Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nichukue nafasi hii kukupongeza kwa namna unavyoendesha Bunge hili na naamini kwamba kuanzia siku ya kwanza ingekuwa wote tunasimamia kanuni na utaratibu ambao tumejiwekea kisheria, haya mambo yote yasingetokea. Kwa hiyo, uendelee na msimamo huo kwa sababu bado huu ndiyo mwanzo. Kwa hiyo tukianza kuzoea kufuata taratibu, kanuni na sheria huko mbele ya safari tutakuwa tunakuja hapa na kulenga hoja mbalimbali katika kuishauri na kuisimamia Serikali, hizi siasa nyingine zote tutazifanya huko nje ya hapa. Kwa hiyo, nakupongeza sana na naomba uendelee na msimamo huo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza Waziri wa Fedha, Naibu wake, Katibu Mkuu ambaye anaongoza na timu nzima ya wataalam kwa juhudi kubwa wanayofanya na wametuletea Mpango wa Maendeleo na Bajeti ya Wizara yao, ambapo Wizara hii ndio Wizara mama inasimamia Wizara nyingine zote. Mafanikio yao ndiyo mafanikio ya Wizara nyingine zote. Kwa hiyo, nimpongeze Rais kwanza kwa kuwateua, lakini kwa uzoefu wake Waziri na timu yao na namna wanavyokubali ushauri, niwapongeze sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze kwenye masuala mawili muhimu. Moja, wenzangu wengi wamesema, ni Sheria ya Manunuzi. Naomba nisisitize kwa Wabunge wenzangu wote; kama itatokea kwamba sheria hii haijaletwa muda bado tunao wa siku 21 wa kuleta hoja binafsi ya kubadilisha baadhi ya vipengele ili fedha nyingi ambazo tutapeleka kwenye maendeleo, asilimia 40, zikatumike vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama itakuwa tupo nje ya muda basi nitaomba Wabunge wenzangu wote tukubaliane tutakapopitisha Bajeti Kuu ya Serikali tuweke kipengele kwamba pesa za maendeleo hata shilingi isitumike mpaka hapo hiyo sheria itakaporekebishwa. Fedha ziwekwe kwenye akaunti maalum, sheria ije, ikipita ndipo fedha zitumike, kwa sababu hiki kimekuwa ni kilio cha miaka mingi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nizungumzie juu ya Sheria ya Micro-Finance. Serikali imekuja na mpango mzuri wa kupeleka milioni 50 kwa kila Kijiji. Kule ni masuala ya Village Empowerment, ile milioni 50 kama VICOBA haitakuwa kisheria ambapo inategemeana na Sheria hiyo ya Micro-Finance bado tutarudi pale pale. Kwa hiyo, ningeomba sheria ya Micro-Finance ni muhimu ije mapema ili zile fedha zikienda kule usimamizi wake uwe kisheria na uweze kusimamiwa vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mbali na hiyo pia ningeomba Wizara ya Fedha iishauri Serikali ingalie namna ya kuhakikisha kwamba tunapata sheria. Asilimia kubwa ya taasisi zetu za Serikali ambazo zinafanya huduma mbalimbali; kwa mfano huduma za simu na data za TTCL, lakini pia NIC. Hapa tumeoneshwa kwenye kitabu, Waziri ametaja baadhi ya mashirika ambayo yanafanya biashara na NIC; leo NIC haina mtaji mkubwa. Ningeshauri kazi zote za Serikali iwepo sheria kwamba zote ziende NIC. Mashirika mengi ya umma hayapeleki kazi huko, kwa hiyo taasisi zote za umma na Serikali zifanye kazi na TTCL, NIC, kazi nyingi ziende VETA, ziende Magereza. Taasisi za Serikali hakuna haja ya kuwapa fedha za kujiendesha wapewe biashara ili waweze kujiendesha wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ni vizuri Serikali ikaangalia namna ya kuangalia hizi regulatory bodies zote, zote ziunganishwe ziwe regulatory body moja na nyingine zote ziwe idara chini yake. Tuangalie sheria zilizounda hizo regulatory bodies ili zifanyiwe kazi na zote ziunganishwe na iwe moja; hii italeta mazingira mazuri ya kufanyia biashara nchini. Wakati wanakwenda kwenye kukagua viwanda, biashara au shughuli yoyote basi ni taasisi moja inakwenda, tozo inakuwa moja ndogo, itakuwa mazingira wezeshi kwa wafanyabiashara. Huko tunapotaka kuelekea, kwenye uchumi wa viwanda, hiyo body ikiwa moja tozo itapungua na ufanisi wa kazi pia utakuwa ni mzuri. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ili kupunguza gharama za kuendesha hizi bodies mbalimbali za Serikali na taasisi zake tungeangalia namna ya kuziunganisha. Kwa mfano RAHCO na TRL zote shughuli ni moja, zingeunganishwa. Mfano mwingine ni kwenye TBS na Weight and Measurements; zingeunganishwa ili shughuli hizi zote zinazofanana zifanywe na moja ili gharama za usimamizi na management yote ipungue na OC nyingi zitapungua. Kwa hiyo, tuhakikishe kwamba tunaweza kufanya namna ya kuziunganisha taasisi nyingi hizi za Serikali ili kupunguza gharama. