Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Stephen Julius Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. STEPHEN J. MASELE: Mheshimwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia hoja hii ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri ambayo imetoa dira ya nchi yetu inakoelekea hasa kwenye siasa za Kimataifa na diplomasia ya uchumi. Nitumie nafasi hii kumpongeza Naibu Waiziri Mheshimiwa Dkt. Susan Kolimba, Katibu Mkuu Dkt. Aziz na watumishi wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya ya kuitangaza nchi yetu na kuvutia uwekezaji katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu ina historia na ina historia kubwa hasa kwenye siasa za kimataifa. Tangu tupate uhuru chini ya uongozi wa Baba wa Taifa alijenga misingi imara ya kuhakikisha kwamba Tanzania inakuwa na sauti kwenye ukanda wa Kusini mwa Afrika na hasa kwenye masuala ya ukombozi wa Bara letu la Afirika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, misingi ile ilijengwa na msingi imara na unatakiwa kuendelezwa kwa kukifanya Tanzania kuwa nchi yenye sauti kubwa na ushawishi wa kisiasa na kiuchumi katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati na Kusini mwa Bara la Afrika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kupongeza uongozi mzima wa Wizara pamoja na Serikali kwa kushiriki kikamilifu kusuluhisha mgogoro wa Kongo (DRC). Wote hapa tunafahamu umuhimu wa Kongo (DRC), mahusiano yetu ya kindugu, ya kijamii na kiuchumi. Kwa hiyo, uhusiano na ushiriki wa Tanzania kuhakikisha kwamba nchi ya Kongo inapata amani ya kudumu ni jambo la kipaumbele kwa Tanzania na kwa Serikali yetu. Lakini hivyo hivyo niipongeze Serikali kwa kuhakisha kwamba Burundi inaendelea kuwa salama na Baba wa Taifa alieleza kabisa kwamba huwezi kuwa salama kama majirani zako wote hawako salama, na wote tunatambua umuhimu wa kiuchumi wa nchi hizi zinazotuzunguka kwa maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitajikita zaidi kwenye diplomasia ya uchumi ambayo mwelekeo wa Wizara na Serikali kwa sasa imeweka mkazo mkubwa kwenye diplomasia ya kiuchumi.
Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba zako zinazofuata ni vyema ukaja na takwimu uoneshe Watanzania mipango na safari na mikutano ya nje ambayo nchi yetu inashiriki imeleta faida gani kwa Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwa taarifa na Ripoti ya Uchumi ya Umoja wa Mataifa Tanzania kwa mwaka 2014 imeongoza kwa kuwa ni Taifa la kwanza kwenye Ukanda wa Afrika Mashariki kwa kuingiza mapato mengi ya uwekezaji wa fedha za kigeni kwa maana ya Foreign Direct Investments. Leo kwa ripoti ile Tanzania iliingiza zaidi ya dola za Marekani bilioni 2.14 ukilinganisha na Taifa ambalo lina uchumi mkubwa kwenye ukanda wetu la Kenya ambalo liliingiza dola milioni 900. Uganda ilifuatiwa ya pili nyuma ya Tanzania kwa kuingiza zaidi ya dola bilioni 1.1. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mafanikio Mheshimiwa Waziri, kwa sababu haya ndio majukumu ya Wizara yako kwa shughuli zote zinazohusiana na uchumi wa Taifa hili na hasa uwekezaji kutoka nje na ukitazama katika uwekezaji huu unaona kabisa ni Sekta ya Gesi, Sekta ya Madini kwa Tanzania ndio imeongeza kwa kuingiza mapato mengi ya uwekezaji baada ya kugundua gesi asilia, Taifa letu limeingiza mapato mengi ya kigeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ni vyema sasa kuangalia ushiriki wetu kwenye majukwaa mbalimbali ya kiuchumi kwa mfano tunaposhiriki kwenye Jukwaa la Kiuchumi la TICAD kwa mahusiano ya Japani na Afrika ama India na Afrika, ama Marekani na Afrika, na block zingine za kiuchumi kwa mfano block ya BRICS lazima tuoneshe kwa takwimu tunapata faida gani. Taifa linapata mapato kiasi gani kutoka nje kwa maana ya uwekezaji unaotoka nje. Hiyo itaweza kuonesha uhalali wa safari ambazo tunakuombeeni fedha mnazokwenda nje na huwezi kuwa mwana diplomasia ambaye unaishia kwenda Shinyanga badala ya kwenda nje kutafuta uwekezaji kwa faida ya Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima niseme kwamba ukitazama kama nilivyoeleza awali, Sekta ya Nishati kwa maana ya utafiti na gunduzi za gesi na madini ndio zimeongeza mapato mengi ya kigeni hasa katika uwekezaji. Je, Wizara inajipangaje sasa kuhakikisha kwamba sekta zingine kama Sekta ya Kilimo na Viwanda inafanya vizuri kuwekeza, kuingiza fedha nyingi za kigeni.
