Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Dr. Augustine Philip Mahiga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti naomba nichukue nafasi hii ya kuhitimisha mjadala huu wa hoja yangu kwa kutoa shukrani za pekee kwa Wabunge wote wa Bunge hili Tukufu kwa mchango wenu wa mawazo, kwa maandishi, lakini pia naamini kabisa kwamba Wizara yangu itaendelea kutegemea mawazo ya ujumla ya Bunge hili katika kutekeleza Sera zake na mipango yake ya kuendeleza uhusiano na nchi za nje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa shukrani za pekee kwa Naibu Waziri wangu ambaye amemaliza tu kujibu baadhi ya maswali. Pia natoa shukrani za pekee kwa wafanyakazi katika Wizara yangu, Wakurugenzi, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu na wengine wote ambao tumeshirikiana katika kuandaa hotuba hii na kujibu maswali ambayo yamejitokeza ndani ya Bunge hili Tukufu
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru mke wangu Elizabeth Mahiga ambaye amekaa pale, ameniunga mkono na ameendelea kunifariji katika utendaji wangu wa kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kujibu maswali yote moja baada ya lingine lakini mengi ya maswali haya tutayajibu kwa maandishi. Nataka kusema yale ambayo ni ya msingi kuhusu Wizara hii ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni suala zima la Diplomacy ya jumla ya Tanzania, halafu nitakuja kuzungumzia Diplomacy ya uchumi. (Makofi)
Mheshimiwa MWenyekiti, Diplomacy ya Tanzania ni urithi na tunu ya pekee kabisa katika Afrika; lazima tuienzi, tuidumishe na tuilinde. Ni kati ya vitu ambavyo tumerithi tangu kwa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na viongozi wengine katika Awamu mbalimbali. Bara la Afrika na dunia inatambua hivyo. Nawaomba mkipata fursa mtembelee katika majukwaa ya Kimataifa. Kuna mikutano mingine haiwezi kuanza kama Tanzania haipo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania inapotoa hotuba inasikilizwa na ulimwengu. Kama watu walikuwa wametoka kunywa chai katika mikutano ya Kimataifa, Tanzania inapoanza kuzungumza waliokuwa wanavuta sigara na kunywa chai wanarudi kwenye ukumbi. Hii ni baadhi tu ya heshima ambayo tunaipata Kimataifa na hapa katika Bara la Afrika na kwa kweli ni kitu ambacho lazima tujivunie na ni jukumu letu; na hakuna mahali pa kuenzi diplomasia ya Tanzania kama ndani ya Bunge hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa diplomasia yetu imekua na ni sahihi kabisa kwamba sasa lazima tujikite kwenye diplomasia ya kiuchumi. Diplomasia ya kiuchumi maana yake nini? Ni kweli tumekuwa na kama wimbo tunasema, diplomasia ya kiuchumi lakini ukimuuliza mtu maana yake nini na ukitoa kauli kwamba Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje haijatekeleza diplomasia ya kiuchumi si sahihi hata kidogo! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hutakuta viwanda kwenye Wizara yangu, hutakuta madini kwenye Wizara yangu, hutakuta mazao ya biashara kwenye Wizara yangu, lakini Wizara yangu ndiyo inayowezesha Wizara zote ziweze kuungana na ulimwengu katika kutekeleza Sera zao tofauti. Msione vinaelea, vimeundwa! Muundaji ni Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ndiyo inayofungua milango na madirisha ya mahusiano kati ya Serikali, sekta binafsi na Mashirika Yasiyo ya Serikali. Wizara hii ndiyo inayoratibu shughuli zote hizo. Kwa hivyo katika Economic Diplomacy Wizara inatakiwa kuleta mawasiliano kati ya Serikali nyingine, viwanda na Mashirika mengine. Kwa hivyo Economic Diplomacy ni kitu ambacho lazima kifuatiliwe kwa karibu na isiwe ni kitu cha mpito.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima pia tuelewe na tufafanue na tuelewane, kwamba katika Economic Diplomacy unatengeneza framework ambayo itakuonesha dira ya wewe kama nchi kuhusiana na nchi nyingine na kama kuweka kitega uchumi ili uinufaishe nchi yako. Wizara ya Mambo ya Nje ndiyo inayofungua mlango halafu inaendelea kuratibu, hiyo ni kazi moja (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya pili ya Economic Diplomacy ni pale ambapo Tanzania inakwenda katika majukwaa ya Kimataifa na mahali kama pale unazungumza sio peke yako na wenzako. Kama ni suala la biashara, viwanda, au uwekezaji, vitu hivyo utavipata katika jukwaa na mtu wako anayekwenda pale kwenye jukwaa awe na uwezo wa kusema, kutetea na awe na uwezo wa kuwaletea nyumbani vitu kama hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa pia kuwahakikishia Wabunge kwamba diplomasia yetu hasa ya uchumi imejikita katika mambo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi Tanzania inahesabika kama nchi ambayo uchumi wake unakua haraka kuliko nchi nyingine za Afrika, kwa asilimia saba. Sasa kama Tanzania inakua hivyo, hicho ndiyo kipimo cha Economic Diplomacy. Katika Afrika ya Mashariki, Tanzania ni ya kwanza katika uwekezaji ndani ya Afrika Mashariki lakini pia kutoka nje. Hivyo ndiyo vipimo vya Economic Diplomacy.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kwa kifupi tu kuwaonesha baadhi ya masuala muhimu ya Economic Diplomacy ambayo tumeyavuna hivi karibuni.
Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji ni mfano tu! Uwekezaji wa kiwanda cha cement cha Dangote. Uwekezaji ulioifanya Uchina ichague Tanzania kuwa moja ya nchi nne muhimu za uwekezaji. Wachina wenyewe wamesema, Balozi wenu pale Beijing ndiye aliyewashawishi vya kutosha kwamba Tanzania iwe moja ya nchi ambazo zitapewa kipaumbele katika uwekezaji wa viwanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipotoa hotuba yangu jana nimesema; sisi tutajikita kwenye diplomasia ya viwanda. Yaani hiyo diplomasia ya uchumi naipandisha safu. Tutajikita sasa kama Wizara kwenye diplomasia ya kushawishi na kuleta viwanda. Vile vile katika hotuba ile ile nimesema kukuza diplomasia ya viwanda haifiki popote peke yake, lazima iende sambamba na diplomasia ya kilimo kwa sababu hivi viwanda vitategemea kilimo. Lazima iende sambamba na diplomasia ya miundombinu kwasababu hivi viwanda vitahitaji umeme na uchukuaji na usafirishaji. Kwahivyo naweza kuwaelezeni ile safu ya Economic Diplomacy baada ya kuieleza kwamba ni ya pamoja na ya katika majukwaa sasa inapandishwa grade na Wizara yangu na itaitwa Economic Diplomacy of Industries. (Makofi) 0714197930
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini utekelezaji wake utakuwaje? Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli amesema; katika Wizara yako punguza watu na napunguza watu, nimepunguza wengi. Hata hivyo, anasema; unapopunguza hawa watu lazima upange na kupangua watu wako. Si tu kuwapeleka kwenye embassies, kwamba sasa mimi ni zamu yangu – posting, hapana! Nani aende wapi na kule aliko awe na nani?
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Economic Diplomacy si tu ya Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje, lazima tushirikiane na Wizara nyingine huko nje kama Utalii, Viwanda na Wizara nyingine ambazo zinahitaji wawekezaji lakini wanahitaji ushawishi wa pekee. Kwa hivyo, kutakuwa na kupanga na kupangua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia chuo chetu cha kule kurasini kitatoa mafunzo maalum ambayo yanaitwa The Economics of Economic Diplomacy. Lakini pia Economic Diplomacy tutaieneza na tutaifuata si tu kwa sababu ya mafunzo lakini pia ndani ya idara yetu tutatengeneza kitu kinaitwa Economic Unit ambayo itakuwa ni unit of economic intelligence na ambacho kitakuwa ni mtambuka, uchumi mtambuka wa sehemu zote za aina hiyo. Hiyo ndiyo aina ya diplomacy ambayo tunataka kuieneza, kuitetea na kuishuhudia katika Wizara yetu ya Mambo ya Nchi za Nje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia nirudie tena lile suala la diaspora. Katika diaspora huwezi kuzungumzia diaspora bila kuitengenezea profile yake, nani yuko wapi na nani anafanya nini? Kuna Watanzania ambao ni wanafunzi, kuna Watanzania ambao ni wataalam wanafanya kazi zao huko, kuna Watanzania ambao ni wazamiaji; lazima tukubali hilo na kuna Watanzania kama nilivyosema ambao wako kwenye majela.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni jukumu letu na tumeanzisha idara maalum katika Wizara yangu inayoitwa Idara ya diaspora. Tunashirikiana na wenzetu walio huko nje na pia na Serikali nyingine ili tuweze kuwatambua Watanzania wetu. Kuna wengine wanasema siji kwenye Ubalozi nitakamatwa, lakini hao hatimaye wanakuja wakipata shida na sisi tuko tayari kuwapokea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunaweka mkakati maalum si tu kuwatambua lakini katika diaspora kuna wale wenye ujuzi wa pekee na wako tayari kuja huku nyumbani ama kwa miezi sita au mwaka mmoja wafanye kazi katika Wizara mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili nilizungumzie tena suala la uraia pacha au utaratibu mwingine wa kuwawezesha Watanzania walio nje washiriki katika mchakato wa uchumi. Hawa Watanzania walio nje ni wabunifu kweli kweli, wamekuwa na makongamano ya aina mbalimbali, mengine ya utalii, mengine uwekezaji, mengine ni ya kusaidiana tu kama jamii na lazima tuwaelewe zaidi ili tuweze kuwasaidia vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitafurahi kama ninyi wenyewe kwa umoja wenu au mmoja mmoja mnaweza kutupatia taarifa. Juzi hapa kuna Mbunge kutoka Upinzani amenifuata, anasema Balozi, sijui Waziri/Balozi; nina ndugu yangu alikamatwa na madawa, akatiwa ndani Nigeria, sasa amefunguliwa na lazima arudi nyumbani, Je, Wizara yako inaweza kutusaidia? Mara moja nilichukua hatua za kumrudisha yule kijana na juzi nimepata barua kutoka familia yake wanasema Waziri tunakushukuru. