Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali katika Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia Mpango uliopo mezani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya nami nikaweza kusimama katika Bunge hili Tukufu kuchangia hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuwashukuru sana wapigakura wangu, vijana wa Kigoma; nakishukuru Chama changu kupitia Jumuiya yake ya Umoja wa Vijana na Jumuiya ya Umoja wa Wanawake kwa kunipa ridhaa mpaka leo hii nikaweza kuwa mwakilishi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuchukua fursa hii kumpongeza Rais wetu wa Awamu ya Tano, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa anayoifanya hasa katika kupunguza matumizi ya Serikali. Sisi kama vijana tunasema tutamuunga mkono, tutakuwa bega kwa bega na yeye kuhakikisha tunatetea maslahi ya Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kutoa pongeza za dhati kwa Mawaziri wakiongozwa na Waziri Mkuu kwa kuteuliwa kuwa katika Baraza la Mawaziri kuunda Serikali ya Awamu ya Tano. Sisi kama vijana, tuna imani kwamba mambo makubwa yatafanyika katika Awamu ya Tano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile napenda kumpongeza Waziri wa Fedha kwa kuwasilisha Mpango huu lakini pia nawapongeza Wabunge kwa michango yao ya kuboresha Mpango huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, kwa mujibu wa takwimu za idadi ya watu Tanzania, uwiano unaonyesha kwamba kundi la vijana linachukua asilimia kubwa zaidi. Kwa hiyo, mimi kama mwakilishi kwa vijana ningependa kujikita na kujielekeza kuzungumzia masuala ya vijana na hasa kuishauri Serikali yangu kwamba ili kuleta maendeleo katika Taifa hili, kundi hili maalum ni lazima tujue na Serikali ijue inalifanyia nini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Tano imejielekeza na imeweka msisitizo, kuhakikisha kwamba changamoto kubwa sana ya vijana ambayo ni ukosefu wa ajira inapata utatuzi. Katika kuleta utatuzi wa changamoto hii ya ajira inashindikana kusema kwamba hatuzungumzii ni jinsi gani sekta ya elimu inaboreshwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya elimu ni sekta ambayo Serikali imejitahidi kufanya mambo makubwa sana na tunawapongeza kwa kazi hiyo. Hata katika Mpango wetu katika ukurasa wa 28 wamezungumzia na wameelezea ni jinsi gani Serikali imejipanga kuboresha elimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sana kuishauri Serikali katika mikopo ya wanafunzi waliodahiliwa kusoma katika Vyuo mbali mbali waweze kupatiwa mikopo yao kwa wakati. Kumekuwa na changamoto kubwa sana ya vijana hawa kukosa mikopo yao kwa wakati. Ukosefu wa mikopo yao kwa wakati unachangia hata kubadilisha mienendo yao na unaathiri hata matokeo yao ya kielimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kusema kweli Serikali imefanya mambo makubwa katika sekta ya elimu na ninapenda kutoa pongezi za dhati na hasa katika maamuzi yake ya kubadili mfumo wa kupanga ufaulu wa wanafunzi kutoka katika ule mfumo uliokuwa wa GPA na sasa hivi wameweka mfumo wa division. Mfumo huu wa division sisi kama vijana tunaupongeza kwa sababu tunauelewa zaidi na hata wazazi wanaelewa zaidi na wanaweza kupima ufaulu wa vijana wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya elimu pia napenda kuishauri Serikali kuboresha mitaala ya elimu. Kwa sababu tunasema kwamba tunataka kuwasaidia vijana ambao wanapata changamoto kubwa sana ya ajira, kwa hiyo, mitaala yetu ya elimu lazima ioneshe ni kwa jinsi gani inamwandaa huyu kijana kuweza kujiajiri yeye mwenyewe, hasa tukiangalia na tukijua kwamba hamna ajira za kutosha kwenye Serikali na hata taasisi binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunahitaji kuwa na mitaala ambayo itaweka msisitizo katika taaluma lakini mitaala hiyo iweke msisitizo katika stadi za kazi. Kwa kuzungumzia stadi za kazi, hapa nitazungumzia vile vyuo vya kati ambavyo vinatoa mafunzo kama ya ufundi, vyuo kama Dar es Salaam Institute of Technology na VETA. Vyuo hivi viweze kuongezewa uwezo ili vidahili vijana wengi zaidi ambao watapata mafunzo ambayo yatawawezesha kujiajiri wao wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya michezo na sanaa ni sekta ambayo inatoa ajira kubwa sana kwa vijana; sio tu vijana lakini kwa Taifa duniani kote. Kwa hiyo, napenda kuishauri Serikali yangu iweke msisistizo na kuwezesha michezo na sanaa kuwekwa katika mitaala yetu ya elimu ili kuibua na kuendeleza vipaji ambavyo vijana wetu wanakua navyo. Ina maana vipaji hivi na sanaa hizi zikifundishwa kwa vijana wetu wanaweza kupata fursa ya kujiajiri wao wenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Taifa hili wako akina Diamond wengi wa kutosha; wako akina Mbwana Samatta wa kutosha; lakini ni kuboresha tu mitaala yetu ili katika mitaala ile ya elimu zipangwe ratiba za kufundisha vijana, michezo, lakini pia kuwa na mafunzo ya sanaa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala zima la ajira kwa vijana, nitakuwa sijatenda haki kama nisipozungumzia miundombinu wezeshi.
Napenda kuunga mkono michango ya Waheshimiwa waliotangulia waliosisitiza kwamba Serikali itengeneze mpango wa kujenga reli ya kati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari ya Dar es Salaam haiwezi kukamilika pasipo reli ya kati; Bandari ya Kigoma haiwezi kukamilika pasipo reli ya kati. Kimsingi, reli ya kati itapanua sekta nyingi za uchumi na itanufaisha siyo tu Mikoa ya jirani, lakini itaongeza uchumi wa nchi kwa sababu itafungua milango ya biashara na nchi jirani.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mengi ya kuchangia…
MWENYEKITI: Ahsante sana.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.