Ukitazama kama Ethiopia imefanikwa sana kwenye viwanda hasa kwenye maeneo ya kilimo, imefanikiwa sana kuvutia uwekezaji kwenye kilimo na viwanda ambayo imechangia mapato makubwa ya Uwekezaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kama Afrika Kusini ambayo ndio inaongoza kwa Afrika kwa zaidi ya dola bilioni 145 za uwekezaji ambazo imepokea, imewekeza zaidi kwenye Sekta ya Viwanda, Biashara pamoja na Madini. Sasa Sekta zingine zinasubiri nini! Je, wizara yako inawezaje kusaidia kutafuta wawekezaji zaidi wa kuongeza mapato na uwekezaji katika sekata za Kilimo, biashara pamoja na viwanda katika nchi yetu.
Mheshimiwa Rais amesema anataka Tanzania iwekeze zaidi kwenye viwanda. Je, Wizara yako inafanya nini na hawa wawekezaji wanaokuja kuwekeza hapa baada ya kuwekeza je, Wizara yako inafuatilia kuona wanaendeleaje? Maana wawekezaji wengine wanakuja kwenye sekta hizi mbalimbali lakini wanaishia kuchanganyikiwa, wanaishia kuwa frustrated na mazingira mengine ya uwekezaji. Je, Wizara hii inafuatilia kujua wanaendeleaje? Na kama kuna changamoto ambazo zinawakabili mnafanya nini kuhakikisha kwamba mnashirikiana na sekta zingine kuhakikisha changamoto hizi mnazitatua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kabisa kwamba Taifa lolote duniani haliwezi kuendelea bila uwekezaji, hasa uwekezaji wa fedha zinazotoka nje. Marekani yenyewe inashika nafasi ya tatu kwa kupokea fedha nyingi za uwekezaji kutoka mataifa mengine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, China imeendelea kwa sababu imepokea fedha nyingi za uwekezaji kutoka mataifa mengine, na kutoka ndani ya China wenyewe. Lakini Tanzania tunapovutia wawekezaji lakini tunatumia muda mwingine kuwa-frustrate wawekezaji na kuona kama ni maadui ama wezi wa mali za asili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni wajibu wetu kuwa na sheria nzuri, ni wajibu wetu kusimamia vizuri rasilimali zetu, lakini taifa hili linahitaji kuendelea, Taifa hili linahitaji kuwa Taifa la uchumi wa kati ifikapo mwaka 2025. Hatuwezi kuwa na uchumi wa kati mwaka 2025 kama dira ya Taifa ya uchumi ya maendeleo inavyoelekeza kama hatutoweza kuvutia uwekezaji kutoka nje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri, badala ya kufanya siasa, badala ya maelezo mengi, next time uje na data, uje na figures uoneshe faida, ya kushiriki kwenye mikutano hii yote, Taifa linapata nini. Uoneshe fedha tunazozipokea kutoka Asia, Marekani, Uingereza katika uwekezaji, wala sio fedha za misaada, nazungumzia fedha za uwekezaji ambazo zinaongeza mzunguko wa uchumi katika Taifa letu. Leo katika mradi wa bombo la gesi tu, tulipokea zaidi ya dola bilioni 1.2, dola bilioni 1.2 imetumika hapa Tanzania, na makampuni ya kitanzania yamepata fedha, na mzunguko wa fedha umemfikia kila mwananchi wa Tanzania.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja asilimia mia moja, na nampongeza Waziri na Wizara yake. Yeye ni mzoefu nina uhakika kwamba atalisaidia Taifa hili, kuhakikisha heshima ya Tanzania, kwenye nyanja za kimataifa inaendelea kuwepo.