Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2015, Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017 na Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia katika bajeti hii. Nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha pamoja na Naibu Waziri wa Fedha kwa hotuba nzuri ambayo waliwasilisha hapa Bungeni kuhusiana na suala zima la uchumi na masuala ya fedha kwa ujumla.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kwa suala la umaskini. Katika hotuba hii nimeona jinsi ambavyo amezungumzia habari ya hali ya umaskini hasa katika mikoa ya Kanda ya Ziwa ambapo umezungumzia kuna Mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Kigoma na Singida. Kwa hiyo ni changamoto ambayo mimi binafsi ninaikubali kwa sababu kutokana na hali halisi ya uchumi na hali halisi ya maisha wananchi walio katika eneo hilo. Kwa hiyo, niombe sasa, nilivyokuwa nikiangalia bajeti kwa ujumla sijaweza kuona jinsi ambavyo Serikali imejipanga kuweza kufanya mabadiliko ya kiuchumi katika maeneo haya ambapo yameonekana kwamba yako nyuma sana kiuchumi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda kuishauri Serikali kwamba kwa sababu tafiti hizi zimefanyika tangu mwaka 2012; kwa hiyo, taarifa hii inajulikana kabisa kwamba mikoa hiyo iko katika hali mbaya ya kiuchumi yaani wana umaskini uliokithiri.
Kwa hiyo, naiomba Serikali sasa iwekeze nguvu katika mikoa hii ili kuweza kunusuru maisha ya wananchi, hasa kiuchumi. Ninasema hivyo kwa sababu tukiangalia wananchi katika maeneo haya wanategemea shughuli mbalimbali za kiuchumi, wanategemea kilimo, wanategemea uvuvi na kuna shughuli nyingi sana za kiuchumi. Kwa hiyo, Serikali iangalie namna sasa ya kuwekeza katika shughuli hizi za kiuchumi ili kuwasaidia wananchi waweze kuondokana na hali ya umasikini iliyokithiri katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiangalia katika Mkoa wangu wa Geita, shughuli za kiuchumi ambazo zinafanyika kwenye mkoa huu ni kilimo, uvuvi, lakini sasa katika uvuvi hakuna jitihada za dhati katika Serikali za kuweza kuwasaidia wavuvi. Wanafanya shughuli hizi za kiuvuvi bila kupata msaada wowote wa kuwawezesha wavuvi ili waweze kujikwamua katika hali ya umasikini waliyonayo. Kwa hiyo, niombe Serikali iweze kutoka na Mpango Mkakati kwa ajili ya kuwasaidia wananchi ili waweze kuondokana na hali ya umasikini wa kipato cha sasa hivi na waweze kujikwamua. Kwa sababu tunakoelekea Serikali tumesema kwamba tunahitaji Tanzania ipige hatua ili tuwe na uchumi wa kati, sasa hatuwezi kufikia kwenye uchumi wa kati bila kuweza kuwasaidia wananchi katika shughuli mbalimbali za kiuchumi walizonazo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nikizungumzia katika masuala ya uchimbaji wa madini, naomba pia Serikali iwekeze nguvu katika eneo hilo kwa sababu eneo hilo pia watu wanajishughulisha na shughuli hizo za uchimbaji wa madini. Kweli mmetenga shilingi milioni 900 lakini niombe Serikali ikiwezekana iongeze zaidi ya hapo, vilevile iweze kuwawezesha hata kielimu wananchi ili waweze kufanya shughuli hizi kwa ufanisi wa kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika upande wa afya, inaonyesha kabisa kwamba kweli katika upande wa afya bado changamoto ni kubwa sana hasa katika maeneo ya vijijini. Sera ya Taifa imezungumzia kwamba katika Mkoa tuwe na hospitali ya rufaa, katika Wilaya tuwe na Hospitali ya Wilaya, katika kata tuwe na kituo cha afya, vijijini tuwe na zahanati. Lakini hali halisi iliyoko kwa sasa inaonyesha jinsi ambavyo changamoto bado ni kubwa sana, unakuta vijiji vingi havina zahanati na ndiyo maana sasa katika harakati ya kuweza kupunguza vifo, hasa kwa watoto pamoja na akina mama wajawazito bado takwimu zinaonyesha kuwa ni juu sana.
Kwa hiyo, niiombe Serikali iangalie uwezekano mkubwa wa kuelekeza nguvu zaidi katika sekta hii ya afya ili kupunguza uwezekano wa vifo vya watoto pamoja na akina mama wajawazito. Kwa sababu haiwezekani unakuta wanawake, wanasafiri kwenda umbali mrefu sana kwenda kufuata huduma za afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hivyo katika zahanati hatuna wataalam wa kutosha, katika vituo vya afya wataalam wa afya ni wachache. Kwa hiyo, niiombe Serikali iangalie kwa kina katika mpango huu kuweza kuona kwamba basi iweze kuangalia uwezekano wa kuwasaidia kuongeza zaidi kasi na fedha nyingi kwa ajili ya kuwezesha kuweza kujenga zahanati za kutosha lakini vilevile kupeleka vifaa tiba katika vituo vya afya, zahanati, Hospitali za Wilaya na Mikoa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika mikoa mipya, natoka katika mkoa mpya, tunaomba Serikali iangalie mikoa hii. Kwa sababu ni mikoa mipya hatuna hospitali za rufaa, hata zile zilizopo ambazo zimetengwa kwa sasa bado zina changamoto kubwa sana, kwa hiyo niombe Serikali katika bajeti hizi iangalie uwezekano wa kuangalia mikoa hii kwa kina iweze kuhakikisha zinapata huduma, zinajenga hospitali hizi ili kuwawezesha wananchi katika mikoa hii kuweza kupata huduma iliyo bora. Lakini vilevile kuongeza vifaa tiba pamoja na wataalam ambao ni madaktari na watu muhimu ambao wanaweza wakasaidia wananchi. Tuna upungufu mkubwa sana wa wahudumu wa afya katika zahanati na katika hospitali hizi, mara nyingi watu wanakwenda kupata huduma, lakini wanachukua muda mrefu kuweza kupewa huduma kwa sababu tuna upungufu wa wataalamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niiombe Wizara inayohusika pia pamoja na Serikali kwa ujumla, hebu tuangalie namna ya kutatua changamoto hasa katika sekta ya afya ili wananchi waweze kupata huduma safi; mtu akiwa na afya atakuwa na uwezo wa kufanya kazi zake vizuri, usipokuwa na afya hata kazi huwezi ukafanya vizuri. Kwa hiyo, niiombe Serikali katika mpango wake huu iangalie namna ya kuboresha huduma za afya ili kuwawezesha wananchi kuweza kupata huduma bora, safi na hatimaye basi tuweze kuwa na afya njema hasa kwa wananchi wetu walioko vijijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika upande wa elimu, naona kweli kabisa Serikali imetenga fedha nyingi kwa upande wa elimu. Naomba hasa katika mikopo kwa wanafunzi, kuna wanafunzi wengi sana wanaotokea vijijini ambao hawapati mikopo hii. Namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Elimu kwa hatua anazozifanya kwa sasa kuweza kuiangalia sekta hii kwa undani.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Naunga mkono hoja, naomba Serikali iweze kuifanyia kazi.