Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Ukerewe kama kisiwa inaweza kuwa chanzo kikubwa cha utalii endapo vyanzo kadhaa katika Wilaya hii vitawekwa sawa na kujengewa mazingira mazuri ya kutembelewa na watalii.
(a) Mapango ya Handebezyo ni mapango ambayo watu wa kale waliyatumia kwa ajili ya kujilinda na kufanya shughuli nyingine mbalimbali wakati wa mashaka kiusalama. Halmashauri ya Wilaya imekuwa ikijitahidi kuyahifadhi mapango haya yaliyoko Kata ya Nduruma.
(b) Nyumba ya Ghorofa ya Chifu Lukumbuzya ni jengo lililokuwa linatumika kama makazi ya Chifu wa Wakerewe, Chifu Lukumbuzya. Hiki kimekuwa kivutio kutokana na muundo wake ikilinganishwa na nyakati za ujenzi wake. Jengo hili liko katika kijiji cha Bukindo na limekuwa likivutia watu wengi, lakini faida yake kwa Taifa haina tija.
(c) Ufukwe wa Rubya ni ufukwe wa aina yake ulioko katika Kata za Ilangala na Muriti ambao umekuwa ni kivutio kikubwa sana kwa watu mbalimbali, kitu ambacho kama Wizara itaweka nguvu yake, basi kinaweza kuwa chanzo kingine kizuri cha mapato kupita utalii.
(d) Katika Kisiwa cha Ukara, Wilayani Ukara kuna jiwe ambalo ni la kimila na ambalo linasimamiwa na moja ya familia zilizoko katika kijiji cha Nyamangana. Jiwe hili limekuwa ni moja ya maajabu ambayo yamekuwa yanavutia watu wengi wanoenda kushuhudia kile kinachotokea. Bahati mbaya limekuwa halitangazwi sana kiasi kwamba ukiachilia mbali watu walioko kule Ukara ni watu wachache kutoka nje ya Wilaya wanaojua jambo hili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Wizara kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe itumie wataalam wa utalii utembelee vivutio hivi na kufanya maboresho na kuvitangaza ili Taifa liweze kufaidika kupitia mapato yatakayotokana na vyanzo hivi (vivutio) vya utalii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, uharibifu wa wanyama kama viboko, limekuwa ni tatizo na kikwazo kikubwa cha maendeleo ya wananchi katika Kata za Nduruma, Bukindo na Kagunguli. Tatizo hili kwa kuwa ni la muda mrefu na Halmashauri imeshindwa kulidhibiti, basi naomba Wizara ichukue hatua za haraka kudhibiti na kunusuru hali hii.