Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA – MHE ANGELLAH J. KAIRUKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Bajeti hii Kuu ya Serikali.
Napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Ashatu kwa maandalizi mazuri ya bajeti na kwa kweli ukiangalia sura ya bajeti hii unaona kabisa ni kwa namna gani Serikali imejipanga katika kumkwamua Mtanzania wa kawaida ili aweze kuona nafuu katika maisha yake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza zaidi kwa namna ambavyo Wizara imeandaa Sera ya Matumizi katika kuhakikisha kwamba tunabana matumizi yasiyokuwa na tija na kuhakikisha kwamba Serikali itakuwa na matumizi yale tu ambayo kwa kweli, yataweza kuwa na tija kwa wananchi wake.
Mheshiumiwa Naibu Spika, napongeza zaidi kwa jitihada za Wizara ya Fedha za kuamua kuja na marekebisho ya Sheria ya Manunuzi ya Umma na kwa hakika kupitia Sheria hii pindi itakapopitishwa itaweza kuwa na manufaa makubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, niingie sasa katika hoja ambazo zimegusa Ofisi yangu na katika hoja ya kwanza ilikuwa ni katika suala zima la watumishi hewa. Kulikuwa na hoja, baadhi ya Wabunge walitaka kufahamu ni hatua gani zimechukuliwa dhidi ya Maafisa Masuuli, dhidi ya Wakuu wa Idara pamoja na vitengo mbalimbali vya Uhasibu ambao kimsingi wao wameamini kwamba wanaweza kuwa walishiriki katika masuala haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kusema kwamba, kimsingi watumishi hewa wanatokana na kwamba, unakuta wakati mwingine labda mtu amefariki, wengine unakuta ni watoro, lakini wanatakiwa wawe wameondolewa katika orodha ya malipo ya mishahara au Payroll, lakini wale waliokasimiwa mamlaka wanakuwa hawajatimiza wajibu wao ipasavyo. Wako watumishi wengine wanakaa katika Payroll na walitakiwa waondoke, hadi inafikia hata miezi 10 na zaidi!
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba, kama Serikali, ili kukabiliana na tatizo hili tumekuwa tukiendelea kuchukua hatua na tunaendelea kumshukuru sana pia, Mheshimiwa Rais kwa jitihada zake na kwa msukumo ambao ameupatia katika suala hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, niwahakikishie tu kwamba, kwa sasa ambacho tumkifanya, kwanza kabisa ni kuhakikisha kwamba tunawaondoa watumishi wote ambao tumewabaini mpaka sasa; na tumeshabaini watumishi hewa 12,246 ambao endapo wangeendelea kuwepo katika orodha ya malipo ya mishahara, takriban shilingi bilioni 25.091 ingeendelea kulipwa kila mwezi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba, ukiangalia, hii ni kuanzia Mwezi Machi tu, tarehe 1; mpaka tarehe 30 Aprili, ambapo Mheshimiwa Rais alitangaza, walibainika watumishi hewa 10,295 na mpaka tarehe 30 Mei ndiyo hii watumishi 12,246!
Mheshimiwa Naibu Spika, tulichokifanya hivi sasa tumezielekeza Mamlaka zote za ajira kuhakikisha kwamba wanachukua hatua za kinidhamu na za Kisheria. Hatutaki tu tutangaze kwamba tumeshaokoa kiasi kadhaa na kuondoa watumishi hawa hewa. Tunachokitaka hivi sasa; na ninapongeza sana mamlaka mbalimbali za ajira katika Mkoa wa Singida, mamlaka mbalimbali za ajira Mkoa wa Dar es Salaam, Mtwara na mikoa mingine yote kwa kazi nzuri ambayo wameifanya katika kuhakikisha kwamba watu wote walioshiriki katika kusababisha watumishi hewa kuwepo, wameweza kuchukuliwa hatua.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaendelea kushirikiana na Ofisi ya Mkurugenzi Mkuu wa Mashitaka na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kuhakikisha kwamba mashitaka yote ambayo yatakuwa yamefunguliwa dhidi ya wale ambao walikuwa wakitafuna fedha za Serikali ambazo hazikuwa zinapaswa kulipwa kwao, lakini vilevile kuhakikisha kwamba, Maafisa Utumishi ambao kimsingi ndio tiumewaidhinishia matumizi ya mfumo huu, tumefundisha Maafisa Utumishi 1,500.
