Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na mimi napenda niungane na wenzangu kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuichangia hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango kuhusu Hali ya Uchumi na Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2016/2017 pamoja na Makadirio na Mapato ya Matumizi kwa mwaka 2016/2017.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nianze kwa kumpongeza, kwa kuona umuhimu wa barabara yetu ambayo sisi wenyewe tunaiita ni barabara ya uchumi ya kutoka Mtwara kwenda Newala hadi Masasi, Mbinga hadi Mbamba Bay kuwa miongoni mwa miradi ya kipaumbele katika mwaka huu wa fedha. Mheshimiwa Waziri kwa hilo nakushukuru sana kwa sababu wananchi wa Mkoa wa Mtwara hasa barabara kutoka Mtwara - Nanyamba - Tandahimba, Newala - Masasi imekuwa ni kilio cha muda mrefu, hii ni barabara yetu ya uchumi inasafirisha korosho zaidi ya asilimia 80. Kila mwaka barabara hii inatengenezwa lakini ukiisha msimu wa korosho inaacha mahandaki. Kwa hiyo ikijengwa kwa kiwango cha lami kwa kiasi kikubwa itaboresha mazingira ya ufanyaji biashara ndani ya Mkoa wetu wa Mtwara, kwa hiyo nakushukuru sana kwa hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ambalo nilitaka nilizungumzie ni suala la kupunguza ushuru wa korosho kwa wananchi. Napenda nilipongeze sana suala hilo kwa sababu siku nyingi tumekuwa tukilalamika wakulima wa zao la korosho wamekuwa wakikatwa makato mengi sana ambayo mengi hakuna hata moja linalowanufaisha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kato la shilingi 10,000 kwa kila kilo eti kwa ajili ya kikosi kazi kufuatilia ununuzi wa korosho. Kikosi kazi hicho ni watumishi wa Serikali, viongozi wa Serikali ambao wamepewa majukumu ya kufanya kazi hizo. Kazi walizopangiwa ni pamoja na kusimamia ununuzi wa zao la korosho, lakini walianza na shilingi moja, ikaenda shilingi tano, ghafla ikaruka shilingi 10 kila kilo ya korosho wao wanataka walipwe kama viongozi kwa ajili tu ya kusimamia ununuzi wa zao la korosho.
Mheshimiwa Naibu Spika, takwimu tulizonazo sasa hivi kwa mwaka tunazalisha zaidi ya tani 45,000, mwaka 2014 tulizalisha kwa mujibu wa korosho zilizosafirishwa nje ya nchi, tani 189,000. Mtwara peke yake inazalisha zaidi ya asilimia 80. Uchukue tu tani 100,000 zimetoka Mtwara na katika kila hizo tani 100,000 kila kilo moja mwananchi amekatwa shilingi 10 kwa ajili ya kuwalipa viongozi wanaosimamia ununuzi huo zaidi ya shilingi bilioni moja! Hivi tukienda kuwauliza hizo shilingi bilioni moja kwa biashara ya miezi mitatu wamezifanyia nini wataweza kutueleza? Wakati wana mishahara, wanatumia magari ya Serikali na kila kitu kimo wanafuatilia, mfano sasa hivi kuna utengenezaji wa madawati, wanalipwa shilingi bilioni moja kufuatilia utengenezaji wa madawati? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Serikali na hasa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa sababu Mheshimiwa Waziri Mkuu zao la korosho analijua hahitaji kuelekezwa na mtu, ana uzoefu alioupata kutokana na Chama chake cha Ushirika Kikuu cha Mkoa wa Lindi cha Ilulu na baada ya kuwa wamechoshwa na Ilulu wakaanzisha Lunali ambayo kwa kiasi kikubwa inafanya vizuri. Kwa hiyo, katika eneo hili Mheshimiwa Waziri Mkuu wala hahitaji kushauriwa na mtu, anajua mbichi na mbivu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu mimi pamoja na Wizara ya Fedha napongeza sana kwa yale makato ambayo yamepunguzwa na fedha hizi tunataka sasa ziende zikamnufaishe mwananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kule ndani eti kuna pesa zinakatwa kwa ajili ya unyaufu na korosho inaanza kunyauka baada ya miezi sita, lakini korosho zinafanywa minada kila wiki na ununuzi wa korosho unaanza mwezi wa kumi na unaisha kwa kuchelewa mwezi Januari. Sasa miezi hiyo mitatu hata kabla ya miezi sita kwa nini mwananchi akatwe eti ni unyaufu. Kwa hiyo niwaombe viongozi wenzangu wa Mtwara tumuunge mkono Mheshimiwa Waziri Mkuu, tuunge mkono Serikali yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wanakata shilingi 50 kila kilo ya korosho kwa ajili ya kusafirisha. Mimi katika Jimbo langu hakuna hata eneo moja ambalo linazidi zaidi ya kilometa 100, kwanza hazifiki. Sasa ndiyo kutaka kusema kwamba kila korosho inayosafirishwa tani 10 kutoka mahali popote, kilometa moja, kilometa mbili, kilometa tatu, tani kumi zinalipiwa shilingi 500,000. Kwa kweli huu ni unyonyaji wa hali ya juu, kwa hiyo, tumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nilitaka nilichangie ni ukusanyaji wa kodi za Halmashuri na TRA. Mimi sina ubishani wowote, property tax zikusanywe na TRA na vyanzo vingine vyote wakusanye lakini mchango wangu ni kwamba pesa zile zikishakusanywa, zote zirudi Halmashauri na zirudi kwa wakati kama ambavyo TRA inakusanya mapato yake kila mwezi ikishakusanya inayagawa katika Sekta mbalimbali ili ziweze kutumika katika mwezi unaokuja. Kwa hiyo, Halmashauri kila mwezi ipate mapato yake yaliyokusanywa katika mwezi ule ili yaweze kufanyiwa kazi katika Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunakusanya naomba pia tuwajengee uwezo watumishi wa Halmashauri ili zoezi hili liwe la mpito. Tufike mahali Halmashauri kupitia huu ugatuzi tunaozungumza wakusanye wenyewe. Isiwe kwamba mwaka huu waanze TRA halafu iwe ndiyo forever, tutakuwa hatuzijengei uwezo Halmashauri halafu ni kinyume cha sera yetu ya Ugatuzi wa Madaraka (Decentralization by Devolution). Kwa upande wa fedha huku tunaanza kurudi nyuma, lakini kama ni zoezi la mpito naliunga mkono lakini msisitizo wangu, kila mwezi Halmashauri zipelekewe pesa zao kwa sababu pesa hizi zimewekwa kwenye bajeti na wanazitegemea kwa ajili ya utekelezaji wa miradi.
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo jingine ambalo ningependa nilichangie ni suala la mradi wa viwanda vya chuma Liganga na makaa ya mawe Mchuchuma. Miradi hii ni miradi ambayo ni kama viwanda mama ambavyo vyenyewe vitachochea viwanda vingine. Kwa hiyo, mchango wangu nilitaka niseme viwanda hivi pia viangalie na ujenzi wa reli ya kutoka Liganga na Mchuchuma kwenda Mtwara ambavyo vinaenda sambamba...
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga Naunga mkono hoja.