Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa lakini vilevile na mimi naomba niungane na wenzangu kukutia moyo kwa kazi nzuri unayoifanya humu ndani. Umekuwa unasimamia vizuri Kanuni tulizojiwekea wenyewe Bungeni, umekuwa una misimamo mizuri ya kuhakikisha kuwa kazi za Bunge zinafanyika vizuri. Wale wanaokulalamikia ni kwa sababu wanataka kufanya kazi wanavyotaka wao wakati wakijua kabisa wana wajibu wa kutumikia wananchi. Sisi tuko nyuma yako, usitetereke wala usife moyo, kaza buti na kazi iendelee. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo na mimi nimpongeze Waziri wa Fedha na Mipango pamoja na Naibu Waziri na Maafisa wake wote kwa hotuba nzuri iliyosheheni maelekezo mazuri sana lakini naomba nichangie machache. Kwanza kabisa, nataka kuzungumzia suala la Msajili wa Hazina. Naipongeza Serikali kwa kuitenganisha hii taasisi ikawa ya kujitegemea ili iweze kufanya kazi zake kwa ufanisi mzuri zaidi. Nataka vilevile kuzungumzia kuwa Msajili wa Hazina sheria yake yeye na sheria za yale mashirika ambayo anayasimamia huenda kutakuwa na haja ya kuzipitia kuona kama kuna kusigana kwa aina yoyote.
Vilevile kazi ya Msajili wa Hazina ni kuhakikisha kuwa anasimamia vizuri uwekezaji wa Serikali katika mashirika mbalimbali. Katika kufanya hivyo anawajibika kuhakikisha kuwa haya mashirika yanaleta tija kwa Serikali na kwa nchi kwa ujumla. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na zoezi la muda mrefu kuangalia jinsi gani mashirika haya yamekuwa yaki-perform ili kuona kama yameshindwa kufanya kazi ambazo zililengwa tangu mwanzo basi itafutwe njia nyingine ya kuyamiliki au kuyaondoa kabisa. Kwa hiyo, hatutegemei mpaka sasa kuendelea kubeba mashirika ambayo ni mzigo. Tunataka kuona vilevile kuna uratibu fulani unafanywa kwa mashirika ambayo yalianza miaka mingi iliyopita na kwa wakati ule pengine yalionekana yanahitajika lakini sasa hivi kufuatana na maendeleo ambayo yamejitokeza katika uchumi duniani na nchini kwetu labda hayana tena umuhimu huo au yanafanya shughuli ambazo zinafanana basi yaunganishwe au yawe harmonized kwa njia ambayo italeta tija kwa Taifa, badala ya kuwa na mashirika ya umma mengi yanatulia fedha tu katika gharama za uendeshaji lakini faida yake kubwa haionekani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumzia mashirika ambayo mengine yalikuwa ni ya research mbalimbali. Mengi yanafanana katika utendaji wao basi hebu tuyapitie tuangalie kama yanahitajika basi yaendelee kuwepo, la sivyo, tuyavunje na tuyaweke katika mfumo ambao utaleta tija na zile sheria ambazo zilikuwa zimeunda mashirika yale zinaweza zikapitiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka kuipongeza Serikali hasa kwa kupitia Msajili wa Hazina kwa kuongeza mapato hasa ile asilimia 15 ya ule mfumo wa kuratibu mapato yanayotokana na mawasiliano, lakini vilevile zile hisa zetu kwa TCC na TBL. Napenda kuwahamasisha kuwa wapanue wigo wa taasisi ambazo Serikali itawekeza tupate mapato zaidi. Mwenyekiti wa Kamati yangu alipokuwa akiwasilisha hapa amezungumzia kupanua wigo wa uwekezaji au hisa katika mashirika ya gesi, madini hata hayo hayo makampuni ya mawasiliano tungepaswa kuwa na hisa humo ndani. Mwelekeo uwe kuwa tunapoendelea sasa kila mwekezaji anayekuja hapa nchini Serikali au wananchi wa Tanzania wawe na hisa ndani ya kampuni hizo. Hii ndiyo njia pekee itakayowezesha kuwafanya Watanzania wengi zaidi kushiriki katika uchumi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie suala zima la Sheria ya Manunuzi. Hatujafika kwenye vifungu lakini naomba niseme kabisa na naomba na Wabunge wenzangu mniunge mkono tushike shilingi ya Waziri leo mpaka atakapotuambia lini Sheria ya Manunuzi italetwa hapa Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tumeongeza fedha nyingi sana za mfuko wa maendeleo kwa hiyo fedha nyingi sana ya miradi itakwenda Majimboni, Wilayani na Mikoani, itasimamiwa vipi kama Sheria mbovu kama hii ya Manunuzi bado ipo? Sielewi kwa nini miaka kumi inapita sasa sheria hii inalalamikiwa kila Bunge lakini hakuna kinachofanyika. Sijui ni kwa sababu kuna watu wana maslahi nayo au ina ugumu gani wa kuileta Bungeni. Naomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu tushinikize sheria hiyo ije hata kama ni kwa udharura. