Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mambo ya Nje ina mchango mkubwa sana katika kukuza uchumi, ustawi na maendeleo ya Taifa letu. Wizara hii ina wajibu mkubwa sana wa kutafuta wawekezaji walio makini, kutafuta wataalam na kujenga mahusiano kati ya nchi yetu na Mataifa ya nje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nalizungumza jambo hili kwa sababu kama kuna tishio kubwa la usalama wa Taifa letu na usalama wa Mataifa basi umaskini duniani ndiyo tatizo kubwa sana. Kwa hiyo, tunaitarajia Wizara ya Mambo ya Nje itekeleze wajibu huo kwa weledi ili nchi yetu iweze kupata matarajio hayo tunayoyatarajia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Mambo ya Nje imejitahidi kuwaunganisha na kuwashajihisha Watanzania wanaoishi nchi za nje kuwekeza ndani ya nchi yetu, kuleta utaalam na kutoa ushauri katika mambo ya kitaalam.
Kwa bahati mbaya kidogo, mchango wa Watanzania hao walioutoa si mkubwa wa kutosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nasoma hotuba ya Mheshimiwa Waziri hapa na ametueleza mchango ambao Watanzania walio nje waliutoa kwa nchi yetu ni takribani shilingi za Tanzania bilioni 36. Fedha hizi kwa maoni yangu ni kidogo sana ukilinganisha na wenzetu. Labda nitoe mfano wa wenzetu wa Kenya, mchango wa Wakenya wanaoishi nje ya nchi yao ni takribani dola bilioni moja. Kwa mnasaba huo basi nasema tunayo kazi ya ziada ya kuifanya ili kuwashajiisha Watanzania hawa waweze kutoa mchango mkubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa katika Bunge hili katika Bunge lililopita, moja ya malalamiko makubwa sana ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyaeleza ni mikataba yetu mingi ambayo tunaingia si mizuri. Kwa utafiti usio wa kina sana inaelekea utaalamu wetu katika kuingia makubaliano ya mikataba si wa kiwango cha juu sana. Kwa hiyo, naishauri Wizara ya Mambo ya Nje ifanye kila linalowezekana kukisaidia Chuo chetu cha Diplomasia ili kiweze kutoa mafunzo mazuri ya international negotiation. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikifuatilia mara nyingi utendaji wa Mashirika ya Kimataifa, najua Waheshimiwa Mabalozi wamefanya kazi nzuri sana nje ya nchi huko, lakini kama tutafanya ulinganisho wa mchango ambao Watanzania tumeutoa katika Mashirika ya Kimataifa, ukilinganisha na nchi kama Ghana, Senegal na Kenya, wataalam wanaofanya kazi katika mashirika hayo Watanzania ni wachache sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya, ukiwa huna wana diplomasia wa kutosha kwenye mashirika hayo, itakuwa vigumu sana kuweza kuwavutia watu wengine ndani ya nchi hata nafasi hizo zikitoka Watanzania wanakuwa hawapati taarifa za kutosha. Kwa hiyo, naishauri Wizara ifanye kila linalowezekana, kwanza tuwape Watanzania mafunzo ya kutosha lakini tuhakikishe kwamba Watanzania wengi zaidi wanafanya kazi katika Mashirika ya Kimataifa ili wawe chachu na wafungue milango kwa Watanzania wengine ambao wangependa kupata fursa hiyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, kwa bahati nzuri mimi ni miongoni mwa wanafunzi ambao walipitia Chuo cha Kidiplomasia na Mheshimiwa Shahari ni miongoni mwa Walimu ambao walitufundisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya sana inaonekana kama Chuo cha Diplomasia pamoja na mchango wake katika kuandaa Mabalozi na Maafisa wa Ushirikiano wa Kimataifa, Serikali haikiendelezi kiasi cha kutosha. Serikali na Wizara ya Mambo ya Nje imekuwa ikishauriwa kwa miaka mingi kukiimarisha Chuo cha Diplomasia kwa kukipatia vifaa na wataalam lakini pia kukipatia eneo ambapo chuo hiki kinaweza kikatanuliwa ili kiweze kutoa fursa nyingi zaidi. Kwa bahati mbaya takriban miaka kumi na tano eneo ambalo limetengwa kwa ajili ya chuo hicho bado halijaendelezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara ya Mambo ya Nje ikiunganishe Chuo cha Kidiplomasia na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ili kunyanyua hadhi yake. Kama ilivyo Taasisi ya Diplomasia na Ushirikiano wa Kimataifa Nairobi ilivyounganishwa na Chuo Kikuu cha Nairobi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana, naomba kuunga mkono hoja.