Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kunipa nafasi hii ya kuchangia hoja ya Waziri wa Fedha na niungane na Waheshimiwa Wabunge waliotangulia kukupongeza sana kwa kazi nzuri unayoifanya, tunakutakia kila la heri na mafanikio, najua kiti kizito, lakini kimepata mwenyewe, hongera sana na tunakutakia kila la heri.(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua fursa hii kumpongeza Waziri wa Fedha kwa hotuba na bajeti nzuri na ni mategemeo yangu kwamba chini ya uongozi wake tutapata utekelezaji unaofanana na hotuba yenyewe.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua nafasi hii kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kukamilisha mradi wa mabasi yaendayo kwa kasi na kuuzindua vizuri na kuwapa wananchi fursa ya kuweza kuuzindua mradi huo kwa siku kadhaa bila ya malipo yoyote. Kwa kweli mradi huu ni mradi mkombozi, utakaowawezesha wananchi wetu kupiga hatua za maendeleo, unawaondoshea adha ya usafiri, lakini mradi huu pia unawapunguzia muda mwingi ambao walikuwa wanaupoteza kwa ajili ya kusafiri na badala yake muda huo sasa watautumia kwa ajili ya kuzalisha mali na bila shaka tutapiga hatua kubwa zaidi ya kimaendeleo kwa sababu ya uwezo huu mkubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali, wakati inaendelea katika kusimamia mradi huu ihakikishe kwamba inashughulikia changamoto zilizobaki ili mradi huu uwe na mafanikio zaidi. Serikali iweze kununua mabasi yale 140 mengine ambayo yanahitajika zaidi katika mradi huu, lakini pia kukamilisha jengo la kuwawezesha watumishi wale waweze kufanya kazi vizuri na mradi uweze kuwa na mafanikio. Mradi ni mzuri na uwekezaji huu ni wa mfano katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kuchangia pia katika kuipa pongeze Serikali katika kuthubutu, uthubutu wenyewe ni katika ujenzi wa reli ya kati kwa ngazi ya standard gauge, huu ni uthubutu mkubwa. Gharama ni kubwa sana lakini Serikali imeamua kuwekeza pale karibu trilioni moja katika gharama ya dola bilioni saba ili ionyeshe nia thabiti ya kutaka kujenga Reli ya Kati. Serikali ya Awamu ya Tano katika hili inaandika historia kwa sababu jambo hili litasukuma maendeleo ya nchi yetu kwa kiasi kikubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, reli ya kati hivi sasa ina takribani miaka 100 sasa, kwa hiyo vizazi vingi vijavyo vitakuja kuikumbuka Serikali ya Awamu ya Tano kwa uamuzi huu adhimu wa ujenzi wa reli ya kati kwa standard gauge. Reli hii ya Kati kwa mawazo ya awamu iliyopita ni reli yenye uwezo mkubwa, treni yake ni ya kilometa mbili yenye uwezo wa kuendesha speed 120 kwa treni ya abiria na speed ya kilometa 80 kwa saa kwa treni ya mizigo na wagon ambazo zinabeba makontena mawili mawili, ni kontena moja juu ya lingine, kwa hiyo huu ni uwekezaji mkubwa sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye dola bilioni saba za uwekezaji ambazo zimetajwa hapa ambazo sawasawa na takribani shilingi bilioni 15, bila shaka tutahitaji wabia wenye nguvu, wenye uwezo ili waweze kushirikiana na Serikali yetu. Ile shilingi trilioni moja ambayo imewekwa pale ya shilingi katika shilingi trilioni 15 haiwezi ikajenga treni hii, kwa hiyo naiomba Serikali yetu iweke mkazo mkubwa kwa kupata wawekezaji wenye nguvu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2009, Serikali tatu; Rwanda, Burundi na Tanzania, iliiomba Benki ya Maendeleo ya Afrika kuwakusanya wawekezaji kwa ajili ya treni hii na mkutano ule mkubwa ulifanywa Tunis. Lakini mwaka 2009 mpaka sasa hivi 2016 ni miaka saba baadaye, hatujaweza kuijenga hii reli, kwa hiyo nina imani kwamba Serikali hii itachukua jambo hili kwa uzito zaidi ili ihakikishe wawekezaji waliojitokeza Tunis mwaka 2009 au wengine waweze kufanya kazi hii wakishirikiana na Serikali yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kusema kwamba reli kubwa kama hii mwenzake ni bandari kubwa. Kwa maana hiyo ningesema kwamba ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo ambao tayari imetengwa jumla ya ekari 2000, sasa usemwe kwa herufi kubwa na uanze ujenzi huo ili uendane sambamba na uwekezaji mkubwa wa reli ya kati kwa kiwango cha standard gauge. Bila kufanya hivyo uwekezaji huu wa reli hautakuwa na tija, tuna jukumu sisi la kutoa fursa kwa nchi zisizokuwa na bahari ili ziweze kuendesha uchumi wao kwa kutumia bahari hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Rwanda, Burundi, Kongo Mashariki nao wote watategemea sana matumizi ya bandari katika nchi yetu kwa kutumia njia hii ya reli ya standard gauge. Sasa nikisema kwamba ni wakati huu sasa ambapo tufanye juhudi kubwa, Serikali ijipambanue kuhakikisha kwamba ujenzi wa bandari unaanza mara moja na zile changamoto zote ambazo zipo ambazo zingeweza kuzuia ujenzi wa Bandari hii ya Bagamoyo mapema basi ziweze kuondolewa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu imesaini MoU kwa ajili ya ujenzi wa bandari mwezi Septemba, 2012, lakini ikasaini pia framework agreement kwa ajili ya ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo mwezi Machi, 2013. Baadaye ikasaini implementation agreement ya ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo mwezi Desemba, 2013, na hatimaye nchi tatu; Tanzania, China na Oman zimesaini mkataba wa ujenzi wa bandari hii na kuzindua ama kuweka jiwe la msingi mwezi Oktoba, 2015 na aliyeongoza uzinduzi ule ni Mheshimiwa Rais Mstaafu. Oktoba, 2015 mpaka hivi sasa ni miezi tisa, nchi za Uchina na Oman ni nchi ambazo ziko serious kabisa katika ujenzi wa bandari hii, na wenzetu wana uwezo wa kifedha na uwezo wa kitaalam.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuitumie fursa hii mapema. Miezi tisa hamna kitu ambacho ardhi hatujaigusa maana yake ni kwamba ujenzi wetu wa bandari unaweza ukaingia katika kitendawili. Muda ndiyo huu lazima tufanye kazi ya uhakika ili kuhakikisha kwamba bandari ya Bagamoyo inajengwa kwa wakati iweze kuungana na reli ya kati ya kiwango cha standard gauge kuhakikisha kwamba reli pamoja na bandari inatugeuza sisi sasa kuwa Singapore ya Africa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Pande na Mlingotini walipwe fidia zao kwa wakati walipwe ahadi zao walizopewa na Serikali za makazi mapya pamoja na kujengewa nyumba zao, bila ya kufanya hivyo tutashindwa kuanza kujenga bandari hii kwa wakati. Wananchi …
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu muda umeisha naunga mkono hoja na nakushukuru sana.