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tukumbushane kwamba hili suala la diaspora tumelizungumza mara kwa mara, lakini nina hakika tutafika mahali ambapo itabidi tukubaliane kwamba hawa diaspora wawe ni sehemu gani ya Watanzania walioko huko nje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa sasa kuzungumzia suala la Mheshimiwa Rais, Dkt John Pombe Magufuli, kwamba haendi nje. Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli ana sababu za kutokwenda nje, kwa sababu kuna mambo ambayo lazima afanye hapa nyumbani na wakati ule alikuwa anafanya uteuzi na kukamilisha Serikali yake. Hata hivyo, ningependa kuwaambia kama wengi hamjui, mimi kama Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje siwezi kwenda popote bila kutumwa na Mheshimiwa Rais! Kila ninakokwenda napata ridhaa ya Mheshimiwa Rais na maagizo ya Rais.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia huyu Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli amekuwa mkarimu sana kukutana na Mabalozi. Siwezi kusoma orodha yote hapa lakini amekutana na kila Balozi aliyepo Tanzania ambaye anataka kukutana naye na mazungumzo yanakuwa mazuri tu na baada ya hapo yanafuata maagizo ambayo mimi kama Waziri mwenye ridhaa nayatekeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hili nimwongeze pia Waziri wetu Mkuu. Juzi hapa nimesafiri naye, katika kile kipindi cha siku mbili cha kufanya kazi ameweza kuwashawishi wawekezaji wengi tu! Wengine wakiwa wamekubali kuleta kiwanda kizima cha matrekta hapa Tanzania. Kampuni ya Shell ambayo ndiyo mwekezaji mkuu kwenye gas yetu walikuwa wanasuasua, Waziri Mkuu aliwaita, tukakaa, tukazungumza nao. Wakasema; haa! Sasa tunaelewana na Tanzania na gesi tutaanza kuichimba.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nizungumzie suala la mjusi. Wiki mbili zilizopita nilikuwa Ujerumani kuangalia mjusi, hapana! Nikawauliza Wajerumani kwamba jamani yule mjusi vipi. (Makofi/ Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wajerumani nao wakaniambia vipi ninyi Watanzania. Nikawaambia kwa nini anasema kwa muda mrefu sasa, kumekuwa na Watanzania delegation after delegation inayokwenda Ujerumani kutazama mjusi. Delegation ya kwanza anasema ilikuwa na watu 19 kutoka Tanzania na ikiongozwa na National Museums, wakazungumza wakakubaliana kabisa jamani tufanye nini kuhusu huyu mjusi?. Wakawapa options anasema mnaweza kumchukua, lakini mkitaka kuchukua lazima kutafuta ndege maalum ambayo ni refrigerated na chemba nzima ambayo huyu mjusi atawekwa iwe katika temperature fulani na kila baada ya muda fulani huyu mjusi awe anapakwa vitu fulani, vinginevyo atayeyuka kama temperature ile haipo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wao wakasema lakini kama mnataka sisi tutawasaidia. Baada ya hapo yule aliyeongoza ule ujumbe nasikia alifariki. Ukaenda ujumbe mwingine safari hii wakiwa Watanzania 24 kule Ujerumani, wakaenda pale kuzungumzia mjusi, wakasema sisi sasa tunarudi nyumbani na hili tutalipeleka kwa mamlaka husika tuanze kulitekeleza. Sasa mimi juzi nimeulizwa, jamani what is the problem with you, mnakuja tunazungumza tunakubaliana mnaondoka halafu mnakwenda tunaona tena delegation nyingine inarudi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukakubaliana hivi, tukasema ninyi Wajerumani pamoja na kuwa mnatupa misaada, juzi wametupa ndege za doria kwa ajili ya magaidi, ninyi mna pesa na mna uwezo na mnaweza kutusaidia pesa kama ni kumrudisha mjusi arudi au mnaweza kutusaidia fedha za maendeleo za ziada na zile ambazo mnatupatia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wamenipa changamoto, wanasema Waziri Mahiga rudi Tanzania, usiorodheshe tu mjusi maana pale alipogunduliwa huyu mjusi, wanasema kuna mijusi mingine ambayo inaweza ikachimbwa pale. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, wakasema pamoja na kuwa sisi tulikuwa pale kama wakoloni nawaombeni mwende mkaorodheshe maeneo yote ya kihistoria na urithi ambayo yanatokana na kuwepo kwa Wajerumani ndani ya nchi yenu. Tunaamini hii itakuwa ni kivutio maalum kwa watalii kutoka Ujerumani. Wakasema siyo mjusi tu, siyo liemba, siyo barabara ya Bismarck tu, bali ni shule, ni mahospitali hata maeneo mbalimbali ambayo yanatuunganisha sisi na Ujerumani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata taarifa kwamba pamoja na kuwa Wajerumani walirudisha fuvu la Mtwa Mkwawa, mwaka 1954 kumbe nasikia kuna mafuvu na mabaki ya Watanzania wengi tu kwenye museum zoo. Hii ni mojawapo ya maeneo ambayo tunaweza kwenda kuzungumza nao. Ukweli ni kwamba, wao wako tayari tukiongozana, tukishirikiana nao, kwamba tuweze kuhamasisha misaada ambayo italeta tija kwa Tanzania ambayo inatokana na kuwepo kwa Wajerumani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili la mjusi kwa kweli nadhani ni suala muhimu sana na lazima tulishughulikie. Nilipokutana na Deputy Minister wa Ujerumani, huyu ndiye alitoa ahadi kwamba maeneo alikotoka yule mjusi kuna barabara ambazo zinahitaji kujengwa. Ameeleza pia kwamba kuna maeneo ambayo Wajerumani waliishi, kuna barabara inaitwa sijui Bismarck road, nyingine inaitwa sijui Bismarck rock, sijui nyingine Bismarck nini; vyote hivi vinaashiria uhusiano fulani kati ya Wajerumani na Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wajerumani wamesema hiyo timu iundwe, tuanze kutazama vile vitu ambavyo Serikali ya Ujerumani inaweza ikagharamia na inaweza ikafanya ni sehemu ya urithi wa historia kati ya Tanzania na Ujerumani, hilo wametoa kabisa kama blank cheque na sasa changamoto ni kwetu na nimeahidi kwamba hilo nitalifuatilia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Ujerumani inasema hakuna nchi ambayo kihistoria Afrika tuko karibu kama Tanzania, pamoja na tofauti zetu ambazo zimejitokeza hapa katikati nadhani suala la mjusi ni moja tu kati ya yale ambayo tunaweza kunufaika kutokana na uhusiano wetu na Ujerumani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa pia kuzungumzia juu ya majirani. Tulipokuwa Uingereza juzi na Waziri Mkuu, msaidizi wa John Kerry, Minister of Foreign Affairs au Minister of State wa Marekani, ambaye ni namba two wake aliomba kukutana na sisi na Waziri Mkuu. Wakasema Marekani inaamini kabisa kwamba katika ukanda wa maziwa makuu au hata katika Afrika, nchi ambayo inaweza ikazungumza na Kongo na ikasikilizwa ni Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, tunaombeni Watanzania mjenge uhusiano wa karibu na Kongo na pia muisaidie Kongo, kuwa na mtangamano wa kisiasa. Suala la kuanzisha Ubalozi mdogo Lubumbashi ni la siku nyingi sana. Sasa hivi, tunaitisha kikao kinachoitwa Joint Permanent Commission kati ya Tanzania na Kongo, kwa sababu inaelekea kwamba wanaweza kuanza kutafuta njia nyingine za kupitishia bidhaa zao. Tukiitisha kikao kile, tutazungumzia suala la consulate ya pale Lubumbashi lakini pia…
MWENYEKITI: Mheshimiwa naomba umalizie
WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tutazungumzia masuala mengine ya uhusiano na hawa majirani zetu. Siwezi kuzungumza juu ya Burundi kwa sababu inajulikana lakini, ni kwamba nchi yetu imekuwa ikipokea wakimbizi. Hata kabla ya uhuru, wakimbizi wa kwanza kuja Tanzania ilikuwa mwaka 1959 walitoka Rwanda, hata uhuru hatujapata. Kwa hivyo, tuna jukumu la pekee na Jumuiya ya Mataifa nimewaambia lazima mtusaidie na lile suala la mazingira bora na mengineyo yashughulikiwe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa shukrani na nitaendelea kuzungumza nanyi, Upinzani nawashukuruni sana, Ndugu yangu Msigwa, tutazungumza mengi, tutasaidiana, tutabadilishana mawazo na tuendelee kuwa karibu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapa, nadhani kuna kutoa hoja. Kutoa hoja baada ya Kamati ya Matumizi kupitisha vifungu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa hoja