Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. JANETH Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa ya kuchangia katika Hotuba ya Wizara hii ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Nachukua fursa hii vile vile kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Balozi Dkt. Augustine Philip Mahiga, Naibu Waziri Dkt. Suzan Kolimba, Katibu Mkuu na watendaji wote kwa hotuba nzuri na taarifa nyingi za muhimu kwetu sisi juu ya utendaji wa Wizara hii muhimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua umuhimu wa vituo vya utoaji huduma mipakani hasa katika kurahisisha taratibu za uhamiaji, forodha, ukaguzi wa ubora wa bidhaa, usalama na ulinzi. Dhana hii na angalau vituo hivi kule vilikowekwa kwenye mipaka yetu kama Holili, Taveta, Horohoro, Tunduma na Sirari, Kyaka, Rusumo na kadhalika vimeleta matokeo mazuri sana katika maeneo yote tajwa hapo juu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Ileje ina kituo muhimu sana kwenye Mto Songwe ambako tunapakana na Malawi kwenye Jimbo la Chitipa. Hata hivyo, inasikitisha kuwa ni miaka 42 tangu Wilaya ya Ileje ianzishwe lakini hakuna jengo, kituo wala miundombinu yoyote inayofaa kwa matumizi ya Serikali kuhakikisha kuwa biashara kubwa inayofanywa kati ya Watanzania na Wamalawi inasimamiwa vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile soko lililoko Isongole, mita 100 tu kutoka mpakani, ni dogo kwa mahitaji ya biashara inayoendelea kati ya nchi hizi mbili.
Kwa bahati mbaya soko hilo limegeuzwa kuwa ghala la kuhifadhia mahindi na NFRA, hivyo hali hii imefanya lisitoshe kukidhi haja ya soko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Wizara chini ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki kujenga kituo cha pamoja mpakani na Malawi, pale Isongole ili huduma ziboreshwe maana tayari upande wa Malawi (Chitipa) wana miundo mizuri sana na wanatusubiri sisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukosefu wa miundombinu ya kituo hiki umesababisha wahamiaji haramu kutumia mpaka huu kuingia nchini na kutoka nchini kwenda nchi jirani. Silaha zimekuwa zikipitishwa katika mpaka huu huu na hivi sasa pombe haramu ya viroba ambayo imepigwa marufuku Malawi huingia kwa wingi nchini Tanzania kupitia mpaka huu, na vile vile kujikosesha fursa mbalimbali kwa Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kukosekana kwa kituo hiki cha pamoja na huduma zote muhimu vile vile kunahatarisha usalama na ulinzi wa Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naitaka Wizara itoe tamko ni lini Kituo hiki cha Pamoja cha Forodha kitajengwa pamoja na kuweka taasisi zote muhimu ili Ileje na Taifa zima liweze kufaidika. Kituo hiki kitafanya biashara iongezeke ndani ya Wilaya na hata fursa za uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawasilisha na naunga mkono hoja.