Mheshimiwa Naibu Spika, tutakuwa tayari wakati wowote hata ikibidi kuwasimamisha Maafisa Utumishi hao wote 1,500 ili tuweze kuanza upya, tuwe na Maafisa Utumishi wenye uadilifu, wenye uzalendo na ambao wana hofu ya Mwenyezi Mungu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba, naendelea kuomba mamlaka za ajira wahakikishe kwamba, wanachukua hatua za kinidhamu pamoja na za Kisheria na wahakikishe mashitaka yote yanafikishwa katika mamlaka zinazohusika. Kwa wale ambao watashindwa kuweza kuchukua hatua stahiki kwa zile mamlaka za ajira kwa Maafisa Masuuli na wengineo tutawachukulia hatua kali za Kisheria kwa mujibu wa Sheria, Kanuni pamoja na taratibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja nyingine iliyouliza, endapo kuna umuhimu wa kuwa na PDB au la!
Mheshimiwa Naibu Spika, wote tunafahamu Ofisi ya Rais ya kusimamia ufuatiliaji wa utekelezaji wa miradi. Ofisi hii ilianzishwa mwaka 2013 na niseme tu kwamba, ni ofisi ambayo kwa kweli ni ya muhimu sana. Ukiangalia katika manufaa mbalimbali ambayo yameshapatikana hadi hivi sasa, sekta takriban 13 za kipaumbele zimeweza kuutumia mfumo huu na zimeweza kufuatilia na kutekeleza miradi yake mbalimbali kwa kweli kwa mafanikio makubwa na tumeshuhudia mafanikio ya takribani asilimia 71.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ukiangalia katika ushirikiano ambao PDB imekuwanao na Pemandu ya Malaysia, ni mfumo ambao ukiangalia Uingereza wameutumia, Rwanda wameutumia, Malaysia wameutumia na kwa kweli, wameona mafanikio makubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda tu kulieleza Bunge lako Tukufu kwamba, pamoja na kwamba, sekta ambazo ziko katika mfumo huu ni 13, lakini hivi sasa Mahakama haikuwepo katika mfumo huu, lakini wenyewe walishaanza kutekeleza mapendekezo ya mfumo huu na wamefanya vizuri sana nawapongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, nalipongeza pia Jeshi la Polisi na ninapenda pia kupongeza mamlaka mbalimbali za maji Mijini kwa namna ambavyo wameimarisha utekelezaji wa majukumu yao, lakini vilevile namna ambavyo wamekuwa na mafanikio katika kupanga na kufuatilia matokeo ya miradi yao mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ukiangalia ofisi hii itakuwa ya muhimu zaidi hasa katika mwaka huu ambapo tumekuwa na mapinduzi katika maandalizi ya bajeti. Takribani asilimia 40 ya bajeti yote ya Serikali itaenda katika miradi mbalimbali ya maendeleo. Usipokuwa na ufuatiliaji mzuri na tathmini, ni namna gani fedha zako zimeenda huko? Ni vipaumbele gani ulikuwanavyo?
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuwa na ripoti mbalimbali za kila wiki ili kuweza kujua namna miradi mbalimbali inavyotekelezwa. Kwa hiyo, niseme tu kwamba, naendelea kuomba mamlaka mbalimbali ambazo ziko katika mfumo huu, lakini na nyingine ambazo bado hazijajiunga na Mfumo wa BRN basi wajitahidi kuona ni kwa namna gani wanaweza wakajiunganao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na ninaunga mkono Bajeti hii Kuu ya Serikali.