Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Wizara ya Maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri ambayo ameiwasilisha mbele zetu siku hii ya leo. Wote tunafahamu kwamba maji ni tatizo kubwa sana hasa katika vijiji vyetu. Nikiangalia katika Jimbo la Busanda, kero kubwa iliyopo kule ni maji. Nikiangalia kwenye Vijiji na Miji ambayo inachipukia naona jinsi ambavyo wananchi wanahangaika sana kwa suala la maji. Vile vile kwenye vituo vya afya, zahanati, shuleni za msingi, changamoto ni kubwa sana ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kuona changamoto hii kubwa ya maji, ni kweli kwamba kuna miradi mbalimbali ambayo ipo hasa hasa katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, kuna Mradi wa Maji wa Benki ya Dunia ambapo ni vijiji kumi na kati ya vijiji kumi, vijiji kama saba viko katika Jimbo la Busanda. Nasikitika kwamba mradi huu umekuwa ni wa muda mrefu sana, yaani haukamiliki, unaendelea tu kila mwaka, lakini hatuoni kukamilika kwake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitumie fursa hii sasa kuiomba Wizara, Mheshimiwa Waziri wa Maji, hebu sasa mradi huu wa Benki ya Dunia katika vijji saba ambapo katika Jimbo langu mradi uko katika Kata ya Nyakagomba na vijiji vyake ambavyo vimezunguka kata hiyo; vile vile Katoro na Kata ya Nyamigota. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, kwamba sasa ifike mahali mradi huu ukamilike ili wananchi waweze kunufaika na mradi huu wa maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa nikiangalia katika kitabu cha bajeti, nimeuangalia huu mradi kwa kweli sijaona. Sasa sijui fedha hizo zimejificha wapi? Naombe sasa nihakikishiwe na Mheshimiwa Waziri kwamba mradi huu wa Benki ya Dunia unakamilika ili wananchi waweze kunufaika na huduma ya maji katika maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kumekuwa na ahadi ambayo ni ya muda mrefu ya mradi mkubwa wa maji kutoka Chankorongo, kutoka Ziwa Victoria. Mradi huu unakusudia kupeleka maji katika maeneo mbalimbali hasa katika Tarafa ya Butundwe ambapo ina miji mingi kama Mji wa Katoro na Buselesele pale ambapo kuna population kubwa, watu ni wengi; wanafika watu zaidi ya 100,000. Kwa kweli mahitaji ya maji ni makubwa sana. Tukiamua kukamilisha mradi huu wa Chankorongo, nina uhakika tatizo la maji kwenye Jimbo la Busanda litakuwa ni mwisho.
Mheshimiwa Mweyekiti, kwa hiyo, naishauri Serikali sasa kupitia Wizara ya Maji, ihakikishe mradi huu wa Chankorongo unafanyiwa kazi. Nimeangalia kwenye kitabu cha bajeti sijaona mradi huu, lakini nitumie fursa hii kuomba sasa Wizara iweke msisitizo wa kuuwezesha huu mradi wa Chankorongo uweze kufanyiwa kazi kwa ajili ya manufaa ya wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nilipokuwa nikisoma kitabu cha bajeti, nimeona kuna miradi ya quick wins ambapo pale Katoro na Buselesele wametenga shilingi milioni 500. Ni kweli shilingi milioni 500 tunashukuru kwamba zimetengwa, lakini sina uhakika kama hizi fedha mmepanga kufanyia nini pale.