa kweli uwiano wa uwekezaji katika viwanda vya uzalishaji nchini hauko vizuri. Naomba huko tuendako ili kusudi hii status iweze kubadilika, huko tuendako tuzingatie uwiano wa maendeleo ya nchi yetu kwa kuzingatia kwamba viwanda vya uzalishaji vinahitajika hata katika mikoa ambayo sasa hivi haina hivyo viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nije sasa kwenye miradi ya kipaumbele. Nimeisoma, ni mizuri na ninatoa maoni kidogo katika miradi ya kipaumbele kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, reli ya kati kwa kiwango cha Kimataifa au standard gauge ni mradi muhimu sana. Juhudi ambazo zimeshaanza za kutafuta fedha kwa ajili ya mradi huu naomba zisilegezwe; zifuatiliwe kwa ukamilifu wake ili kusudi hii reli ijengwe kama ambavyo inaonekana katika mapendekezo. Umuhimu wake unaonekana kutokana na matokeo ya kiuchumi yatakayopatikana. Kwanza, ujenzi wa reli ya kati utashusha gharama za usafiri na usafirishaji ambazo ndizo kiini kikubwa cha kupanda gharama za maisha. Mfano, gharama za kusafirisha mbolea, gharama za kusafirisha mafuta ya petrol na diesel zitapungua kwa kiasi kikubwa na hivyo kupunguza bei ya petrol, bei ya diesel na bei ya pembejeo na hiyo itasababisha maisha yawe nafuu kwa wananchi. Kwa hiyo, mradi huo ni muhimu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunahitaji barabara za lami, viwanja vya ndege, tunahitaji kuboresha barabara za changarawe na hili niliwekee msisitizo kwenya maeneo yangu ya Jimbo. Barabara ya Tabora – Ipole – Mpanda ambayo sasa hivi inajengwa, mkazo uwekwe, barabara ile ikamilike kwa ajili ya kunganisha Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Katavi. Barabara ya Ipole - Rungwa inaunganisha Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Mbeya. Naomba katika kipindi hiki cha mwaka 2017/2018 ianze kujengwa; na barabara ya kutoka Chunya – Itigi – Mkiwa, kipindi cha mwaka 2017/2018 barabara hii nayo ikamilike kwa sababu hapo kuna uchumi mkubwa sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria ni muhimu sana. Imetajwa miradi ya maji kwa ujumla jumla, sasa mimi nakwenda kwenye specific ili Mawaziri husika wa sekta husika wazingatie wakati watakapokuwa wanaweka maoteo ya bajeti rasmi kwa ajili ya kuingia kwenye rasimu ya mpango wenyewe, naomba sana mradi wa maji kutoka Ziwa Victoria ufike Sikonge.
Mheshimiwa Mwenyekiti, status ya sasa hivi wametangaza kandarasi tatu. Kuna lot inatoka Solwa mpaka Nzega; kuna lot inatoka Nzega mpaka Igunga; na kuna lot inatoka Nzega mpaka Tabora Mjini. Ile lot ya kutoka Tabora Mjini mpaka Sikonge haijatangazwa. Naomba wakati wa bajeti utakapofika, Waziri wa Maji asimamie hilo ili lot ya kutoka Tabora Mjini mpaka Sikonge ionekane kwenye bajeti ya mwaka 2017/2018; vinginevyo kwa kweli tutakuwa hatuwatendei haki wananchi wa Sikonge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona mapendekezo ya jumla kuhusu afya; lakini nilitegemea kuona mkakati wa kujenga zahanati kila kijiji na kituo cha afya kila kata, unakuwa wazi katika huu mpango. Nimesoma maelezo, yako jumla jumla sana, naomba tuwe specific; zahanati kila kijiji na kituo cha afya kila kata ni sera ya Serikali na ni sera ya nchi yetu. Kwa hiyo, naomba sana iwe specific.
Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni kuhusu mpango kwenye sekta ya kilimo. Sisi Sikonge hatuwezi kuzungumzia kilimo bila kuzungumzia tumbaku. Status ya sasa hivi kwa mwaka 2016/2017; hawa ndugu zetu makampuni yanayonunua tumbaku, yameshusha makisio kwa zaidi ya asilimia 50, maana yake nini? Maana yake ni kwamba kijiji ambacho kilikuwa na wakulima 300 wa Tumbaku mwaka huu hawataweza kulima wote 300, watalima labda wakulima 100. Ina maana wengine hata wakilima hawana pa kuuza.
Naomba sana Serikali kwanza kwa mwaka huu iwe macho kuhusu haya makampuni ili yafanyike marekebisho ya makusudi, lakini kwenye mpango wa 2017/2018 matatizo kama yaliyotokea mwaka huu naomba yasijitokeze kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mwongozo wa Uandaaji wa Bajeti ya mwaka 2017/2018, naunga mkono na ninaipongeza Serikali kwa kuendelea na vigezo vya asilimia 40 kwamba itumike kwa ajili ya miradi ya maendeleo na asilimia 60 kwa ajili ya matumizi ya kawaida. Kwa kweli huo ndiyo msingi ambao utaendeleza pale ambapo tumeanza mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono vigezo hivyo vikuu vya ugawaji wa rasilimali kwa sababu nchi yetu itaendelea kuweka uzito unaostahili kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vigezo vikuu vya OC, napendekeza viwe ni pamoja na idadi ya miradi ya maendeleo inayosimamiwa na taasisi husika ili miradi hiyo utekelezaji wake usimamiwe vizuri na ulingane na thamani ya fedha itakayotumika. Kama idadi ya miradi ya maendeleo haitakuwa miongoni vya vigezo vya kugawa OC, basi tutakuwa tunatekeleza miradi ambayo haisimamiwi vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile upo umuhimu wa kupitia upya vigezo vya kisekta ili kulingana na wakati uliopo ziandaliwe; maana yake hivi vigezo ambavyo viko kwenye hivi vitabu viliandaliwa kipindi kirefu sana, mwaka 2005/2006.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana vigezo hivyo vifanyiwe mapitio ili vilingane na wakati wa sasa. Mfano, ruzuku katika sekta ya maji kwa sasa inahitaji kigezo cha idadi ya watu tu wanaokaa vijijini, lakini kwa sasa hivi kuna wakazi wengi katika Miji Mikuu ya Wilaya na Miji Midogo ambayo ndiyo imejitokeza hivi karibuni. Mimi naomba vigezo hivi vifanyiwe mapitio ili kusudi vilingane na mahitaji ya wakati wa sasa maana yake ni vya muda mrafu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu yalikuwa ni machache tu, ni hayo, nawapongeza sana Serikali, ahsante sana na naunga mkono hoja.