Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nitoe shukrani zangu za dhati kwako kwa kuniona. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema kuweza kuzungumza kwa mara nyingine kwa niaba ya wananchi wangu wa Jimbo la Rufiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nianze kwa kusema kwamba maji ni miongoni mwa mambo ya msingi kabisa ambayo yameainishwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2015/2020. Ukisoma ukurasa wa 86 wa Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi unazungumzia mchakato huu wa kusogeza karibu huduma za kijamii, lakini pia tatizo la maji katika Jimbo langu la Rufiji ni kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda siku zote nimekuwa nikisimama nikizungumza kwa masikitiko, lakini pia hata katika hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri sijaona sehemu yoyote katika hotuba yake kuzungumzia Rufiji kwa ujumla. Tatizo la maji Jimbo la Rufiji ni kubwa sana. Labda niseme tu kwamba ni asilimia tano tu ya wananchi wa Jimbo la Rufiji ambao wanapata maji safi na salama na hata hii asilimia tano ambayo tunaizungumzia ni katika Kata ya Utete tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepata tatizo la maji Tarafa ya Ikwiriri na tumepeleka maombi kwa Katibu Mkuu kuhusiana na ukarabati wa moter ambayo imeharibika kwa muda mrefu toka mwezi wa Kumi na Mbili, lakini mpaka hii leo tunavyozungumza tatizo la maji bado lipo. Shilingi milioni 36 ambayo tuliiomba Wilaya ya Rufiji kwa ajili ya ukarabati wa moter katika Kata hii, Tarafa hii ya Ikwiriri mpaka leo hatujapata.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukiangalia kiundani, Rufiji sisi hatukupaswa kuwa na tatizo la maji kwa sababu kwanza tuna Mto Rufiji ambao una uwezo wa kusogeza maji maeneo yote. Ni masikitiko makubwa, toka Adam na Hawa, mto huu haujawahi kutumika, siyo kwa kilimo wala siyo kwa maji tuweze kutumia wananchi wa Jimbo la Rufiji, lakini pia mto huu kama ungeweza kutumika vizuri, Wilaya ya Kibiti ingeweza kupata maji safi lakini pia Wilaya ya Mkuranga, Wilaya ya Kilwa na Wilaya ya Kisarawe zingeweza kupata maji safi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni masikitiko makubwa. Niliwahi kuzungumza na Waziri wa Wizara hii akaniambia kwamba kwa sasa hivi Mto Rufiji hautatumika kwa sababu wanategemea visima ambavyo vimechimbwa. Sasa unajiuliza; tunaeleka wapi? Tunategemea maji ya visima ambavyo vinaweza vikakauka wakati wowote!
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Wizara hii, nina fahamu kwamba Serikali yangu inachapa kazi na siwezi kupingana na ndugu zangu hawa Wahandisi ambao Mheshimiwa Rais amewateua katika Wizara hii. Ninachokiomba kwa mwaka unaofuata, basi Wizara hii iweze kutufikiria sisi wananchi wa Pwani kwa sababu naamini iwapo Serikali itaweka mpango mzuri kwa ajili ya kusaidia wananchi hawa hususan kwenye jambo hili la maji, basi hata Dar es Salaam itapata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua matatizo ya maji siyo Rufiji tu, ukienda Temeke leo hii maji hakuna; ukienda Mbagala maji hakuna; ukienda Kigamboni kwenyewe maji hakuna; maji kidogo ambayo yanapatikana yanasaidia maeneo ya Upanga, Oysterbay na maeneo mengine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara hii itusaidie. Leo hii tunachukua maji kutoka Kanda ya Ziwa tunaleta mpaka Tabora, zaidi ya kilometa 500, lakini ukisema uchukue maji ya Mto Rufiji uyasambaze maeneo ya Rufiji, Mkuranga, Kisarawe, Kibiti na maeneo mengine ya Dar es Salaam haitagharimu zaidi ya kilometa 200 kwa sababu kutoka Dar es Salaam mpaka Rufiji ni kilomtea 160 tu! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara hii, ni kwa muda mrefu sasa sisi wananchi wa Jimbo la Rufiji na Pwani tumenyanyasika kwa muda mrefu sana. Naamini ujio wangu Bungeni hapa basi itakuwa ni fursa kwa wananchi wangu waweze kufurahia usururu wangu, kwa sababu mimi najiita sururu kutokana na uchapakazi wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara hii sasa itusaidie. Matatizo ya maji yako katika kata zangu zote, tukiondoa Kata moja tu ya Utete. Kata ya Ngarambe wananchi wangu wanakanyagwa na tembo kwa sababu tu ya kwenda kutafuta maji; Kata ya Mbwala wananchi wanalazimika kusafiri umbali wa zaidi ya kilometa tano kufuata maji; lakini pia hata kata nyingine zote hakuna maji safi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri aweze kutusaidia, tuingie katika mpango ili mradi mkubwa uweze kutokea pale katika Mto wa Rufiji tuweze kupata maji safi ambayo yataweza kusaidia wananchi wetu wa maeneo mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini iwapo tutatekeleza hili, tutakuwa tumetekeleza Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi na hii itatusaidia sana kuondoa kero kubwa ya wananchi ambayo imekuwa ni kilio cha muda mrefu. Masikitiko yangu kwa Rufiji nimekuwa nikiyazungumza kwa muda mrefu, inawezekana labda wenzangu walikuwa wakitoa malalamiko haya, hayafanyiwi kazi, lakini namwomba Mheshimiwa Waziri, mimi na Naibu Waziri tumekaa kwa muda mrefu sana tumekuwa tukizungumza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nitoe shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Naibu Waziri wa Wizara hii kwa namna ambavyo amekuwa akichapa kazi. Namwomba apate muda ili aweze kufika Rufiji ajionee kero hizi za wananchi. Leo hii watoto wanashindwa kwenda shule ili waweze kufuata maji kwenye maeneo ambapo kuna mito. Katika maeneo hayo ambayo inabidi waende kufuata maji kuna hatari nyingi. Kuna wengine ambao wanaliwa na mamba, lakini pia inasababisha watoto washindwe kwenda shule kwa sababu ya kwenda kutafuta maji. Wanasafiri zaidi ya kilometa tano, kilometa sita kwenda kufuata maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu kubwa leo hapa ni kumwomba Mheshimwa Waziri; nafahamu katika kitabu hiki, katika hotuba ya leo hajazungumza lolote kuhusiana na Rufiji. Hata kiasi cha fedha ambacho wamekitenga kwa ajili ya Rufiji, shilingi milioni 460 ni kiasi kidogo sana ambacho hakitaweza kutatua kero za maji katika Jimbo la Rufiji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nikumbushe tu, Jimbo la Rufiji na Wilaya ya Rufiji ni kubwa kuliko Mkoa wa Kilimanjaro. Eneo la Rufiji ni zaidi ya square kilometa 13,600 ambayo ni sawasawa na Mkoa wa Kilimanjaro; lakini utajionea kwamba Rufiji tunapata maji asilimia tano tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nawaomba Waheshimiwa Mawaziri, nafahamu wanachapa kazi sana, katika mpango unaokuja waweze kufikiria Rufiji ili kuwasaidia wananchi wangu wa Jimbo la Rufiji kuondoa kero kubwa ya maji ambayo ni kilio na imekuwa ni aibu kwa muda mrefu. Kwa sababu ukianza kuzungumza matatizo ya maji Rufiji wakati tuna Mto Rufiji ambao leo hii wananchi hawawezi kusogea kutokana na hatari ya mamba, kwa kweli ni masikitiko makubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, yangu ni hayo. Naiomba Wizara ichape kazi kuweza kutusaidia wananchi wa Jimbo la Rufiji, Kibiti, Kilwa ambao tuko karibu; na naamini iwapo mradi huu utatekelezwa na Serikali basi tutaweza kutatua kero ya maji kwa maeneo yote ya Pwani mpaka Dar es Salaam ambako tunaamini kwamba hivi visima ambavyo leo hii Mheshimiwa Waziri anasema kwamba anachimba visima kwa ajili ya Dar es Salaam, ipo siku vitakauka. Sasa sioni sababu ni kwa nini tusichukue maji ya asili ambayo yapo; yalikuwepo toka Adamu na Hawa ambayo hata leo hayajawahi kutumika. Hayajatumika katika irrigation na hayajatumika katika maji safi ya kunywa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, basi naomba Wizara hii iweze kufikiria. Naamini kabisa hata kama utakuwa na PhD lakini unafikiria visima, ukashindwa kufikiria maji ya asili ya Mto Rufiji, kwa kweli naona kuna matatizo. Labda kama Wizara ituambie kuna mpango mkakati wa kuamua kuitenga Rufiji kwa sababu mambo haya nimekuwa nikiyazungumza kwa muda mrefu sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara hii sasa kukaa na Wataalam kufikiria mradi mkubwa wa maji ambao utaweza kusaidia watu wa Pwani na maeneo mengine ya Dar es Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nashukuru na naunga mkono hoja.