Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie machache kuhusu Wizara hii. Kwanza, niungane na Wabunge wenzangu, nakupongeza sana wewe binafsi na endelea na msimamo huo. Mimi nimo Bungeni humu sasa ni kipindi cha tano, Bunge ni mhimili, lazima uheshimike, Bunge si mkutano wa hadhara, siyo lazima kila hoja inakotoka kule, kwa mfano kuna tukio limetokea Mpwapwa sasa tuahirishe Bunge tujadili mambo ya Mpwapwa, sijawahi kuona kitu kama hicho mimi. Kwa hiyo, mimi nakuomba endelea asubuhi unakuja, jioni unakuja waendelee kutoka tu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Waziri wa Fedha, Naibu Waziri wa Fedha, Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri wanayoifanya.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nianze na TRA. Niwapongeze TRA wanafanya kazi nzuri sana ya kukusanya mapato lakini jiulize, kazi ya sisi Wabunge hapa ni kupitisha bajeti ya Serikali na tukishapitisha bajeti fedha zinagawanywa Wizara, Mikoa na Wilaya na mradi ukishapangiwa bajeti, kama ni barabara basi fedha yote ipelekwe. Nashangaa kwamba fedha zinapangwa, Bunge linapitisha bajeti lakini utakuta mwisho wa mwaka wa fedha karibu nusu ya fedha hazijaenda kwenye miradi.
Kwa hiyo, hii inatusababishia kuwa na viporo na vingi miradi mingi haikamiliki. Mheshimiwa Waziri hebu anieleze anayezuia/anayekata hizi fedha kule Hazina ni nani? Kwa sababu wenye madaraka ya kupitisha bajeti ni Wabunge, hakuna mtu mwingine ambaye anaweza kupunguza hizi fedha kwa ajili ya kazi nyingine. Kwa hiyo, naomba sana tukishapitisha bajeti basi Wilaya, Mikoa ipelekewe fedha zile ambazo Bunge limepitisha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, nizungumzie kidogo Mfuko wa Mahakama, hili Fungu 40. Mahakama wanafanya kazi katika mazingira magumu sana hasa Mahakama za chini, tuna upungufu mkubwa sana wa mahakimu na wa mahakama. Kwa mfano, Wilaya ya Mpwapwa ina Mahakama za Mwanzo tatu tu na Kata ziko 33, kwa hiyo, wananchi wanasafiri mwendo wa kilometa zaidi ya 60-70 kufuata mahakama. Pamoja na ufinyu wa bajeti, naomba Serikali itenge fungu la kutosha kwa ajili ya kujenga Mahakama za Mwanzo na kuendelea kufundisha Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo. Tuna chuo chetu kile cha Lushoto, hebu tuongeze idadi ya wanafunzi. Nimekitembelea kile chuo mwaka juzi, mazingira yake hayaridhishi, tuongeze majengo ili wanafunzi wawe wengi tuweze kupata Mahakimu wengi wa Mahakama za Mwanzo.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niongelee jengo langu la Mahakama ya Mpwapwa. Nashukuru sana lile jengo la Mahakama ya Wilaya ya Mpwapwa ni jipya lakini halijakamilika bado. Hosteli ya Majaji hakuna, mgahawa hakuna, kama ilivyo kwenye majengo mengine mfano Kongwa. Kwa hiyo, naomba lile jengo likamilishwe ili Jaji akija asilale kwenye hoteli za kawaida, hapana, siyo vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, Fungu la 42, Mfuko wa Bunge, hapa nimeona fedha za miradi zilizotengwa ni shilingi bilioni saba na Wabunge wengi hawana Ofisi. Sasa labda nipate maelezo Mheshimiwa Waziri, hizi fedha ni pamoja na kujenga Ofisi za Wabunge au kwa shughuli zingine? Kwa sababu Wabunge wanalalamika hawana ofisi na zimetengwa fedha kidogo sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Sheria za Manunuzi, sheria hii inatuumiza sana. Mimi nimewahi kuwa Mjumbe wa Bodi za aina mbalimbali, kwa mfano ukichukua shule ya sekondari ya bweni, dukani sukari unanunua shilingi 2000 au shilingi 2500 lakini mzabuni ananunua shilingi 3000 au shilingi 4000. Kwa hiyo, kwa kweli sheria hii inatuumiza sana. Hivi kuna tatizo gani kuleta huu Muswada hapa Bungeni turekebishe hii sheria? Maana kila mwaka Serikali inasema italeta, italeta kwa nini msilete, watu wanaumia, fedha nyingi za Serikali zinaishia hapa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi yangu yalikuwa ni hayo machache lakini nisisitize sana ujenzi wa Mahakama hususani Mahakama za Mwanzo na kuongeza mafunzo ya Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo ili waweze kusambazwa kwenye Mahakama za Mwanzo. Nakushukuru na naunga mkono hoja hii lakini narudia tena uendelee na msimamo wako huo huo, asubuhi na mchana uwepo waendelee kutoka.