Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Azimio la Bunge Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Matumizi ya Dawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Michezoni

Hon. Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Azimio la Bunge Kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Matumizi ya Dawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Michezoni

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, WASANII NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, ikiongozwa na Mheshimiwa Peter Joseph Serukamba. Namshukuru sana Mheshimiwa Juma Nkamia kwa kuwasilisha maoni ya Kamati na nashukuru kwa ushauri wao na kwa kweli ushiriki wao katika kuhakikisha Azimio hili linafika hapa lilipofika, nawashukuru sana!
Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa masikitiko pengine, kwa kutopata mawazo ya Kambi Rasmi ya Upinzani kwa uwasilishaji wa kutosha ukiacha kuleta hotuba yao hapa kwa uamuzi ambao pengine wanadhani unawasaidia wao, lakini nadhani utaratibu huu mbovu wa kuwa wanakuja wanasaini, wanachukua posho na kuondoka haufai!
Mheshimiwa Naibu Spika, michango iliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge, inaonesha namna ambavyo ni muhimu sasa kwa Tanzania kuridhia mkataba huu ili Taifa letu liweze kunufaika na fursa zitokanazo na mkataba huu ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa ushindani uliosawa michezoni na pia kulinda afya na ustawi wa michezo na wanamichezo wetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo, sasa nitoe ufafanuzi wa hoja chache. Niwashukuru Wabunge wote waliochangia, natambua mchango wa Mheshimiwa Hafidh Tahir Ali, Mheshimiwa Stanslaus Nyongo, Mheshimiwa Joseph Kakunda, Mheshimiwa Esther Mahawe, Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile, Mheshimiwa Venance Mwamoto, Mheshimiwa Seleman Jafo, Naibu Waziri wa TAMISEMI, mchango pia wa Dkt. Mwakyembe, Waziri wa Katiba na Sheria. Pia namshukuru sana Naibu Waziri wa Wizara hii kwa ufafanuzi wa baadhi ya hoja zilizowasilishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nilihakikishie Bunge lako, utayari wa Serikali katika kutekeleza mkataba huu. Kuna mashaka yameoneshwa hasa kwenye maneno ya Kambi ya Upinzani Bungeni kwamba wakati mwingine mikataba hii inaridhiwa halafu utekelezaji wake unakuwa na mashaka. Nataka nilithibitishie Bunge lako, kwanza, kitendo cha kuleta mkataba huu uridhiwe Bungeni ni uthibitisho kwamba, Serikali iko tayari kuutekeleza ndiyo maana tumeuleta hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, tayari kama alivyosema Naibu Waziri, tumeshaanzisha ofisi pale Uwanja wa Taifa. Uanzishwaji wa ofisi hii ambayo itashughulikia jambo hili pia ni uthibitisho wa utayari wa Serikali kutekeleza mkataba huu. Kwa hiyo, sioni sababu ya kuwa na mashaka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumeshapeleka wataalam wetu kwenda kufanya mafunzo ya awali. Watumishi kadhaa wamekwenda wamefanya mafunzo ya awali juu ya utafiti, elimu na mafunzo katika kutekeleza jambo hili, tuna hakika wataalam wetu wamefanya vizuri kwenye mafunzo yale na wako tayari kwa kazi hii. Kwa hiyo, walichokuwa wanasuburi ni kuridhiwa tu kwa mkataba huu ili waanze utekelezaji. Hivyo, nataka nilihakikishie Bunge lako kwamba, Serikali iko tayari kutekeleza mkataba huu. Sasa hivi tuko katika mchakato wa kupitia upya sera ya michezo na sheria zinazoongoza Baraza la Michezo katika nchi yetu. Katika mapitio haya tutazingatia uwepo wa sheria, ambazo zitasaidia sana utekelezaji wa Mkataba huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya Bunge katika maoni yao ya Kamati wameeleza kwa umuhimu sana na hata baadhi ya Wabunge waliochangia, suala la kuelimisha wadau juu ya jambo hili. Jambo hili ni kubwa, lina madhara makubwa lisipotekelezwa vizuri na inawezekana kwa kutokuwa na elimu ya kutosha, utekelezaji wake ukawa na tabu!
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imejipanga vizuri kuhakikisha pamoja na wadau ambao kwa kweli hata mwanzo wakati tukijadili mkataba huu, tulikuwa tukizungumza jambo la kutoa elimu ya kutosha kwa wanamichezo wetu na wadau wetu kwa pamoja ili walielewe vizuri jambo hili ili utekelezaji wake uwe na mafanikio.
Mheshimiwa Naibu Spika, natambua mchango wa Dkt. Mwakyembe, alikuwa anazungumza hapa wakati mwingine, kwetu huku unaweza ukawa na vitu, ambavyo huvioni kama vina madhara kwenye kuongeza nguvu kwenye mwili, lakini baada ya kuvitumia vinaoneka ni vya kawaida vikawa na madhara.
