Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi nichangie hoja hii iliyoko mbele yetu na nianze kutoa pongezi za dhati kabisa kwa Waziri wa Fedha, Naibu Waziri pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Fedha na Mipango kwa bajeti nzuri ambayo wameiwasilisha mbele yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja hii na nitatoa sababu kwa nini naiunga mkono hoja hii. Bajeti hii imeandaliwa kwa umakini mkubwa na ina dhamira ya dhati kabisa ya kuondoa matatizo ya wananchi na kuleta maendeleo. Ukiangalia sekta ya elimu, sekta ya elimu imetengewa kiasi cha shilingi trilioni 4.77 ambayo ni sawa sawa na asilimia 22.1 ya bajeti yote hii na mgawanyo huu wa fedha unaonesha bayana, jinsi gani ambavyo Serikali ina dhamira ya dhati ya kuwahudumia wananchi wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa elimu katika maendeleo ya nchi hii na ndio maana fedha zimetengwa za kiasi kikubwa na fedha hizi nyingi zitaelezwa katika miradi ya maendeleo.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naipongeza Wizara ya Fedha,kwa kuja na vyanzo vipya vya mapato ambavyo vitaiwezesha Serikali kupata fedha, za kutekeleza mpango ambayo imeahinishwa na kama walivyozungumza wachangiaji wengine, hii ni bajeti ya mwaka mmoja tu.
Mheshimiwa Naibu Spika,hii bajeti imetokana na Mpango wetu wa Maendeleo wa Miaka Mitano na imezingatia katika kutufikisha kule ambako tunatarajia kufika ukizingatia Ilani yetu ya uchaguzi na Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano, kwa hiyo niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuiunge mkono tukitambua kwamba hii ni bajeti ya mwaka mmoja, haiwezi kumaliza matatizo yote kwa sababu Serikali inakwenda hatua kwa hatua. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kuunga mkono bajeti hii ya mwaka mmoja, kutaiwezesha Serikali kuanza hatua yake ya kuwatumikia wananchi na kuwaletea maendeleo, katika maeneo ambayo yameainishwa. Vilevile napongeza kwa dhati kabisa, hatua za Serikali za kubana matumizi na kudhibiti matumizi yasiyokuwa ya lazima, hii yote inaonesha jinsi gani ambavyo Serikali ina dhamira ya dhati kabisa kuwatumikia wananchi wake hivyo tuna kila sababu ya kuunga mkono bajeti hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba sasa nizungumzie kidogo masuala ambayo yalielekezwa katika sekta ya elimu na kutokana na muda nitazungumzia mambo machache na mengine tutayajibu kwa maandishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, limejitokeza suala la fedha za utafiti,na Waheshimiwa Wabunge wameonesha wasiwasi wao kwamba kiasi cha fedha kilichotengwa ni kidogo na kwamba msisitizo katika utafiti wa kilimo, haupewi kipaumbele kinachotakiwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kusema kwamba Serikali imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya utafiti, kupitia kwenye Tume ya Taifa ya Utafiti yaani COSTECH; na kuna kazi nyingi ambazo zimekuwa zikifanyika na utaratibu tu ambao umekuwa ukitumika ni utaratibu wa ushindani. Kumekuwa na hoja kwamba kwa nini utumike utaratibu wa ushindani kutoa fedha za utafiti?
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa ushindani kwanza unaihakikishia Serikali kwamba yule anayeomba fedha yuko tayari, kwa maana ya kwamba tayari atakuwa na mpango kazi wake. Anajua anataka kufanya nini kwa hiyo inaihakikishia kwamba yule anayepata fedha kwa ushindani anakuwa anazitumia fedha hizo vizuri, badala ya kuzigawa hata kwa mtu ambaye hajawa yuko tayari.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia suala la ushindani jumla ya miradi 102 imeweza kufadhiliwa,na ambapo kuna masuala mengi tu yamefanyika ikiwa ni pamoja na kujenga rasilimali watu kuwajengea uwezo wa kuweza kufanya utafiti; na katika hilo jumla ya watafiti 517 wamepatiwa mafunzo na jumla ya watu 130 wamepata mafunzo katika ngazi ya uzamili na uzamivu. Vilevile fedha za utafiti zimewezesha kujenga miundombinu ya kufanyia utafiti ambapo kwa mfano Serikali imeweza kujenga mabwawa 42 ya zege na kukarabati maabara za uzalishaji wa vifaranga vya samaki katika Chuo Kikuu cha Sokoine.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika bajeti ya mwaka 2016/2017 Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 12.8 kwa ajili ya suala la utafiti. Lakini pamoja na fedha hizi, bado Serikali itaendelea kupata fedha kupitia kwa wafadhili mbalimbali ambao wamekuwa wakipeleka fedha hizo moja kwa moja katika vyuo vyetu vya elimu ya juu.
Suala lingine ambalo limezungumzwa katika Wizara yangu ni suala la kuitaka Serikali iangalie kozi zinazoanzishwa katika vyuo vya elimu ya juu, kujiridhisha kama kuna walimu wa kutosha. Niwahakikishie Watanzania kwamba katika kuhakikisha ubora wa elimu hiyo ndio kipaumbele chetu katika Awamu ya Tano. Hivyo basi hakuna kozi yoyote ambayo itaanzishwa kama Serikali haijaridhika na miundombinu, kama Serikali haijaridhika na uwepo wa elimu ambao wana sifa stahiki. Pamoja na kuangalia kozi mpya lakini niseme kwamba hata kozi ambazo zipo Serikali inafanya mapitio kuona kwamba kozi zote zinazotolewa katika elimu ya juu zina wataalam wa kutosha na ziko katika mazingira ambayo yanastahiki. Kwa hiyo, tutachukua hatua zinazostahiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo limezungumziwa ni suala la ukarabati wa vyuo vikuu, pamoja na miundombinu ya kutolea elimu. Ukiangaliwa kitabu cha hotuba ya bajeti ya Waziri wa Fedha na kitabu cha hotuba cha Wizara yangu, tumebainisha wazi mikakati ya Serikali katika kuhakikisha kwamba tunakarabati miundombinu ya shule na vyuo vikuu ili kuhakikisha kwamba Watanzania na wananchi wanapata elimu katika mazingira ambayo ni rafiki na kama nilivyosema tunafanya hatua kwa hatua, kwa mfano katika mwaka huu wa fedha, tutaweza kufanya ukarabari kwenye shule kongwe 40. Lakini vilevile Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambacho ni Chuo Kikuu kongwe tumekitengea kiasi cha shilingi bilioni tisa kwa ajili ya kufanya ukarabati na hili zoezi ni endelevu. Kama nilivyosema hii ni hatua tu, lakini ahadi zetu zitatekelezwa katika miaka mitano. Kwa hiyo tutaendelea kukarabati na kuhakikisha kwamba mazingira ya kujifunzia yanakuwa ni rafiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo limezungumziwa ni suala la elimu bure, kwamba hii sera iende mpaka kidato cha sita. Ninachoweza kusema ni kwamba kama Serikali, tumepokea huo ushauri lakini tungeomba kwamba kama tunavyosema tunataka utekelezaji wetu wa ahadi kwa wananchi uende hatua kwa hatua. Kwa hiyo tumeanza na mpaka kidato cha nne tungeomba kwanza tuendelee kuimarisha utekelezaji wa sera ya elimu bila malipo kwa kidato cha nne na kutatua changamoto ambazo zipo kabla hatujafikiria kuongeza wigo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine lililozungumziwa katika eneo langu ni suala la VETA kuwa na vifaa vya kisasa na hilo tutalifanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.