Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kukupongeza wewe mwenyewe kwa kazi nzuri unayoifanya, tuko pamoja na wewe, uendelee kukaa hapo mpaka tarehe Mosi Julai. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nimpongeze Waziri wa Fedha, Naibu Waziri wa Fedha na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya. Niipongeze sana TRA kwa kufanya kazi nzuri ya kukusanya mapato. Sasa hivi mapato yetu ni mazuri, ninachoomba tu ni kwamba hiki kinachokusanywa basi kifike kwa walengwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kuna miradi mingi ambayo haijakamilika vijijini, kwa sababu fedha za miradi hazifiki au zinafika kidogo, lakini Bunge kazi yetu ni kupitisha bajeti na tukishapitisha bajeti lazima fedha zifike kwenye miradi ya maendeleo, kama hazitafika kule miradi haitakamilika.
Kwa hiyo, ninachoomba baada ya makusanyo haya basi fedha ziende kwenye miradi ya maendeleo. Kwa mfano, katika Jimbo langu la Mpwapwa nina zahanati kwa mfano zahanati ya Mgoma haijakamilika, zahanati ya Igojimbili haijakamilika, Igojimoja haijakamilika pamoja na vituo vya afya vya Mboli na Mima sasa ni miaka kumi havijakamilika, kwa sababu fedha hazijatengwa kwa ajili ya kukamilisha vituo hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine huduma za afya. Sasa hivi kuna tatizo kubwa sana la dawa katika zahanati, vituo vya afya, Hospitali za Wilaya, Mikoa na Rufaa, ni kwa sababu wanaosambaza dawa ni MSD, lakini hatuwezi kuwalaumu MSD kwa sababu hawana fedha. Fedha wanazotengewa ni kidogo sana, halafu hata zile fedha kidogo hazipelekwi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kuna deni la MSD shilingi bilioni 71, nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha, deni hili lazima lilipwe. Mheshimiwa Waziri wa Afya alitueleza Bungeni kwamba ametenga shilingi bilioni 251 kwa ajili ya kupeleka MSD kwa ajili ya kununua dawa, basi naomba hizo fedha zipelekwe MSD; kwa sababu MSD bila kupeleka dawa katika zahanati itakuwa ni kazi ngumu sana, wananchi wanalalamika hakuna dawa. Wananchi wanakwenda kwenye zahanati, vituo vya afya, hospitali, wanaandikiwa vyeti wanaambiwa wakanunue dawa kwenye maduka binafsi. Kwa kweli hii haipendezi hasa kwa Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nizungumzie kuhusu ukusanyaji wa mapato katika Halmashauri zetu za Wilaya na Manispaa. Mapato ndiyo uhai wa Halmashauri kwa hiyo, Halmashauri isipokusanya mapato hasa ya ndani kwa kweli, lazima Halmashauri zitayumba. Halmashauri lazima zijitegemee kwa mapato ya ndani, ninapozungumza hakuna Halmashauri ambayo inakusanya mapato zaidi ya asilimia kumi kwa kujitegemea, zote zinakusanya chini ya asilimia kumi, kwa hiyo, wanategemea ruzuku ya Serikali Kuu. Na mimi najiuliza hivi siku Serikali Kuu ikisema haitoi ruzuku, Halmashauri zitabaki? Hazitabaki! Kwa hiyo, wajitahidi kukusanya mapato, ni suala la TRA kukusanya mapato na hasa kodi ya majengo (property tax), mimi siliungi mkono kwa sababu hiki kilikuwa ni chanzo kimojawapo cha mapato ya Halmashauri ya Wilaya. Vyanzo vingi vya Halmashauri za Wilaya vimechukuliwa na Serikali Kuu, kulikuwa na hotel levy, kulikuwa na mambo haya ya mafuta, walikuwa wanakusanya Halmashauri za Wilaya, lakini baadaye Serikali Kuu ilichukua hivi vyanzo. Kwa hiyo, naomba hata kama TRA ikikusanya, lakini fedha zote zikabidhiwe Halmashauri. Siyo tena waanze kudai kama deni, hapana. Kama watakusanya TRA basi fedha hizo zipelekwe kwenye Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wenyeviti wetu wa Vijiji wanafanya kazi nzuri sana, lakini hawalipwi hata senti tano. Kwa hiyo, naomba katika bajeti yako Mheshimiwa Waziri wa Fedha wafikirie angalau kidogo kwa sababu hawa ndiyo wanaofanya kazi za Serikali za Mitaa na kazi za Serikali Kuu katika vijiji kwa hiyo, wafikiriwe angalau kulipwa posho kidogo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kuhusu umeme; naipongeza Serikali kwa kusambaza umeme katika vijiji na mimi vijiji vyangu vya Jimbo la Mpwapwa na Wilaya ya Kongwa tumepata umeme, lakini kuna baadhi ya vijiji bado! Kwa mfano Kijiji cha Sazima nguzo zinapita karibu na kijiji, lakini hakuna umeme; Igoji Kaskazini hakuna umeme nguzo zinapita pale; Iwondo hakuna umeme; Mkanana hakuna umeme mpaka sehemu za Mlembule Tambi kule tayari nguzo zimeshapelekwa. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri Serikali ijitahidi kusambaza huu umeme; umeme ni maendeleo, umeme ndiyo uchumi wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi. Naunga mkono kwa asilimia 100.