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo haya yote tutayazingatia kwa pamoja kuhakikisha elimu inayotolewa inasaidia na kwa kuwa naamini Bunge lako litaridhia, sisi tutakuwa moja ya wanachama halali kwenye harakati hizi. Kwa hiyo, baadhi ya maoni na ushauri wa namna ya kuboresha hata mkataba wenyewe, tutakuwa na fursa ya kutoa maoni yetu kama wanachama halali.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati ya Kudumu ya Bunge imependekeza na mengi kwa kweli ni mapendekezo kwamba mkataba usainiwe mapema. Wanasema ni rai ya Kamati kuwa, maazimio ambayo ni mazuri na yenye faida kwa nchi yetu, Serikali iwe inaridhia mapema ili kuweza kunufaika nayo kama inavyokusudiwa. Ni kweli ushauri ni mzuri, lakini pia nadhani ni vizuri kuchukua tahadhari kutosaini kwa haraka baadhi ya mikataba, ni vizuri tukajiridhisha kama ina manufaa kwa nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati pia inaishauri Serikali kuangalia sheria mbalimbali zilizopo na kuona zinaweza kukidhi mahitaji ya Azimio hili. Kama nilivyosema kwamba, tunapitia upya sasa Sheria ya Baraza la Michezo na Sera zake, kuona namna gani tutaziboresha ziendane na wakati na moja ya jambo kubwa tutakalolizingatia ni namna ambavyo sheria hizi zitasaidia utekelezaji wa Azimio hili.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati imetushauri pia kwamba, utekelezaji wa mkataba huu uzingatie kundi la wakufunzi. Zimekuwepo hizi hoja hapa kwamba, siyo wanamichezo tu pengine na wakufunzi nao, tutazingatia ushauri huo. Ilikuwepo hoja iliyotolewa na Mheshimiwa Stanslaus Nyongo kwamba pamoja na mkataba huu lakini bado michezo yetu inakabiliwa na changamoto nyingi likiwemo tatizo kubwa la rushwa kwenye michezo, ambalo linachangia sana uporomoshaji wa michezo katika nchi yetu na hasa kwenye eneo la upangaji wa matokeo.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa hotuba ya bajeti ya Wizara yangu, nilizungumza hili kwamba, ni changamoto kubwa katika michezo yetu. Sisi tumejipanga kuanza na vita dhidi ya rushwa kwenye Vyama vya Michezo. Kwa sababu kule ndiko ambako pasipotengenezwa vizuri tunapata viongozi ambao wanatokana na rushwa, wakiingia kwenye michezo, maslahi yao siyo kuendeleza michezo, maslahi yao ni kurudisha pesa walizozitumia kuingia madarakani. Kwa kuwa, ziko chaguzi mbalimbali zinaendelea, nitoe wito kwa vyombo vyetu hasa TAKUKURU kutusaidia kupambana kiukweli na tatizo hili kubwa la rushwa kwenye hasa chaguzi za Vyama vyetu vya Michezo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati pia imeshauri lishe bora kwa wanamichezo kama sehemu mojawapo ya kuangalia kwamba wanamichezo wetu, basi hawakumbwi na maswahibu haya, lakini pia wanafanya vizuri michezoni. Nadhani ni ushauri mzuri na Wizara tunauchukua na tutaufanyia kazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nichukue nafasi hii kuwashukuru Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Hawa wanasaidiana na sisi na kwa kweli wao ndiyo waratibu wa michezo kwenye shule zetu kwa commitment yao, kwa sababu kama elimu hii ya utekelezaji wa Azimio hili itaanza kutolewa vizuri kwa vijana wetu na mwezi huu mwishoni wanaanza mashindano pale Mwanza, naamini tukitumia fursa hii tutajenga vijana wanaojiamini, wanaotumia uwezo waliojaliwa na Mwenyezi Mungu kuonesha vipaji vyao, tutapata wachezaji wazuri. Nadhani huku ni mwanzo mzuri na tutatumia fursa hiyo kila michezo hii inapofanyika, ikiwezekana mpaka mashuleni, elimu hii itolewe ili vijana wetu wajiamini, waachane na vishawishi vya kutumia madawa kuongeza nguvu michezoni.
Mheshimiwa Naibu Spika, na tunaamini hili likifanyika, samaki ukimkunja angali mbichi inawezekana mambo yakawa mazuri. Kwa hiyo, uamuzi wa kupitisha Mkataba huu kwa Bunge lako kutasaidia sana kuliletea heshima Taifa letu. Mwezi wa Nane tunakwenda kwenye michezo ya Olympic, safari hii tutakwenda kifua mbele kwa sababu tumeridhia na tumesaini mkataba huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoa ufafanuzi huo, sasa naliomba Bunge lako Tukufu, liridhie Mkataba wa Kimataifa wa Udhibiti wa Matumizi ya Dawa na Mbinu za Kuongeza Nguvu Katika Michezo, yaani International Conversion Against Doping in Sport wa Mwaka 2005.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.