Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mchango wangu nianze katika sekta ya utalii. Juhudi ya Serikali katika kutengeneza vivutio vya utalii bado siyo wa kuridhisha kwani kuna vivutio vingi bado hatujaweza kuvitambua na kuvitangaza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu malikale, ukanda wa Kusini kuna vivutio vya malikale kama vile Boma la Mdachi (Wajerumani) lililojengwa miaka ya 1904 -1907 wakati wa vita vya Majimaji Mjini Liwale. Ndani ya boma hili kuna mabaki ya sanamu na michoro ya watumwa kwa ajili ya biashara ya utumwa.
Vilevile katika ukanda wa Liwale kuna milima ya Rondo yenye misitu na vipepeo ambao hawapatikani popote duniani. Tunayo pia bwawa la Mlembe na Kiulumila. Haya ni mabwawa yenye mamba na viboko wenye kuwasiliana na wazee wa mila zetu.
Kuhusu ulinzi wa misitu yetu siyo wa kuridhisha. Kuna Mamlaka ya Uvunaji wa Mali ya Misitu (TFS). Taasisi hii imekuwa kero kubwa kwa watu wanaokaa karibu na hifadhi zetu. Badala ya kuwa na wastawishaji wa misitu wamekuwa waharibifu wakubwa wa misitu yetu. TFS wanatuhumiwa kila mahali kuwa wao ndiyo waharibifu wakubwa wa misitu yetu. Kazi kubwa inayofanywa na watu hawa ni kugonga mihuri tu na kusafirisha mazao ya misitu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu migogoro ya mipaka, kumekuwa na migogoro mingi ya mipaka kati ya hifadhi zetu na wanavijiji. Hali hii huchangiwa sana na watendaji wa hifadhi kusogeza mipaka bila kushirikisha jamii husika. Mfano mgogoro wa kijiji cha Kikufungu Wilayani Liwale uliosababishwa na wahifadhi kuhamisha mpaka wa hifadhi bila kushirikisha jamii. Mgogoro huu una zaidi ya miaka kumi sasa. Hadi sasa zaidi ya watu wanne wamepoteza maisha na kuharibu kabisa mahusiano ya askari wa hifadhi na wanakijiji. Aidha, kijiji cha Ndapata wako watu wawili wamepoteza maisha kwa sababu ya mgogoro huu wa mipaka.
Kijiji cha Kichonda Mwenyekiti wa Kitongoji mwezi wa 8 mwaka 2015 amekatwa mikono na askari wa wanyamapori hadi leo hakuna kesi wala fidia juu ya kadhia hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Lindi sehemu kubwa ni sehemu ya Selous lakini kwa masikitiko makubwa Mkoa huu hauna manufaa yoyote na Selous. Mkoa wa Lindi hasa Wilaya ya Liwale hakuna hoteli ya kitalii Mkoa wa Lindi pia kiwanja cha ndege cha Mkoa wa Lindi hakijapanuliwa na kuwa na hadhi ya kuwezesha ndege kubwa kutua.
Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Nangurukuru - Liwale ndiyo barabara ingewapeleka watalii kwenye hifadhi hiyo. Kanda ya Kusini haina Chuo cha Misitu Kanda nzima. Eneo kubwa la Hifadhi ya Selous ipo Mkoa wa Lindi Wilaya ya Liwale. Kuhusu ulinzi shirikishi, Serikali imeweza sana kwenye ulinzi wa silaha na mabavu kama njia pekee ya kulinda hifadhi zetu, jambo ambalo halina tija kubwa zaidi ya kuongeza uhasama baina ya wahifadhi na jamii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu katika hili Serikali ijikite zaidi katika kutoa elimu juu ya ulinzi shirikishi sambamba na kuwaonyesha wananchi faida itokanayo na hifadhi zetu. Kwa mimi nadhani walinzi wa kwanza wawe wale watu wanaozungukwa na hifadhi husika badala ya kutumia silaha zaidi na kuendelea kuua watu na kuongeza uhasama. Mkoa wa Lindi hatujaona faida ya moja kwa moja inayotokana na hifadhi ya Selous zaidi ya kushuhudia mauaji.
Kuhusu uhaba wa watumishi na vitendea kazi, kwa Wilaya ya Liwale uhaba wa watumishi wa wanyamapori kumesababisha hasara kubwa sana kutokana na wanyama kuharibu mashamba ya wakulima. Ukienda kutoa taarifa watakujibu hawana gari au watumishi wa kwenda kuwasaidia watu hao wa vijiji vya Mpigamiti, Barikiwa, Kimambi, Kikulyungu na Ndapata wanakabiliwa na njaa mara kwa mara kutokana na mazao yao kuliwa au kuharibiwa na wanyama kama tembo na nguruwe. Nguruwe wamekuwa ni tishio kubwa sana kwa wakulima wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la watu kuliwa na simba Wilayani Liwale ni kubwa sana hasa baada ya watu kunyang‟anywa silaha zao kwenye Operesheni Tokomeza. Wizara ifikirie namna bora ya kuanza kurudishiwa silaha watu wale ili zisaidie kuimarisha ulinzi vijijini hasa zile silaha ndogo ndogo. Naomba kuwasilisha.