Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kwa mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kuchangia Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya, nimpongeze Rais, Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri na pia kwa uteuzi wa viongozi wa Wizara ya Maliasili na Utalii. Nimpongeze Waziri Mheshimiwa Profesa Jumanne Maghembe na Naibu Waziri Mheshimiwa Engineer Ramo Makani na Katibu Mkuu - Meja Jenerali Gaudence S. Milanzi kwa kuongoza Wizara hii nyeti na maalum katika Taifa letu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie katika baadhi ya maeneo na kushauri kutokana na maoni yangu na mengine ya kutoka kwa viongozi wa Wilaya na Mkoa wetu wa Manyara. Niombe Wizara ya Maliasili na Utalii isaidie Halmashauri zetu ambazo zina hoteli za kifahari na camp sites ambazo kisheria wanatakiwa kulipa ushuru wa huduma (service levy) asilimia 0.3 ya mapato yao hadi leo wamekataa na walienda mahakamani na kushindwa kesi, wamekata rufaa katika Mahakama ya Rufaa. Mapato mengi tunapoteza na hasa Halmashauri zetu zinazotegemea mapato hayo. Wizara inaweza kukaa na chama cha wenye Hoteli Tanzania (HATS) na kuleta suluhisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, katika WMA nyingi tunapokusanya mapato ya utalii, fedha hizo ambazo hugawanywa kwenda Taifa, Halmashauri na vijiji husika WMA huenda baada ya kukusanywa katika WMA zetu na kupelekwa hadi Taifa, baada ya hapo hurudishwa chini tena. Tunaomba zile za Halmashauri na WMA zibadilishwe na gawio la Taifa ndiyo pekee liende.
Tatu, leo ni mwaka wa tatu, kifuta jasho na kifuta machozi wananchi wa Babati hawajalipwa pamoja na kufuatilia Wizarani mara kadhaa nikiwa na Mkurugenzi na Mwenyekiti wa Halmashauri hadi leo shilingi milioni 12 tu kati ya hizo zimelipwa. Nashauri badala ya Wizara kupitia kitengo cha wanyamapori kulipa hizo gharama za kufuta machozi na vifuta jasho, hifadhi husika mfano, TANAPA, Ngorongoro Conservation Authority ndiyo walipe. Tubadilishe sheria yetu ili malipo haya yaende kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nne, naomba miradi ya kusaidia vijiji vinavyopakana na hifadhi zetu mfano, TANAPA, NCA, KINAPA ziwe zaidi ya kulenga mtu mmoja mmoja katika miradi ya kuwaongezea mapato. Wakiwa na uchumi mzuri basi wao wataweza miradi ya sasa kwa mfano, ujenzi wa madarasa, mabweni, zahanati na wataalam wamenufaika moja kwa moja, watu kuwa walinzi wazuri na watetezi wa hifadhi zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tano, tunashauri matokeo ya Tume ya Kimahakama au Kijaji kufuatilia suala la mauaji ya Operesheni Tokomeza yatolewe mapema. Imani ya wananchi kuwa sheria itachukua mkondo wake na haki itendeke.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sita, tunaomba suala la vijiji vya Ayamango, Gedemas na Gidejabung, Wilayani Babati sasa vipatiwe ufumbuzi wa kudumu. Wananchi waliopewa ardhi hiyo kisheria na baadaye kujikuta wako ndani ya Hifadhi ya Tarangire. Aidha, walipwe fidia ya ardhi, wapewe fedha ili wajitafutie ardhi wenyewe. Wapatiwe ardhi mbadala na kama haiwezekani wapewe hiyo ardhi yao waliyotumia miaka zaidi ya 30.
Mheshimiwa Mwenyekiti, saba, eneo la Tarangire na vijiji vya Ayamango, Gedemas na Gedejabung wapewe wafugaji kwa malisho kwa mkataba maalum. Miundombinu ya josho na malambo yawekwe, idadi maalum ya mifugo iruhusiwe hapo (carrying capacity) na wachunge kwa miezi sita, Januari hadi Juni na kutoka Julai hadi Disemba mifugo irudi vijijini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nane, eneo la kisheria la Burunge Game Controlled Area na zingine kama hizo zifanyiwe marekebisho yanayoendana na wakati. Leo hii kuna vijiji na miji mingi kutoka Manyoni, Minjingu, Mdorie, Magugu, Mamire, Galapo, Kash hadi maeneo ya Kondoa yapo humo, kisheria imekaa vibaya na itaweza kuleta athari.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tisa, Tanzania Forest Service Agency inakusanya mapato mengi yanayotokana na maliasili ya misitu, magogo, mkaa, mbao, nta, asali na kadhalika. Kwa mwaka takribani bilioni 45 hadi bilioni 50, lakini hakuna fedha hata kidogo inayoenda kupanda miti na kurudishiwa pale palipovunwa. Nashauri asilimia 30 ya mapato hayo yaende kwenye Mfuko wa Taifa wa Mazingira ili itumike kupanda miti, kuboresha upatikanaji wa mbegu za miti mbalimbali na utoaji wa elimu kwa jamii. Taasisi ya Taifa ya Miti (National Tree Centre) pia wana hali mbaya kifedha hii michango itaweza kusaidia kueneza elimu na mbegu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumi, nashauri uwindaji wa kitalii upigwe marufuku kwa muda angalau miaka kumi ili wanyamapori wetu waweze kurudi kama zamani. Nashauri hadi kwenye zana na vifaa vya ufugaji wa nyuki na kusindika asali iondolewe ili kukuza sekta hii na kupata viwango vizuri (quality).
Mheshimiwa Mwenyekiti, kumi na mbili, tozo mpya ya maliasili kwenye vinyago katika viwanja vya ndege iondolewe.