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusisitiza kwamba hizo shilingi milioni 500 na pengine zingeongezwa fedha zaidi, ufanyike ule mradi wa Chankorongo ili kuvuta maji kutoka Ziwa Victoria, tutaweza kumaliza kabisa tatizo hili; lakini kwamba shilingi milioni 500 tunachimba visima, kweli visima vinachimbwa, lakini havitoshelezi kutokana na wingi wa watu katika eneo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali sasa iangalie mradi wa Chankorongo wa kuvuta maji Ziwa Victoria. Nasema hivyo kwa sababu Jimbo la Busanda na Geita kwa ujumla tumezungukwa na Ziwa Victoria. Ni aibu pia kuona kwamba hatuna maji na wananchi wanahangaika, akina mama wanahangaika, hakuna maji. Ifike mahali sasa Serikali iwekeze kama ilivyopeleka maji kule Shinyanga na maeneo mengine ya Tabora kutoka Ziwa Victoria, sisi tumezungukwa na Ziwa, moja kwa moja. Yaani tunagusa Ziwa Victoria lakini hatuna maji. Kwa hiyo, naomba Serikali basi iangalie uwezekano wa kuvuta maji Ziwa Victoria ili wananchi waweze kunufaika na rasilimali maji ambayo imetuzunguka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kama nilivyosema kwamba changamoto ya maji ni kubwa, lakini napenda kuishauri Serikali kwamba tuanzishe hata Wakala wa Maji Vijijini kama ambavyo kuna REA kwenye umeme. Tukianzisha pia Wakala wa Maji Vijijini kama vile ilivyo REA nina uhakika kwamba changamoto ya maji itaweza kutatuliwa. Tunaona jinsi ambavyo REA inafanya kazi zake vizuri na tunaona kabisa na impact na vijiji vinapata umeme wa uhakika. Kwa hiyo, tukianzisha Wakala wa Maji Vijijini, nina uhakika pia tutaweza kutatua changamoto hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuongezea hapo, naomba sasa kwa sababu kumekuwa na tozo kwenye REA, sh. 50/= kwenye mafuta, kwa hiyo, naomba ile tozo iongezeke ifike sh. 100/= kama ambavyo wenzangu wamesema ili tuone kabisa umuhimu wa tatizo la maji, maana ni tatizo sugu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia hapo wachangiaji walioomba tu kwenye maji humu Bungeni; yaani kila mtu ni kilio kikubwa, kila mtu anataka achangie hii hoja ya maji, kwa sababu ya umuhimu wake. Kwa hiyo, naiomba Serikali hebu ilifanyie kazi suala hili, ikiwezekana tuongeze tozo iwe sh. 100 kwenye mafuta ili kuona kwamba suala la maji tunalipa kipaumbele kwa uhakika ili wananchi waweze kunufaika, kwa sababu tunajua maji ni uhai, hatuwezi kuwa na viwanda bila kuwa na maji na katika hospitali zetu tunahitaji maji, nasi wenyewe wananchi tunahitaji maji safi na salama. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kama alivyotembelea Mji wa Geita tukazindua maji pale tarehe 5 Januari, namwomba Mheshimiwa Waziri hebu apange basi aje ziara na Jimbo la Busanda aone jinsi ambavyo watu wanahangaika na suala la maji. Mheshimiwa Waziri najua akifika pale na kuona changamoto hiyo, nina uhakika kwamba tutaweza kupata sulution ya changamoto hizi ambazo ziko katika eneo hilo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu katika Jimbo langu kuna centers nyingi ambazo zina watu wengi kutokana na shughuli za uchimbaji wa madini. Watu wanashughulika na mambo ya madini, kwa hiyo, watu ni wengi, population ni kubwa sana. Mara nyingi kutokana na shughuli za madini, wakati mwingine kuna uchafuzi pia wa vyanzo vya maji na kwa sababu hiyo tunaomba Serikali sasa iangalie uwezekano wa kuongeza bidii kuwezesha ili tuweze kupata maji ya uhakika. Waweke visima na ikiwezekana kuvuta maji Ziwa Victoria; nina uhakika tutaweza ku-solve tatizo la maji katika Jimbo la Busanda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naiomba Serikali iweze kuanzisha Wakala wa Maji. Hili litaweza kutusaidia tuongeze tozo ili kuhakikisha kwamba tatizo la maji linakwisha kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, nikizingatia kwamba Waziri aweze kutekeleza kulingana na bajeti ambayo amepewa. Ahsante sana.