Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa maoni yangu au mchango wangu kwenye hotuba hii muhimu ya Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango. Kabla sijatoa maoni yangu na mimi niungane na wenzangu waliokupongeza wewe kwa msimamo sahihi, haki na kutokubali kuyumbishwa. Nadhani ni mmoja kati ya watu ambao tayari nilishakupongeza na uendelee na msimamo huo. Ningekuwa nina uwezo wa kukupangia basi ningesema umalize ngwe hii yote mpaka tutakapoondoka, nakushukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie maeneo machache tu katika Hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, nikianza na lile la mafanikio ya MKUKUTA II.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri amesema vizuri kwamba mafanikio makubwa yameonekana katika MKUKUTA II na moja ya mafanikio hayo ni pale ambapo umaskini umepungua kwa karibu asilimia 6.2. Sasa tukiangalia mmoja mmoja kwenye Majimbo yetu basi ndipo tunapoona kwamba kipimo kile kumbe sisi wengine bado hatujakifikia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwangu mimi vijiji vyangu nikianza na pale nilipozaliwa Lugeni niende maeneo mengine ya Konde, Kisaki Station, Nyingwa ni ndoto ukisema kwamba umaskini umepungua; umaskini umeongezeka. Sasa hii maana yake ni kwamba mpango huu haukuwanufaisha wale waliolengwa na inawezekana sana Waheshimiwa Wabunge, Madiwani na watendaji wengine wa karibu na wananchi hawakuhusishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe kwenye mpango mwingine unaokuja na matayarisho yake yaanze sasa, tuwe na takwimu sahihi ya hao walengwa, tuwe na utaratibu mzuri wa kuwafikia hawa walengwa, Wabunge wahusishwe kikamilifu, sisi ndiyo tunaojua watu wetu wanaohitaji msaada mkubwa, tunaojua umaskini umekaa wapi ili mafanikio haya yanayozungumzwa sehemu nyingine yaweze kufika kwenye maeneo yetu haya ambayo kwa bahati mbaya kwenye MKUKUTA II hatukuweza kunufaika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie pia suala la hili la Sheria ya Manunuzi. Wenzangu wamesema na mimi niongeze tu sauti. Nashukuru sana kaka yangu Mheshimiwa Chenge ametuonesha ukubali wake na utayari wake wa kulifanya hili kama Serikali itakuwa bado ina kigugumizi cha kuleta hapa mbele ya Bunge. Sidhani kama Serikali inaona ugumu; ninachojua kwa sababu nimetoka huko Serikalini, muda wote nilipokuwa pale Serikalini kilio ni hicho hicho kwamba sheria hii ni mbaya, itokee nafasi tuibadilishe.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nashangaa fursa hiyo tunaiacha inapita lakini hata Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alituahidi hapa Bungeni kwamba sheria hii italetwa ili tuweze kuibadilisha; nawaomba sana Serikali, Waziri wa Fedha , ashughulikie hili tulimalize. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu naomba nilizungumzie hili ambalo pia wenzangu wamelizungumza, pesa hii shilingi milioni 50 kwa kila Kijiji. Hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, Mkuu wa nchi, imetangazwa nchi nzima, dunia nzima inajua hakuna shortcut yake, ni utekelezaji tu unaotakiwa hapa. Mheshimiwa Waziri utafute hizi pesa tutengeneze utaratibu mzuri ili pasiwepo na ufujaji wa pesa hizi ili kwa kweli wananchi wetu maskini waweze kunufaika na mchango huu mkubwa uliotolewa na Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wapo Wabunge wenzangu wawili wamezungumzia kuhusu mikopo ya benki za biashara. Mikopo hii inayotolewa kwa wananchi na kwa kweli mwananchi anapokwenda kukopa ni kwamba, ana shida, lakini mabenki haya yanatumia shida za hawa wananchi kuwabana. Dhamana wanayoweka ya nyumba, mikopo hii masharti yake ni magumu sana, utekelezaji wa mkopo huu ukijumlisha na riba, mkopo unakuwa ni mara mbili. Wapo wananchi wengi sana wamepoteza nyumba zao za kuishi, wengine wamejiua, wengine wamepata maradhi ya kusononeka na wengine ndoa zao zimeharibika.
Mheshimiwa Naibu Spika, yote haya yameletwa kwa sababu nadhani Serikali haikuangalia sana. Faida zinazotengenezwa na benki hizi kutokana na mikopo hii, wote sisi ni mashahidi, baada ya mwaka utasikia wametengeneza bilioni 10 wanagawana; lakini wamefanya hivi kwa kumgandamiza huyu mwananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hebu Wizara ya Fedha ikishirikiana na Benki Kuu iangalie upya mwenendo wa benki hizi na mikopo yao kwa wananchi na hasa kama inawezekana, dhamana hii ya nyumba itolewe katika mpango mzima wa kuwakopesha watu. Kwa sababu kwa kusema ukweli tunawarudisha wananchi wetu kwenye umaskini mkubwa sana kwa ajili ya matatizo haya ya mikopo ya kibenki.
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Fedha ametuelezea kuhusu ukusanyaji wa mapato ya Serikali, na katika hotuba yake ameeleza kwamba wafadhili kwa mwaka 2015/2016 wameweza kupunguza ahadi yao ya mchango kutoka Shilingi bilioni 660 hadi kufikia Shilingi bilioni 399, punguzo hilo ni karibuni asilimia 40. Hili jambo linanisikitisha sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, hawa ni wafadhili ambao tuliona ni marafiki zetu, tumekaa nao katika meza, tumewaeleza mipango yetu na wao wala si kwa kushurutishwa wamekubali kuchangia hicho walichoahidi. Leo hii kwa sababu yoyote ile wanafika mahali wanajitoa anavuruga kabisa bajeti na mpango mzima wa maendeleo wa nchi yetu, haikubaliki. Serikali inatakiwa iwaeleze, Serikali inatakiwa ifike mahali ijulishe dunia kwamba hawa ni marafiki ambao wametuangusha katika nia yetu ya kufika mahali fulani kwenye maendeleo, haikubaliki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, na-declare interest, nilikuwa Kamishna wa External Finance pale Wizara ya Fedha, nimefanya kazi kwa muda mrefu sana. Mahusiano ni muhimu lakini mahusiano hayo yana heshima ya nchi na nchi. Inapofika mahali dharau inaoneshwa namna hii ni juu ya Serikali kuonesha kwamba mwenendo huo hatukuupenda katika mahusiano yetu. Kwa hiyo, nawaomba sana Serikali hebu tusiwe wanyonge hivyo, dalili ninazoziona ni kwamba kuna unyonge unyonge hivi, ndiyo maana tunachezewa hivyo, ndiyo maana barabara nyingine sasa zimeachwa kwa sababu tu wafadhili fulani hawakutoa pesa ambazo waliahidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.