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu nyingine nitakayoendelea kuisisitiza ni kwamba Serikali iangalie na iwe na nidhamu ya matumizi ya fedha. Fedha ambazo ni ring-fenced Wizara ya Fedha ijitahidi isitumie sehemu yoyote nyingine. Pia katika hii Mifuko mitatu; Mfuko wa Bunge, Mfuko wa Mahakama na Mfuko wa CAG, fedha zile ziwe consistent ziende kwa wakati, hasa kwenye huu Mfuko wa Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali; wao wanakwenda kwa calendar year na wanafuata ratiba. Tunawaomba muwape kipaumbele na zile fedha zihakikishwe kwamba zinaenda kwa wakati kufuatana na kalenda yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tutakapokuja kwenye mid-year review; kwa sababu hawataweza kufanya kazi yao inavyopaswa, ni vizuri tuangalie ili waongezewe bajeti wanayoihitaji. Kwa sababu ya fedha za maendeleo tutazoongeza, hiyo asilimia 40, ni muhimu sana watchdog, ambayo ni Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ipatiwe fedha za kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la mid-term review naamini kwamba hiki kidogo ambacho Serikali inacho sasa hivi, basi tukisimamie vizuri na wote tuwe wavumilivu. Nina uhakika kutokana na uwazi na maoni na ushauri unaopokelewa na Wizara safari hii, naridhika kabisa kwamba najua huko tutafika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ningeomba; Wizara ya Fedha kwenye Tume ya Mipango iwawezeshe sana, tena wewe mwenyewe Waziri ulikuwa huko kwa muda mrefu; tunaomba pawe na namna ya kuiunganisha Tume hiyo ifike mpaka ngazi ya Mkoa na Wilaya kwa sababu huko ndio tunakopanga mipango. Kwa sababu Halmashauri na Mikoa yetu ingekuwa na mipango mizuri basi na huku juu pia hii mipango itakuwa ni endelevu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunaomba Tume hiyo ndiyo iwe inashauri. Kwa mfano, kwenye Halmashauri yangu na Halmashauri nyingi, Afisa Mipango ni mmoja hivyo ni ngumu sana kupanga mipango mingi. Hii mipango ikiwa integrated, yaani wakiwa wanafanya kazi kwa pamoja mafanikio ya Serikali yatakuwa yanaonekana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu nyingine ni suala la kuhakikisha kwamba tunaongeza mapato ya Serikali. Taasisi ambayo inakusanya mapato ya Serikali (TRA) tunawapongeza, lakini kwenye baadhi ya maeneo waendelee kujirekebisha. Kwa mfano, suala la uplifting kwenye bidhaa ambazo zinaingizwa ni kero kubwa ambayo inawakatisha tamaa wafanyabishara. Lakini pia kuna kodi nyingine wanakusanya ambazo tayari sheria ilishafuta, sasa na hizo pia zifanyiwe kazi. Yale ambayo tunaongeza yaongezwe immediately lakini yaliyoondolewa pia yaondolewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, muhimu ni kwamba kila Mtanzania ajitahidi kuwa na tabia ya kulipa kodi, bila kulipa kodi sisi wenyewe basi huko hatutaweza kufika na haya malengo ambayo tunajiwekea hatutayafikia. Kwa hiyo, pawe na fair trade competition kila mahali.
Mheshimiwa Naibu Spika, lingine muhimu ni ile Tume ya Fair Competition Commission, tunaomba basi bodi yake iundwe mapema ili hizi shughuli nyingine ambazo zinakwama kutokana na shughuli ambayo inatakiwa kufanywa na hiyo Commission basi hizo ziweze kufanywa mapema.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia sehemu nyingine muhimu ni kuhakikisha kwamba kodi na tozo zile ambazo ni kero katika biashara Wizara ya Fedha ingekuwa na timu maalum ambayo itakuwa inafanya uchunguzi, la si vyo hii ndoto yetu ya kufika kwenye uchumi wa viwanda hatutafikia na bado bidhaa za nje sisi hatutakuwa na uwezo wa kuwa kwenye ushindani nazo. Kwa hiyo, zile kodi na tozo ambazo ni kero ambazo zinafanya biashara hizo zisifanikiwe, basi ziondolewe na pawe na mazingira wezeshi ili wafanyabiashara wetu waweze kufanya biashara vizuri zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nina imani kubwa na timu nzima ya Wizara ya Fedha na kuna masuala mengi ambayo wameweza kuweka wazi safari hii pia. Hata kile kitabu cha volume one tulipewa kabla ya muda wa bajeti, ambapo huko miaka ya nyuma huwa tunapewa siku ile ambapo Bajeti ya Serikali inasomwa, kwa hiyo hata mwelekeo wa namna ya makusanyo tayari tumeshaanza kuyajua. Muhimu tena naomba Benki hii ya Kilimo ipatiwe fedha ya kutosha ili uchumi uendelee kukua.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo machache, naomba nishukuru na naunga mkono hoja mia kwa mia.