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba vilevile nizungumzie suala la zile mashine za kielektroniki za kuratibu mapato pamoja na kodi. Hili jambo limetuletea mizozo mingi sana hapa Bungeni na hata kwa wananchi lakini najua tumefika mahali pazuri Serikali imekubali sasa kununua zile mashine na kuzigawa kwa wale ambao wanastahiki kuzipata. Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, naomba sasa hili jambo tusilifanyie siasa tena kwa sababu kwanza lina faida hata kwa wafanyabiashara wenyewe, lakini vilevile linatusaidia kupata mapato mengi zaidi kwa ajili ya uchumi wetu na kwa maendeleo ya nchi yetu. Naomba sasa Serikali ituambie ni lini mashine hizo zitapatikana zote kwa pamoja ili wafanyabiashara wanaohusika wazipate tuanze kupata hayo mapato. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kutakuwa na ukusanyaji mkubwa wa mapato, wigo wa ukusanyaji kodi uongezwe kwa maana ya kwenda kwenye sekta isiyokuwa rasmi. Kwa kuwa tutaanza kuwa tunapata mapato mengi kwa kupitia mashine hizi basi vilevile uangaliwe uwezekano wa kupunguza viwango vya kodi ili watu wengi zaidi wavutiwe kulipa kodi. Maana kodi inaeleweka kuwa ni mchango wa maendeleo siyo adhabu na kama siyo adhabu basi iwekwe katika kiwango ambacho wananchi wengi zaidi watahamasika kulipa kodi wakijua kabisa wananachangia maendeleo ya nchi yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuzungumzia suala la Deni la Taifa na mimi nataka kujikita sana sana kwenye suala la Eurobonds. Nchi nyingi za kiafrika kwa kupitia Wizara zao za Fedha wameingia katika kununua madeni au kupata madeni kwa kupitia Eurobond. Wame-float Eurobond na wengi sasa hivi wako matatani. Ghana sasa hivi inatafuta kukwamuliwa na IMF kwa sababu wamefika mahali ambapo sasa uchumi umegoma hali kadhalika Mozambique, Namibia, Nigeria na Uganda. Sisi pia najua tumenunua Eurobond, je, tutegemee nini huko tunakokwenda maana nyingi karibu zinaanza kuiva na tayari chumi hizo ziko matatani. Najua kwa wakati ule mwaka 2008 kulikuwa kuna haja yakufanya hivyo kwa sababu ya uchumi ulikuwa umetetereka lakini na sisi tunavyojiingiza huko ni mkumbo au sisi tumejipanga vizuri zaidi kuwa hatutakuja kuathirika na hii Eurobond huko tunakokwenda? Ningependa kupata maelezo ya Mheshimiwa Waziri atuambie tunategemea kulipa nini, kwa vipindi vipi na itatuathiri au itatuletea faida kiasi gani? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ili kupunguza deni la Taifa kwa nini tusijiingize kwenye uwekezaji wa kutumia PPP? Mpaka sasa hivi tunazungumzia sheria, sheria imeshapatikana, tayari kuna wawekezaji wengi wanaotaka kuingia kuwekeza nchi kwetu katika mtindo huo lakini Serikali bado inaonekana kama ina mashaka ndiyo kwanza tunafikiria kukopa sisi wenyewe, hii itazidisha deni na tutashindwa kuhimili. Kwa nini sasa Serikali isiamue kujiingiza katika uwekezaji mkubwa kwa kupitia PPP? Nchi nyingi na wawekezaji wengi wana interest, wanatufuata hata sisi kuja kutuambia.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwa nini Serikali haifanyi biashara na taasisi zake yenyewe? Tunalalamikia TTCL lakini Serikali haiwapi biashara. Maofisi mangapi wana land line za kutosheleza ukilinganisha na simu za mkononi ambapo maafisa wao wote wanazo mikononi, mbili mbili au tatu tatu. Uchumi wetu utakuaje kama hatufanyi biashara na taasisi zetu wenyewe? Tunazungumzia mabenki, ni kiasi gani fedha ya Serikali iko kwenye mabenki ambayo sio ya Taifa ukilinganisha na yale ya kizalendo? Sisi wenyewe tunaanzisha taasisi halafu tunazikimbia, tunazikimbia zitafanya biashara na nani? Lazima tufanye biashara na taasisi zetu wenyewe. Nataka Serikali iweke mkakati na ije na agizo kabisa kuwa taasisi zake zote zitafanya kazi na Serikali, Serikali itakuwa mdau wa kwanza kwa taasisi za Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana.